Biashara ya utumwa kupitia Atlantiki

Biashara ya utumwa kupitia Atlantiki (vilevile: Biashara ya utumwa ya pembetatu au Biashara ya utumwa ya ng'ambo ya Atlantiki) ni jina la kutaja aina ya biashara ambayo ilikuwa ikifanyika baina ya mabara matatu, yaani, Afrika (upande wa magharibi), Amerika na Ulaya (hasa katika pande za magharibi mwa Ulaya).

Mfano wa mchoro wa Biashara ya Pembetatu

Biashara ilihusisha hasa wafanyabiashara kutoka Ulaya ambao walikuja na bidhaa za viwandani na kuvibadilisha na watumwa na vitu vya thamani kubwa barani Afrika kama vile dhahabu, almasi, fedha na kadhalika ambapo wao walichukua watumwa na bidhaa nyingine na kwenda nazo Amerika.

Wakiwa huko, watumwa walizalisha malighafi za kilimo na madini ambapo Wazungu walizichukua na kuzipeleka Ulaya kwa ajili ya kutengenezea bidhaa nyingine.

Watumwa waliochukuliwa Afrika walisafirishwa kwa njia ya meli kupitia Bahari ya Atlantiki hadi huko Amerika ambapo walitiwa utumwani katika sekta mbalimbali za kiuchumi. Mahusiano ya biashara ya namna hiyo yameunda "Umbo la Pembetatu" ambalo likaja kujulikana kama "Biashara ya Pembetatu".

Historia hariri

Kipindi hariri

Biashara hii inaaminika ilianza mwishoni mwa karne ya 15 na kukua hadi mwishoni mwa karne ya 18 ambapo ilikomeshwa mazima.

Washiriki hariri

Washiriki wakuu wa biashara hii walikuwa wanatoka Ulaya ambao hao ndio waliokuwa wanashikilia biashara hii. Wengine walikuwa wenyeji wa Kiafrika (Watemi) ambao walikuwa wanatoa watumwa kwa wafanyabishara Wazungu kwa kubadilishana nao bidhaa za viwandani. Kituo kikuu cha kuanzia shughuli hizi za Biashara ya Utumwa ya Pembetatu ilikuwa Ulaya na biashara pia ilimalizikia hukohuko Ulaya (kifupi: Biashara inaanza barani Ulaya na kumalizikia barani Ulaya).

Biashara zilizohusishwa hariri

Kutoka Ulaya hariri

Kutoka Ulaya, wafanyabishara walileta Afrika bidhaa za viwandani kama vile nguo, vinywaji, sigara, bunduki na unga wake, mapambo, vyombo vya kupikia na vinginevyo ambavyo vilibadilishana kwa watumwa na mali njema nyinginezo za Kiafrika.

Kutoka Afrika hariri

Kutoka Afrika, wafanyabiashara wa Kizungu walibadilishana biashara zao na kuchukua watumwa na bidhaa nyingine za thamani kama vile dhahabu, pembe za ndovu, fedha, na ngozi za wanyama. Watumwa walichukuliwa hadi Amerika na India-za-Magharibi (Visiwa vya Karibi) ili kufanya kazi katika mashamba makubwa na migodi iliyoanzishwa na Wazungu.

Kutoka Amerika hariri

Kutoka Amerika, Wazungu walichukua malighafi za kilimo kwa mfano pamba, mkonge, majani ya chai na tumbaku na madini kisha kwenda nayo Ulaya kwa ajili ya kuzalisha viwandani.

Sababu zilizopelekea kuibuka kwa Biashara ya Utumwa ya Pembetatu hariri

Kuna sababu mbalimbali zilizochangia kuibuka na kukua kwa Biashara ya Utumwa ya Pembetatu - nazo ni kama ifuatavyo:

Kuibuka kwa daraja la wafanyabiashara huko Ulaya hariri

Kuibuka kwa wafanyabiashara barani Ulaya kwenye karne ya 15 kulipelekea hitaji la mtaji mkubwa kwa ajili ya ukuzaji wa viwanda. Hili nalo lilipelekea kukua kwa biashara hii.

Kugunduliwa kwa Amerika (Dunia Mpya) hariri

Kugunduliwa kwa Amerika na Christopher Columbus mnamo 1492 kuliandaa kukua kwa Biashara ya Utumwa ya Pembetatu.

Kuanzishwa kwa mashamba makubwa na migodi barani Amerika hariri

Baada ya kugunduliwa Amerika, Wazungu walianzisha mashamba makubwa ya mazao aina mbalimbali kama vile pamba na tumbaku huko Magharibi mwa Indi. Hili lilihitaji wafanyakazi, hivyo basi lilipelekea kukua kwa biashara.

Kushindwa kufanya kazi kwa Wahindi Wekundu katika mashamba makubwa hariri

Awali, Wazungu waliwatumia wenyeji wa Amerika (Wahindi Wekundu) katika mashamba yao kama wafanyakazi. Lakini watu hao walikufa haraka. Tatizo kuu lilikuwa hali ya pekee ya Amerika ambako watu waliwahi kuendelea kuishi bila mawasiliano na sehemu nyingine za dunia kwa milenia nyingi. Walikosa kinga dhidi ya magonjwa mengi yaliyokuwa kawaida katika mabara yaliyokaa karibu kama Asia, Afrika na Ulaya, hivyo walikufa haraka baada ya kukutana na Wazungu na magonjwa yao. Hilo liliwafanya Wazungu waende Afrika kutafuta wafanyajikazi. Hivyo biashara ikakua kwa sababu watumwa kutoka Afrika walikuwa na afya na nguvu kuzidi Wahindi Wekundu.

