Kolombia (kwa Kihispania: República de Colombia) ni nchi kwenye pembe la kaskazini la Amerika ya Kusini.

Kolombia


Ramani ya Kolombia

Imepakana na Venezuela, Brazil, Ekuador, Peru na Panama. Ina pwani mbili, kwenye Pasifiki na Atlantiki.

Jina la nchi limeteuliwa kwa heshima ya Kristoforo Kolumbus (Kihisp.: Cristóbal Colón; kwa Kiitalia: Cristoforo Colombo) aliyegundua njia kati ya Hispania na Amerika mwaka 1492.

Jiografia hariri

Upande wa magharibi wa nchi una milima ya Andes inayopatikana kwa safu tatu za milima zinazoitwa "Kordileri".

Kati ya milima hiyo kuna chanzo cha mito miwili mikubwa ya nchi: ndiyo Rio Cauca na Rio Magdalena inayoishia katika Bahari ya Karibi (Atlantiki). Mto mkubwa upande wa magharibi ni Atrato unaoishia Pasifiki.

Milima ya juu ni Pico Cristobal Colon na Pico Simon Bolivar yenye kimo cha mita 5,775 juu ya UB kila mmoja.

Sehemu ya mashariki ya Kolombia ni tambarare yenye misitu minene. Mito yake, kama vile Putumayo, Yapura, Meta na Guaviare inaishia ama katika mto Orinoko au kwenye Amazonas.

Visiwa hariri

Kolombia ina visiwa katika bahari zote mbili.

Upande wa Karibi / Atlantiki kuna funguvisiwa vya San Andres na Providencia vilivyoko baharini km 770 kutoka bara. Karibu na pwani ya Karibi ni kisiwa cha Fuerte na funguvisiwa vya San Bernardo na del Rosario.

Visiwa vya Malpelo, Gorgona na Gorgonilla viko katika Pasifiki.

Miji hariri

Miji mikubwa ni mji mkuu Santa Fé de Bogotá, Medellín, Cali, Cartagena de Indias, Barranquilla, Ibagué, Manizales, Pasto, Cúcuta na Bucaramanga.

Historia hariri

Mataifa asilia ya Waindio walikuwa Wachibcha, Waarawak na Wakaribi.

Hasa Wachibcha waliokalia nyanda za juu walikuwa na utamaduni wa kimaandishi; walitumia kalenda, hesabu na alfabeti yao. Lakini hawakujenga miji na madola yao yalikuwa madogo.

Wahispania walijenga miji ya kwanza: Santa Marta (1527) na Cartagena de Indias (1533) kwenye pwani. Tangu mwaka 1537 waliingia katika nyanda za juu na kuvamia maeneo ya Wachibcha. Hapo walijenga miji ya Santa Fé de Bogotá na Tunja (yote miwili 1539).

Baadaye Kolombia ilikuwa kitovu cha ufalme mdogo wa Granada Mpya.

Tangu mwaka 1813 kiongozi Simon Bolivar alipigania uhuru wa makoloni ya Amerika ya Kusini. Mwaka 1819 Jamhuri ya "Gran Colombia" (Kolombia kubwa) iliundwa ikadumu hadi 1831. Baadaye iliachana kuwa nchi za pekee za Kolombia (pamoja na Panama), Venezuela na Ecuador.

Kolumbia iliona vita za wenyewe kwa wenyewe; wakati wa "vita ya siku 1000" Marekani ilitumia udhaifu wa nchi na kusaidia ghasia katika Panama iliyosababisha uasi wa Panama kuwa nchi ya pekee mwaka 1903.

Sehemu ya pili ya karne ya 20 iliona vita vipya vya wenyewe kwa wenyewe vilivyoendelea hadi mwaka 2016. Sehemu za nchi zilikuwa chini ya wanamgambo wanaodumisha utawala wao kwa biashara ya madawa ya kulevya, hasa kokain.

Wakazi hariri

Kuna wakazi milioni 41: wengi wako mjini hasa katika mabonde ya Rio Cauca na Rio Magdalena na kwenye mwambao wa bahari ya Karibi. Mwaka 2014 asilimia 76 za wakazi wote wa nchi walikaa mjini.

Kuna uhamiaji mkubwa kutoka mashambani kuelekea mjini. Mikoa ya mashariki ina zaidi ya nusu ya eneo la taifa lakini asilimia 3 za wakazi pekee.

Asili ya wakazi ni ya mchanganyiko wa vikundi vitatu:

Sehemu kubwa ni machotara wa Waindio na Wazungu (takriban 49%), halafu Wazungu (37%), machotara wa Kiafrika na Wakolombia wenye asili tupu ya Afrika (10.6%). Wenye asili tupu ya Waindio ni 3.4%.

Lugha rasmi na ya kawaida ni Kihispania (99.2%).

Upande wa dini, asilimia 90 ni Wakristo, hasa wa Kanisa Katoliki (70.9%) na wa madhehebu mbalimbali ya Uprotestanti (16.7%).

Tazama pia hariri

Viungo vya nje hariri

 
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
Nchi na maeneo ya Amerika Kusini

Argentina | Bolivia | Brazil | Chile | Ekuador | Guyana | Guyani ya Kifaransa | Kolombia | Paraguay | Peru | Surinam | Uruguay | Venezuela

  Makala hii kuhusu maeneo ya Amerika Kusini bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Kolombia kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.