Buruji za falaki (pia: alama za nyota; kwa Kiingereza: zodiac constellations) ni jina la makundinyota yanayoonekana kwenye ekliptiki zaani njia ya Jua angani (ing. ecliptic) na kuunda Zodiaki.

Buruji za falaki katika muswada ya Kiosmani, karne ya 16
Uchoraji wa Kausi (hapa kwa jina mbadala "al-Rami") katika muswada ya Al-Sufi "Kitāb Ṣuwar al-kawākib (al-thābitah)" , mnamo mwaka 1006

Katika maarifa ya unajimu (au: falaki, tofauti na fani ya sayansi inayoitwa astronomia) Waswahili wa kale, pamoja na tamaduni nyingi za zamani, waliamini ya kwamba nyota hizi zina tabia fulani na kuwa na athari juu ya maisha ya binadamu wanaozaliwa chini ya nyota fulani.

Hali halisi Jua linapita katika maeneo ya makundinyota 13 lakini tangu zamani za Babeli idadi ilifupishwa kuwa 12 kwa kusudi la kulingana na kalenda ya miezi 12. Kwa kufikia idadi hii kundinyota la Hawaa (Ophiuchus) liliondolewa katika idadi ya Zodiaki.

Jina

Kwa jumla majina mengi ya nyota yametokana na urithi wa falaki ya Waarabu. Hao walirithi habari hizi pamoja na mpangilio wa nyota kwenye mzingo wa njia ya jua angani kutoka Ugiriki ya Kale. Asili yake iko katika falaki ya Babeli.

"Buruji" yatokana na Kiarabu "برج", burj, tafsiri ya neno la Kigiriki πυργοι pirgoi, yaani mnara au boma[1].

Buruji za falaki kwenye njia ya jua angani

Buruji za falaki katika utamaduni wa Waswahili ni kama zifuatazo:[2]

Katika unajimu wa siku hizi majina mengi ya kimapokeo katika unajimu wa Afrika ya Mashariki yamesahauliwa na badala yake wapiga falaki wanatumia orodha ya majina ambayo mara nyingi ni tafsiri ya majina ya Kiingereza tu, au pia namna ya kutaja alama ya makundinyota kwa neno la Kiswahili. Isipokuwa Mizani na Mashuke bado ni majina asilia. Majina katika unajimu wa kisasa jinsi yalivyo kawaida ni yafuatayo:

  1. Kondoo (Aries): Machi 21 – Aprili 19
  2. Ng’ombe (Taurus): Aprili 20 – Mei 21
  3. Mapacha (Gemini ): Mei 22 – Juni 20
  4. Kaa(Cancer): Juni 21 – Julai 22
  5. Simba (Leo): Julai 23 – Agosti 22
  6. Mashuke (Virgo):Agosti 23 – Sept 22
  7. Mizani (Libra): Sept 23 – Okt 22
  8. Ng’e (Scorpio): Okt 24- Nov 21
  9. Mshale (Sagittarius): Nov 22- Des 21
  10. Mbuzi (Capricorn):Des 22 – Jan 19
  11. Ndoo (Aquarius):Jan 20 – Feb 18
  12. Samaki (Pisces):Feb 19 – Machi 20

Marejeo

  1. Hakuna uhakika juu ya maana asili ya jina hili; Hartner-Kunitsch katika makala MINTAKAT AL-BURUDJ wanarejelea elezo kuwa asili iko katika mitholojia ya Babeli kwa maana "makazi ya miungu"; tazama kamusi elezo ya Uislamu "The Encyclopaedia Of Islam, New Edition", Volume VII Mif — Naz
  2. J Knappert, fungu "In East Africa", makala AL-NUDJUM katika THE ENCYCLOPAEDIA OF ISLAM, LEIDEN BRILL 1997, VOLUME VIII NED — SAM, uk 105

Tazama pia