Gaspare Bertoni (9 Oktoba 177712 Juni 1853)[1] alikuwa padri Mkatoliki wa Verona (Italia) aliyeanzisha shirika la Wastigmatini ambalo limeenea hata Tanzania. Lengo lake lilikuwa kuandaa wamisionari walio tayari kutumikia maaskofu.

Mt. Gaspare katika vazi rasmi la kipadri.

Papa Paulo VI alimtangaza mwenye heri tarehe 1 Novemba 1975, halafu Papa Yohane Paulo II alimtangaza mtakatifu tarehe 1 Novemba 1989.

Sikukuu yake huadhimishwa tarehe aliyoaga dunia[2].

Maisha hariri

Gaspare Luigi Bertoni alilelewa na wazazi wake, Francesco Bertoni (mwanasheria) na Brunora Ravelli. Baadaye alilelewa na Wajesuiti na chama cha Bikira Maria huko kwao Verona.

Alipopokea kwa mara ya kwanza sakramenti ya ekaristi, alipata njozi yenye ujumbe wa kumtaka awe padri. Hivyo alianza masomo yake mwaka 1796.

Tarehe 1 Juni 1796 - wakati wa Mapinduzi ya Kifaransa - jeshi la Ufaransa liliteka mji huo kwa miaka karibu 20. Hapo Bertoni alijiunga na Jamaa ya Kiinjili ya Hospitali akafanya kazi kwa waliojeruhiwa au kuathiriwa na uvamizi huo.

Alipewa upadrisho tarehe 20 Septemba 1800, akafanya uchungaji kwa masista na waseminari.

Katika kazi hiyo Bertoni alihimiza sana watu waheshimu madonda matano ya Yesu msulubiwa. Pia alihamasisha sala kwa ajili ya Papa Pius VII aliyefungwa na Napoleon Bonaparte. Tena alianzisha vikundi vya Kimaria na shule kwa ajili ya mafukara.

Tarehe 4 Novemba 1816 alianzisha shirika la Wastigmatini ambalo mwaka 2012 lilikuwa na nyumba 94 na wanachama 422 wakiwemo mapadri 331, baadhi wakiwa wazaliwa wa Tanzania au wanaofanya kazi katika nchi hiyo na nyinginezo za Afrika.

Pamoja na kwamba afya ya Bertoni ilivurugwa na homa na usaha wa kudumu mguuni miaka 20 ya mwisho ya maisha yake, hata akafanyiwa upasuaji mara 300 na zaidi, aliendelea kuongoza watu kiroho kutoka kitandani hadi alipofariki mwaka 1853.

Tazama pia hariri

Tanbihi hariri

  1. Gaspar Bertoni (1777-1853) - biography
  2. Martyrologium Romanum

Marejeo hariri

  • C. FABRO, C.S.S., Mtakatifu Gaspari Bertoni, Mtumishi Mkamilifu wa Kanisa – tafsiri ya R. R. Kilumanga – ed. Stigmatine Fathers – Kisanga 1989

Viungo vya nje hariri

  Makala hii bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mkristo huyu, kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Je, unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuiongezea habari.