Njia ya reli

(Elekezwa kutoka Njia za reli)

Njia ya reli ni barabara maalumu iliyojengwa kwa ajili ya matumizi ya treni.

Ujenzi wa reli ya Uganda wakati wa ukoloni - misingi kuinuliwa penye hatari ya mafuriko

Kwa kawaida njia hii hutengenezwa kwa kufunga pau mbili za feleji sambamba kwenye mataruma ya mbao, simiti au chuma zinazokaa juu ya msingi wa mawe ya kokoto.

Umbali kati ya reli mbili umesanifishwa katika kila nchi au angalau eneo la kampuni ya reli. Umbali huo unapaswa kulingana kikamilifu na upana wa magurudumu ya treni maana tofauti na magari barabarani treni hazilengwi na dereva bali na reli za njia zenyewe.

Muundo wa ujenzi wa njia ya reli
Ujenzi wa njia ya reli nchini Finlandi mnamo mwaka 1950
Mashine ya kujenga njia ya reli inaweka mataruma njiani katika nchi ya Ujerumani.

Muundo wa ujenzi hariri

Kazi ya kwanza ni kujenga msingi wa njia ya reli. Pale ambako ardhi si imara tabaka la ardhi linaongezwa kwenye msingi. Juu yake matabaka mengine ya mchanga au kokoto yanaweza kuongezwa, kutegemeana na mazingira.

Juu ya msingi huu panawekwa tabaka la mawe ya kokoto ambayo ni tako kwa mataruma yanayobeba reli za garimoshi. Mataruma haya yanashika reli kwa umbali unaotakiwa. Mataruma yalitengenezwa zamani kwa kawaida kwa ubao mgumu, siku hizi pia mara nyingi kwa simiti, wakati mwingine pia kwa chuma.

Reli hushikwa kwa mabano yanayofungwa kwa parafujo ndefu kwenye mataruma.

Uwezo wa njia ya reli kubeba treni nzito na pia treni za haraka unategemea uwezo wa msingi pamoja na uzito wa reli za garimoshi zenyewe.

Zamani ujenzi ulifanywa kwa mikono pekee. lakini siku hizi kuna mashine maalumu (tazama filamu inayoonyesha jinsi mashine inavyolaza mataruma ya simiti mfululizo nchini Ujerumani).

Kabla ya ujenzi wa njia kuna kazi ya kukagua eneo na kuchagua njia bora inayowezekana. Wakaguzi wanaangalia aina za udongo, mitelemko, hatari za mafuriko njiani na mengine mengi.

Reli za kutambuzwa hariri

Zamani vyuma vya reli za garimoshi vilifungwa kwa kuacha mapengo madogo kati yake. Hii ilikuwa muhimu kwa sababu chuma na feleji inapanuka wakati wa joto na kujikaza yaani kuwa fupi kiasi wakati wa baridi kali. Siku hizi vyuma hivyo vinashikwa pamoja kwa njia ya kufuma yaani tambuzo (kuyeyusha uso wa vyuma kwa joto kubwa na kuviunganisha hivyo). Mtutuko unaoweza kutokea ndani ya vyuma hubanwa kwa njia ya ujenzi imara zaidi. Kama ni lazima wajenzi wanaongeza sehemu za pekee za upanuzi.

Swichi hariri

Pale ambapo njia za reli zinaungana au kuachana kuna swichi zinazowezesha treni kubadilisha njia. Swichi hizi kwenye njia zinazotumiwa na treni chache zinaweza kubadilishwa kwa mkono, na kwa kazi hii ni lazima kuwa na kituo au ofisi kwa wafanyakazi. Kwenye reli zilizoendelea swichi hizi hutawaliwa kwa mbali ama kupitia nyaya ndefu au siku hizi pia kwa njia ya elektroniki ilhali kila swichi ina injini ndogo ya umeme.

Penye usafiri mwingi njia za reli hujengwa kwa jozi, yaani njia mbili kandokando ili treni mbili ziweze kupishana bila matatizo. Pale ambapo kuna njia 1 tu ni lazima kupanga sehemu ambapo treni 1 inaweza kusubiri hadi treni nyingine imepita.

