Tanganyika Rifles ilikuwa jina la jeshi la Tanganyika kuanzia uhuru wa nchi mwaka 1961 hadi uasi wake na mwisho mwaka 1964. Iliendeleza mfumo wa King's African Rifles wa awali. Nafasi yake baada ya 1964 ilichukuliwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.

Historia ya Tanzania
Coat of Arms of Tanzania
This article is part of a series
Uendo
Historia ya Zanzibar
Afrika Mashariki 1800-1845
Ukoloni
Afrika ya Mashariki ya Kijerumani
Mkataba wa Zanzibar-Helgoland
Mkwawa
Vita vya Maji Maji
Vita vikuu vya kwanza Afrika Mashariki
Tanganyika
Mapambano ya uhuru Tanganyika
Uhuru
Uhuru wa Tanganyika
Mapinduzi ya Zanzibar
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar
Julius Nyerere
Ujamaa
Tamko la Arusha
Vita vya Kagera
Ali Hassan Mwinyi
Benjamin Mkapa
Jakaya Kikwete
John Magufuli
Samia Suluhu Hassan

Tanzania Portal

Historia hariri

Tanzania bara ilipata uhuru wake kutoka ukoloni wa Kiingereza mwaka 1961 kwa jina la Tanganyika. Zanzibar bado ilikuwa nchi ya pekee.

Hadi mwaka ule kulikuwa na jeshi la kikoloni katika Afrika ya Mashariki lililokuwa la askari Waafrika waliosimamiwa na maafisa Waingereza na jeshi hilo liliitwa King's African Rifles (KAR). Vikosi viwili vya jeshi hili ambavyo askari hao waliwahi kuajiriwa katika eneo la Tanganyika vilitengwa na KAR na kukabidhiwa kwa taifa jipya. Kikosi cha Dar es Salaam kiliitwa sasa "1st Tanganyika Rifles" na kikosi cha Tabora kilikuwa "2nd Tanganyika Rifles".

Maafisa Waingereza wa vikosi hivyo waliajiriwa pia na serikali ya Tanganyika. Afisa mkuu alikuwa Brigedia Jenerali Patrick Sholto Douglas.

Uasi wa 1964 hariri

Katika miaka ya kwanza baada ya uhuru Waafrika wachache walipelekwa masomoni kwenye vyuo vya kijeshi huko Uingereza na kupandishwa cheo kuwa maafisa. Waziri wa mambo ya nje Oscar Kambona alituma vijana wa TANU kwenda Israel kwa masomo ya kijeshi.

Kati ya askari Waafrika wa siku nyingi uchungu ulianza kuenea kwa sababu walikuwa na tumaini uhuru utaleta nafasi za kupandishwa cheo, lakini waliendelea kusimamiwa na maafisa Wazungu. Pia waliona mishahara yao ilibaki kama awali ilhali Waafrika katika huduma ya serikali nje ya jeshi walipandishwa vyeo na mishahara.[1]

Usiku wa tarehe 19 Januari 1964 kundi la askari Waafrika walijipatia silaha wakakamata maafisa wote Wazungu na Waafrika na kusambaa mjini wakitangaza madai yao. Tarehe 20 Januari kikosi cha pili katika Tabora kiliwafuata. Maafisa Waingereza walipelekwa Kiwanja cha Ndege na kutumwa Kenya. Mawaziri wa serikali pamoja na rais Julius Nyerere walijificha, isipokuwa waziri Kambona alipatikana kujadiliana na waasi.

Baada ya Kambona kutia sahihi na kukubali madai ya waasi, Nyerere aliamua kuomba msaada wa Uingereza. Kikosi cha askari Waingereza kilifika kwa meli kutoka Aden na kumaliza uasi katika saa chache. Kikosi cha pili huko Tabora baada ya kusikia habari hizi walitangaza ya kwamba waliacha uasi wakakabidhi silaha kwa kikundi kidogo cha Waingereza.

Uasi huo wa askari Waafrika ulifuatwa na wenzao huko Uganda na Kenya. Tarehe 22 Januari askari wa Uganda Rifles katika kambi la Jinja walikatama maafisa wao na tarehe 24 Januari kikosi kimoja cha Kenya Rifles huko kambi ya Lanet (Nairobi) walijipatia silaha na kupeleka madai kwa serikali. Serikali za Jomo Kenyatta (Kenya) na Milton Obote (Uganda) zilipaswa kufuata mfano wa Nyerere na kuomba msaada wa jeshi la Uingereza kukandamiza uasi.

Mwisho wa Tanganyika Rifles hariri

Hapo serikali ya Tanzania iliamua kuachisha askari wote na kumaliza Tanganyika Rifles kabisa. Jeshi jipya likaundwa katika Septemba 1964. Maafisa Waafrika waliweza kurudi na pia askari wengi wa Tabora waliajiriwa upya.

Lakini jeshi jipya liliundwa kama taasisi chini ya usimamizi raia, yaani chini ya amri ya wanasiasa na jeshi hili linajulikana kama Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.

Marejeo hariri

  1. Linganisha madai ya askari wakati wa uasi jinsi kiongozi wao Iloga alimwambia waziri Kambona, ling T. Parsons uk 111

Viungo vya nje hariri

Kujisomea hariri

Vyanzo hasa kuhusu uasi wa 1964 hariri