Telegrafu (kutoka neno la Kiingereza telegraph lililotokana na mawili ya Kigiriki: τῆλε, tele, "mbali", na γράφειν, graphein, "kuandika") ni njia ya kupeleka habari andishi kwa mpokeaji wa mbali bila kubeba barua kwake.

Telegrafu ya kihistoria nchini Ujerumani ilitumia alama za mikono ya ubao kwa kuonyesha herufi.
Alfabeti ya Morse ilikuwa msingi wa uenezaji wa telegrafu.
Mwanamaji anatumia taa ya pekee kwa ujumbe wa nuru akitumia alama za Morse.

Telegrafu zilizotumiwa wakati wa karne ya 19 na ya 20 zilipitisha ujumbe kwa mkondo wa umeme uliopitia kwenye waya.

Telegrafu za zamani zaidi zilitumia alama za nuru au alama nyingine zilizoonekana kwa mbali.

Kwa njia hii herufi za alfabeti zilitafsiriwa kwa alama zilizoweza kupitishwa kirahisi.

Baada ya majaribio mbalimbali, mbinu ya Samuel Morse ilifaulu mwaka 1844 na kusababisha uenezaji wa teknolojia hii kote duniani. Morse alitafsiri kila herufi katika mfumo wa alama fupi au ndefu zinazoweza kuandikwa kama mfuatano wa nukta na kistari au kutumwa kama alama fupi au ndefu ya nuru, sauti au umeme na kadhalika.

Mashine ndogo ilitafsiri alama hizo katika mishtuko ya umeme iliyoweza kuchora tena alama katika mashine upande mwingine wa waya ambako sumakuumeme uliweza kusukuma kalamu juu ya karatasi. [1]

Mawasiliano kwa telegrafu yaliwezesha kwa mara ya kwanza kutuma habari kote duniani katika muda mfupi. Magazeti na makampuni makubwa ya kiuchumi yalitangulia kutumia teknolojia hii, na serikali na jeshi zilifuata. Nyaya kubwa zilipitishwa kutoka nchi hadi nchi na pia kwenye tako la bahari kwa mawasiliano baina ya mabara.

Katika karne ya 20 yalianza pia matumizi ya simu za upepo kwa habari za telegrafu.

Makampuni ya telegrafu zilipokea ujumbe ulioitwa "telegramu" kutoka wateja na kuzituma kwa mji au nchi nyingine; pale ziliandikwa tena kwenye karatasi na kupelekwa kwa mtu aliyeandikiwa. Makampuni yale yalipokea pesa kwa kila herufi iliyowasilishwa hivyo ujumbe ulikuwa mfupi.

Tangu kupatikana kwa simu matumizi ya telegrafu yalipungua lakini bado zilitumwa hadi kupatikana kwa simu za mikononi na barua pepe.

Katika nchi mbalimbali huduma hiyo ilifungwa kuanzia mwaka 2000 hivi, katika nchi nyingine huduma bado iko. [2]

Marejeo hariri

  1. "Telegraph". 150.si.edu. 2007 [last update]. Ilihifadhi kwenye nyaraka kutoka chanzo mnamo 2012-12-28. Iliwekwa mnamo November 26, 2011.  Check date values in: |date=, |accessdate= (help)
  2. Siegel, Robert (February 2, 2006). "Western Union Sends Its Last Telegram : NPR". npr.org. Iliwekwa mnamo November 26, 2011.  Check date values in: |date=, |accessdate= (help)

Viungo vya nje hariri

 
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
  Makala hii kuhusu mambo ya teknolojia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hiyo kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.