Upana wa njia au geji hariri

Geji ni jina la upana kati ya reli mbili (kwa Kiingereza gauge) ambao unatofautiana kati ya nchi na nchi. Kwa kawaida nchi jirani huwa na geji ya pamoja ili kurahisisha mwendo wa treni na mabehewa.

Geji sanifu ya kimataifa (ing. Standard Gage Railroad SGR) leo hii ni mita 1.435 (futi 4 inchi 8 1⁄2). Katika Afrika ya Mashariki reli za kwanza zilijengwa na Wajerumani wakati wa ukoloni, pia Waingereza walijenga reli yenye upana wa mita 1 pekee kama vile Reli ya Tanganyika. Wakati ule hii ilitazamwa kutosha kwa mahitaji ya usafiri, tena ilipunguza gharama. Lakini siku hizi geji hii ndogo hairuhusu kutumia njia kwa treni nzito wala treni za haraka.

Wakati wa ujenzi wa reli ya TAZARA nchini Tanzania geji ya mita 1.067 ilichaguliwa kwa sababu reli hii inaungana na reli ya Zambia huko New Kapiri Mposhi na reli zote za Kusini mwa Afrika hutumia geji hii. Hivyo ndani ya Tanzania kuna matatizo ya kwamba mabehewa ya TAZARA na Tanzania Railway Corporation hayalingani, yaani hayawezi kuingia kwenye njia za kampuni nyingine. Njia zote mbili za TAZARA na TRC zinakutana Dar es Salaam na pale Kidatu kuna kituuo cha kubadilishana kontena kati ya makampuni mawili.

Urusi na nchi zilizokuwa sehemu ya Umoja wa Kisovyeti huwa na upana wa mita 1.520 ambayo ni pana zaidi kuliko nchi nyingi za jirani. Kwa sababu ya wingi wa usafiri wa reli ndani ya Urusi na nchi za Ulaya na China kuna vituo mbalimbali ambako sehemu ya chini za mabehewa zinabadilishwa kwa ajili ya upana husika wakati wa kuvuka mipaka.

Kujenga njia mpya kwa kutumia geji sanifu ya kimataifa (SGR) katika Afrika ya Mashariki hariri

Nchi za Afrika za Mashariki zilirithi njia za geji nyembamba ya mita moja. Ujenzi wa TAZARA ulileta geji ya Afrika Kusini hadi Dar es Salaam. Nchi jirani ya Ethiopia ilirithi pia geji ya mita 1, na Eritrea geji ya sentimita 95.

Tangu mwaka 2007 shughuli za kubuni mpango mkuu wa reli ya Afrika ya Mashariki ziliendelea[1] na kufikia makubaliano. Tangu mwaka 2014 ujenzi wa reli yenye geji sanifu kutoka Mombasa kwenda Nairobi ulianza na mnamo Juni 2017 treni za kwanza zinatakiwa kuanzisha huduma[2]. Njia imepangwa kuendelea hadi Kampala na Kigali.

Vivyo hivyo nchini Tanzania ujenzi wa awamu ya kwanza ya reli ya geji sanifu ilianzishwa Aprili 2017 itakayounganisha Dar es Salaam na Morogoro[3] na kuendelea baadaye hadi Kigoma na Mwanza, na baadaye hadi Burundi na Rwanda itakapokutana na njia kutoka Mombasa.

Marejeo hariri

  1. http://ecdpm.org/great-insights/regional-integration-dynamics-africa/railway-rivalry-east-african-community/ Archived 30 Januari 2017 at the Wayback Machine. Railway rivalry in the East African Community], tovuti ya European Centre for Development Policy Management (ECDPM) ya Julai 2016, iliangaliwa Aprili 2017
  2. This is the year Nairobi finally welcomes standard gauge rail, tovuti ya Daily Nation, Nairobi ya 2 Januari 2017, iliangaliwa Aprili 2017
  3. Ujenzi SGR wafikia asilimia 36, gazeti la Mtanzania, tar. 27-11-2018