Mtakatifu

(Elekezwa kutoka Watakatifu)

Mtakatifu ni binadamu aliye hai au aliyekufa ambaye dini fulani au watu mbalimbali wanamheshimu kwa namna ya pekee kwa jinsi alivyoonekana kuwa karibu zaidi na Mungu hata akashirikishwa utakatifu wake. Kwa hiyo hutazamwa kama kielelezo cha uadilifu na pengine kama mwombezi pia.

Katika utamaduni wa Kikristo, watakatifu huchorwa na nembo takatifu, kama ishara ya utakatifu wao; tazama jinsi Yuda Iskarioti (wa mbele kabisa) ni mtume pekee ambaye hana nembo hiyo.

Katika Uyahudi hariri

Jina linalotumiwa zaidi na Wayahudi ni tzadik (mtu wa haki, mwadilifu), aliyejitahidi kufuata Torati.

Kitabu cha Talmud kinasema kila mara duniani walau watu 36 wa namna hiyo (tzadikim) wanaishi kati yetu na kuzuia ulimwengu usiangamizwe kama adhabu ya dhambi.

Pengine wanaitwa hivyo hata watu wa mataifa, hasa waliojitahidi kusaidia Wayahudi, k.mf. wakati wa dhuluma. Baadhi yao wanaorodheshwa na kupewa heshima rasmi.

Katika Ukristo hariri

Mwanzoni mwa Kanisa kila Mkristo aliitwa mtakatifu kwa sababu alitengwa na ulimwengu na kuwekwa wakfu kwa Mungu aliye mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu.

Sifa hiyohiyo ilitolewa pia kwa mahali, siku, vitu n.k. kutokana na matumizi yake ya kidini.

Katika Kanisa Katoliki hariri

 
Klara wa Asizi alivyochorwa na Simone Martini katika basilika la Mt. Fransisko wa Asizi huko Asizi, Italia.

Kwa Wakatoliki mtakatifu ni yule aliyemfuata Yesu Kristo, akiishi kwa upendo na maadili mengine yanayoutegemea, hasa aliyeyatekeleza kwa kiwango cha ushujaa katika kufia dini, kutoa uhai wake katika kuhudumia wengine au katika maisha ya kila siku.

Utakatifu si wa aina moja, bali kila binadamu anatakiwa kuitikia siku kwa siku wito maalumu aliopewa na Mungu. Hivyo yeyote anaweza na kupaswa kulenga utakatifu, bila kujali sifa zake za kimaumbile tu.

Ili kuzuia udanganyifu, tangu mwanzoni mwa milenia ya pili Kanisa Katoliki linamuachia Papa kusimamia kesi ndefu za kumtangaza mtakatifu mpya, miaka baada ya kifo chake.

Wakatoliki wanawapatia Bikira Maria na watakatifu wengine heshima ya pekee kama marafiki wa Mungu, lakini si ibada halisi ambayo ni kwa Mungu tu. Heshima hiyo inadai waumini wajitahidi pia kufuata mifano yao kama wao walivyofuata ile ya Yesu.

Katika Makanisa ya Kiorthodoksi hariri

 
Masalia ya Demetrio wa Thesalonike katika kanisa lake huko Thesalonike, Ugiriki.

Makanisa ya Kiorthodoksi yanamuita mtakatifu hasa anayesadikiwa yuko katika paradiso, kuanzia Abeli, Adamu na Eva, Musa na manabii wengine, lakini pia malaika.

Ni Mungu anayefunua watakatifu wake kwa kuitikia sala anazotolewa kwa kuwapitia hao hata akatenda miujiza. Wakristo wanaanza kuwatambua lakini uamuzi wa mwisho unachukuliwa na sinodi ya maaskofu.

Waorthodoksi na Waorthodoksi wa Mashariki wanawatendea watakatifu kama watu hai, kwa sababu wanaishi mbinguni pamoja na Kristo mfufuka, ingawa miili yao haijaungana tena na roho zao.

Kila mtu anapobatizwa anapewa jina la mtakatifu fulani kama msimamizi kwa maisha yake yote.

Katika Uprotestanti hariri

Madhehebu mengi ya Uprotestanti hayakubali mawazo hayo, yakipenda kusisitiza kwamba wokovu unamtegemea Mungu tu. Hata hivyo mara nyingi waamini bora wanakumbukwa kwa heshima na kuchukuliwa kama mfano (taz. Confessio augustana art. 21).

Hasa Waanglikana wanakaribia msimamo wa Wakatoliki na kuadhimisha sikukuu za watakatifu kadiri ya kalenda maalumu.

Katika Uislamu hariri

Ingawa dini hiyo haikubali tofauti kati ya watu, Waislamu wengi wanapenda kuheshimu kwa namna ya pekee marafiki wa Mungu (wali), wakisadiki wana uwezo wa kutabiri, kuombea na kuponya.

Tazama pia hariri

Viungo vya nje hariri

  Makala hii kuhusu mambo ya dini bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hii kama historia yake au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.