Mlima Karmeli (kwa Kiebrania הר הכרמל, Karem El/Har Ha'Karmel, "Shamba la mizabibu la Mungu"; kwa Kiarabu |الكرمل/جبل مار إلياس, Kurmul/Jabal Mar Elyas, "Mlima wa Mt. Eliya" unapatikana katika pwani ya Israeli kaskazini ukijitokeza katika Bahari ya Kati.

Mlima Karmeli jioni.

Ni mlima muhimu kwa biolojia, akiolojia na dini mbalimbali na unahesabiwa na UNESCO "urithi wa dunia" upande wa viumbehai.

Kadiri ya masalia yaliyopatikana huko, kwa kipindi fulani watu wa aina Homo neanderthalensis na Homo sapiens waliishi pamoja katika eneo hilo.

Katika Biblia hariri

 
Nabii Eliya alivyochorwa na José de Ribera.

Biblia (1Fal 18) inausifu kwa uzuri wake, na kusimulia jinsi juu yake nabii Eliya alivyoshindana na manabii wa uongo wa Baali ili kurudisha Waisraeli kwa Mungu wao pekee, YHWH.

Ni kwamba Waisraeli walielekea dini za jadi zilizoenea kandokando yao kwa sababu zilikuwa zinaahidi kufanikisha maombi yao kwa ibada za hakika, wakati Mungu ana hiari ya kupokea au kukataa sadaka zao. Waisraeli walijaribu kufuata pande zote mbili kwa pamoja, ila Mungu hakuweza kukubali, kwa kuwa ni peke yake tu.

Imani yao iliyumba hasa wakati mfalme Ahabu alipotawala Kaskazini (869-850 hivi K.K.), ambapo Yezebeli, mke wake, alifanya juhudi kubwa za kuikomesha kabisa imani yao kwa YHWH ili wamuabudu Baali, mungu mkuu wa kwao aliyehusika na mvua, kufuatana na sanamu mbili zilizotengenezwa na Yeroboamu I zikiwa na sura ileile ya Baali (fahali wa dhahabu). Mezani pa malkia huyo walikuwa wanalishwa manabii wa uongo 850 kumbe manabii wa Bwana waliuawa karibu wote.

Hapo Mungu akamtuma Eliya (1Fal 17-18) ambaye jina lake lina maana ya kwamba, “Mungu wangu ni YHWH” na linajumlisha kazi yake ya kutetea kwa ari zote imani ya kweli hata akaiokoa. Ili kuondoa utata wa kuabudu pande mbili, Eliya kwanza alizuia mvua isinyeshe nchini miaka mitatu na nusu, ibada kwa Baali zisifanikiwe hata kidogo, halafu akashindana na manabii hao hadhara ya Israeli yote juu ya mlima Karmeli.

Tofauti na mbinu za manabii 450 wa Baali, waliofikia kujichanja na kutoka damu ili kuvuta moto kutoka mbinguni wasifaulu, Eliya aliomba tu kwa unyofu kwamba Mungu ajitokeze ili kugeuza mioyo ya watu wake wamrudie. Kwa kuteremsha moto toka mbinguni juu ya sadaka yake YHWH alithibitisha kuwa ndiye Mungu pekee na kuwa anaendelea kuwaokoa watu wake. Baada ya Eliya kuwachinja wote aliruhusu mvua inyeshe tena. Ndiyo sababu anasifika kwa nguvu ya sala yake (Yak 5:17-18).

Katika historia ya Ukristo hariri

Uzuri wa mlima na mandhari yake, pamoja na umuhimu wake wa Kibiblia ulivuta tangu zamani Wakristo wakaapweke kuishi juu yake. Kutokana nao lilienea baadaye shirika la Wakarmeli katika matawi yake mbalimbali.

Tazama pia hariri

Tanbihi hariri

Viungo vya nje hariri

 
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
  Makala hii kuhusu eneo fulani bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu eneo hilo kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Je, unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuiongezea habari.


Usitaje majina ya madiwani na viongozi au maafisa wengine wa sasa maana wanabadilika haraka mno.