Kipimaanga (kutoka maneno pima na anga, kwa Kiingereza space probe) ni chombo cha angani kisichobeba watu na kutumwa katika anga-nje kwa kusudi la kukusanya data na kutekeleza vipimo vya sayari, miezi, Jua au violwa vya angani kwa jumla.

Kipimaanga Rosetta kikikaribia nyotamkia 67P/Churyumov–Gerasimenko kwenye mwaka 2014.

Tofauti na satelaiti, haizunguki Dunia bali inafuata njia iliyopangwa nje ya uga wa graviti ya Dunia..

Kuna aina mbalimbali za vipimaanga kama vile

  • kipimaanga kinachopita karibu na gimba la angani kwa kusudi la kupiga picha na kukusanya data zake na za mazingira yake
  • kipimaanga kunachoingia katika njiamzingo ya kuzunguka gimba la angani inapoendelea kukusanya data zake kwa muda mrefu kiasi
  • kipimaanga kinachotua kwenye uso wa gimba la angani
  • kipimaanga kinachorudi duniani baada ya kukusanya sampuli za mata ya gimba la angani, angahewa yake au chembe kutoka anga-nje

Kipimaanga cha kwanza kilikuwa Luna 1 ya Umoja wa Kisovyeti kilichopita karibu na Mwezi kwenye Januari 1959. Kilikusanya data kuhusu Ukanda wa van Allen na kuthibitisha kuwepo kwa upepo wa Jua.

Vipimaanga vya baadaye vilifika kwenye uso wa Mwezi na Mirihi, vilipita karibu na sayari zote nyingine hadi mwisho wa mfumo wa Jua.

Chombo kilichosafiri mbali kabisa ni Voyager 1 iliyorushwa angani kwenye mwaka 1977 na kwenye Januari 2018 imeshapita obiti ya Pluto na kufikia umbali wa kilomita bilioni 21 kutoka kwenye Jua.

Makala hii kuhusu mambo ya teknolojia bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hiyo kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.