Kleopatra

Malkia wa Ufalme wa Ptolemaic wa Misri kutoka 51 hadi 30 BC

Kleopatra (69 KK - 30 KK) alikuwa malkia na farao wa mwisho wa Misri. Alizaliwa katika nasaba ya Waptolemaio. Alipata elimu nzuri hadi kusema lugha nyingi kama vile Kikopti, Kiarabu, Kiaramu, Kihabeshi, Kifarsi na Kigiriki kama lugha ya mama.

Sarafu ya Kimisri yenye picha ya Kleopatra
Taswira ya 1660: Kifo cha Kleopatra

Malkia na fitina hariri

Alipokuwa na miaka 18 baba yake Ptolemaio XII aliaga dunia naye akarithi ufalme pamoja na kaka yake aliyekuwa mdogo wa miaka 12. Mwaka 49 KK washauri wa kaka walimfukuza Kleopatra katika ufalme. Alikaa jangwani kati ya makabila yaliyokuwa waaminifu naye hadi kuingia kwa Waroma nchini.

Kleopatra na Caesar hariri

Mwaka 48 KK vita ya wenyewe kwa wenyewe ya Kiroma ilifika Misri. Pompeius, adui wa Julius Caesar, alikimbilia Misri alipokamatwa na kuuawa na washauri wa mfalme. Julius Caesar mwenyewe alimfuata akajaribu kumaliza fitina ndani ya familia ya Kimisri. Alimpenda Kleopatra akamsaidia kushika ufalme tena. Akazaa naye mtoto aliyeitwa Caesarion (47 KK - 30 KK).

Caesar alirudi Roma na Kleopatra pamoja na mtoto alimfuata mwaka 44 KK na alikuwako Roma wakati wa uuaji wa Caesar akarudi tena Misri.

Mke wa Marcus Antonius hariri

Katika vita kati ya Marcus Antonius na Octavianus (Augusto wa baadaye) hakushikamana na upande wowote hadi kukutana na Marcus Antonius. Akawa mpenzi wake na Marcus alimfuata Misri walipozaa watoto wawili. Marcus alimwacha nyuma alipoondoka Misri akarudi Roma mwaka 40 KK akapatana na Octavianus na kufunga ndoa na dada yake Octavia.

Mwaka 37 KK alipokuwa mtawala wa nusu ya mashariki ya dola la Roma alirudi kwa Kleopatra akamwoa mwaka 37 KK hata kama kisheria Mroma hakuruhusiwa kuwa na wake wengi. Katika agano lake Marcus aliwapa watoto wa Kleopatra majimbo katika mashariki.

Mwaka 33 KK Marcus Antonius alifarakana na Octavianus. Huyo alitumia nafasi ya kushawishi senati ya Roma kutangaza vita dhidi ya Misri kwa sababu ya majimbo yaliyokabidhiwa mikononi mwa watoto wa Kleopatra.

Mwisho na kifo hariri

Katika mapigano ya Aktium meli za Octavianus zilishinda; Marcus Antonius alijiua. Baada ya kufika kwa Octavianus nchini Misri malkia alijaribu kupatana naye ikashindikana. Alielewa ya kwamba atapelekwa Roma na kuonyeshwa kama mfungwa mbele ya watu wa mji huo. Hapo aliamua kuaga dunia tarehe 12 Agosti 30 KK. Octavianus alimtafuta pia Caesarion kwa sababu aliogopa mtoto wa Caesar angekuwa hatari kwake akamwua.