Ukuaji wa teknolojia ya meli hariri

Kukua kwa teknolojia ya meli (utengenezaji wa meli na mwongozo wa kidira) ulirahisisha usafirishaji baina ya Afrika, Amerika, na Ulaya. Kwa mfumo huu, ukuaji wa biashara ukawa hauepukiki tena.

Mahali/nafasi ya kijiografia ya mabara matatu hariri

Amerika, Afrika na Ulaya zimekaribiana mno. Hili nalo lilirahisisha ukuaji wa biashara.

Upatikanaji wa watumwa katika Afrika Magharibi hariri

Watumwa na vitu vingine vya thamani kama vile pembe za ndovu, dhahabu na almasi vilipatikana kwa wingi Afrika Magharibi. Hili lilipelekea ukuaji wa biashara kuwa hauepukiki.

Nafasi ya viongozi wenyeji wa Afrika Magharibi hariri

Huko Afrika Magharibi, baadhi ya viongozi walishirikiana na Wazungu kinaganaga katika kuratibu Biashara ya Pembetatu hasa kwa kukusanya watumwa na kuwasaidia wafanyabiashara wa Kizungu kupanga mikakati ya kibiashara na utelekezaji wake huko Afrika Magharibi. Kati ya hao viongozi alikuwemo Mfalme Agaja, Alfin Abipa, Alfin Ojago, na Alafin Ojig. Hili nalo lilichangia ukuaji wa biashara ya Pembetatu.

Matokeo/athari za Biashara ya Pembetatu katika Afrika hariri

Baadhi ya matokeo ya biashara ya Pembetatu hasa huko Afrika Magharibi yalikuwa kama hivi:

Kupungua kwa idadi ya watu - walikwenda utumwani hariri

Waafrika wengi walichukuliwa kama watumwa na kupelekwa Amerika ili wakafanyaje kazi katika mashamba na migodi ya Wazungu. Hili lilipunguza idadi ya Waafrika hasa Afrika Magharibi.

Kutokea kwa ukame na njaa kwa sababu ya uzalishaji hafifu hariri

Biashara ilipelekea kuleta ukame na njaa kwa sababu uzalishaji ulisimama hasa kwa kupoteza nguvukazi ya Afrika. Waliokuwa wanachukuliwa utumwa ni wale wenye miili yenye uwezo tu na si watoto wala watu wazima.

Familia kutengana hariri

Biashara ya Pembetatu ilichochea mno utenganisho wa familia hasa kwa kufuatia kuchukua Waafrika kama watumwa na kuwapeleka Amerika na Indi-za-Magharibi.

Kuanguka kwa Biashara ya Ng'ambo ya Sahara hariri

Biashara ilichangia mazima kuanguka kwa Biashara ya Ng'ambo ya Sahara. Mwishoni mwa karne ya 15, Biashara ya Ng'ambo ya Sahara ilishindwa kabisa kuendelea hasa kwa kuibuka kwa Biashara ya Pembetatu.

Utumwa uliochochewa na biashara utumwa hariri

Biashara pia ilichochea (kufanya watu wapende biashara ya kuuza wenzao) vilivyo huko Afrika hasa katika upande wa Afrika Magharibi. Viongozi wengi wa Kiafrika walijihusisha vilivyo katika kununua na kuuza watumwa katika kanda hiyo.

Kuanguka kwa baadhi ya falme/madola hariri

Biashara ya Pembetatu ilipelekea kuanguka kwa baadhi ya falme/dola huko Afrika Magharibi hasa zile ambazo zilitegemea kuuza bidhaa na si watumwa kwa Wazungu. Baadhi ya hizo dola ni pamoja na [[Dola la Ghana], Dola la Mali na Dola la Songhai na mengine mengi.

Kuibuka kwa baadhi ya madola hariri

Biashara ilipelekea kukua kwa baadhi ya madola hasa yale yaliyokuwa yanategemea kuuza na kununua watumwa kama vile Tokolar, Ife, Dahomey na kadhalika.

Maendeleo duni hariri

Kiujumla biashara ilichochea kufifisha maendeleo ya Afrika katika nyanya zote ikiwa kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Kupatikana kwa jamii kubwa za Wanegro hasa Brazil na Marekani hariri

Watumwa waliopelekwa Amerika na sehemu nyingine walizaliana wenyewe kwa wenyewe au wanawake wao walipata mimba kwa Wazungu au wengineo. Ndiyo asili ya makundi makubwa ya watu wenye asili ya Afrika katika nchi kama Brazil, Marekani n.k. Hasa katika visiwa vingi vya Karibi, wakazi wengi leo wana asili hiyo.

Tazama pia hariri

Viungo vya Nje hariri

 
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
  Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Biashara ya utumwa kupitia Atlantiki kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.