Alhamisi kuu ni sikukuu ya Ukristo inayoadhimisha saa za jioni ile karamu ya mwisho ya Yesu Kristo na mitume wake kabla hajakamatwa na kuhukumiwa na kuhani mkuu wa Israeli, Yosefu Kayafa na hatimaye kukabidhiwa kwa liwali Ponsio Pilato ili asulubiwe.

Karamu ya Kiroho ilivyochorwa na Simon Ushakov (1685).
"Karamu ya mwisho", kazi ya mchongaji Master Paul.
Mwaka wa liturujia
Magharibi
Mashariki
Picha takatifu ya Kiorthodoksi inayomuonyesha Kristo akiwaosha miguu Mitume wake (shule ya uchoraji ya Pskov, karne ya 16).
Askofu Sebouh Chouldjian (Kanisa la Kitume la Armenia) akimuosha miguu mtoto.

Katika karamu hiyo Yesu alitoa maneno yake ya buriani kwa wanafunzi hao akikazia amri mpya ya kwamba wapendane jinsi yeye alivyowapenda upeo, inavyosimuliwa hasa katika Injili ya Yohane ambayo inaripoti hotuba ndefu kutoka kwa Yesu wakati huo.

Umuhimu wa tukio hilo unasisitizwa hasa na madhehebu yanayoamini kuwa ndipo Yesu Kristo alipoweka sakramenti ya ekaristi (na ya upadri), inavyosimuliwa katika Injili nyingine tatu. Humo ni wazi kwamba karamu hiyo ilikuwa ya Pasaka ya Kiyahudi, lakini Yesu aliitia maana mpya kuhusiana na kifo na ufufuko wake, akisema, "Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu" (badala ya kuendelea kuwa ukumbusho wa Musa na jinsi alivyowakomboa Waisraeli kutoka Misri).

Tangu hapo Wakristo hawajaacha kufanya mara kwa mara, na hata kila siku, ibada hiyo ambayo imeitwa "Liturujia ya Kimungu", "Misa", "Karamu ya Bwana" na kwa majina mengine. Hata hivyo kuna uzito wa pekee kuifanya katika Juma Kuu, wakati uleule wa Yesu kuianzisha, yaani Alhamisi kabla ya Pasaka, saa za jioni.

Tarehe ya adhimisho hilo inabadilikabadilika kila mwaka pamoja na ile ya Pasaka, lakini inaangukia daima kati ya tarehe 19 Machi na 22 Aprili. Kwa Waorthodoksi wanaofuata kalenda ya Juliasi tarehe hizo ni sawa na tarehe 1 Aprili na 5 Mei ya kalenda ya kawaida.

Adhimisho la karamu ya mwisho, ambalo kwa kawaida linaendana na kutawadha miguu ya wanaume 12 (au ya watu kadhaa bila kujali jinsia) kwa kuiga tendo la Yesu, ndio mwanzo wa siku tatu kuu za Pasaka ambazo kilele chake ni kesha la usiku wa Pasaka, Yesu anaposadikiwa na Wakristo kuwa amefufuka mtukufu.

Viungo vya nje hariri

  Makala hii kuhusu dini ya Ukristo bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Alhamisi kuu kama historia yake, matokeo au athari zake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.