Kanisa la Anglikana la Tanzania


Kanisa Anglikana la Tanzania ( ACT ) ni jimbo la Jumuiya Anglikana Duniani. Makao makuu yake yako Dodoma. Lina dayosisi 28 ambazo ziko 27 Tanzania bara na 1 iko Zanzibar. Kila dayosisi huongozwa na askofu wake.

Hadi mwaka 1970, Waanglikana wa Tanzania walikuwa sehemu ya Jimbo la Afrika ya Mashariki pamoja na Kenya hadi kuanzishwa kwa majimbo ya pekee kila upande.

Askofu Mkuu wa Kanisa Anglikana Tanzania tangu mwaka 2018 ni Maimbo Mndolwa. [1]

Jina rasmi hariri

Baada ya kutoka kwenye Jimbo la Afrika Mashariki mnamo 1970 hadi 1997, lilijulikana kama "Kanisa la Jimbo la Tanzania". Sasa jina rasmi ni "Kanisa Anglikana la Tanzania", au ACT (Anglican Church of Tanzania).

Historia hariri

 
James Hannington alikuwa askofu wa kwanza wa Afrika ya Ikweta ya Mashariki.

Tanganyika hariri

Asili ya kanisa hilo iko katika Dayosisi ya Afrika ya Ikweta ya Mashariki ( Uganda, Kenya, Tanzania) iliyoanzishwa mnamo 1884, James Hannington akiwa askofu wa kwanza.

Shughuli za kimishonari za Kianglikana zilikuwepo katika eneo hilo tangu 1864 wakati ambapo mashirika ya Universities' Mission to Central Africa (UMCA) na Church Missionary Society (CMS) zilipoanza kazi huko Mpwapwa. Mnamo 1898, dayosisi hiyo iligawiwa ilhali upande mmoja uliendelea kuwa Kanisa Anglikana la Uganda, na mwingine kuwa dayosisi mpya ya Mombasa ikitawala Kenya na Tanganyika.

Dayosisi ya Masasi kusini mwa Tanzania ilianzishwa mnamo 1926.

Mnamo 1927 maeneo mengine ya Tanganyika yalitengwa na Mombasa kuwa Dayosisi ya Tanganyika ya Kati iliyojumuisha theluthi mbili za nchi hiyo.

Askofu wa kwanza alikuwa George "Jerry" Chambers, aliyewekwa wakfu mnamo 1927. [2] William (Bill) Wynn-Jones alikuwa askofu wa pili wa Tanganyika ya Kati.

Mnamo 1955, maaskofu wa kwanza wa Kiafrika wa dayosisi hiyo, Wakenya Festo Olang' na Obadiah Kariuki, na Mtanganyika Yohana Omari waliwekwa wakfu na Askofu Mkuu wa Canterbury, Geoffrey Fisher, nchini Uganda kama maaskofu wasaidizi. Mnamo 1964, John Sepeku alikuwa askofu wa dayosisi mpya ya Dar es Salaam (ambaye hapo awali alikuwa askofu msaidizi wa Zanzibar).

Mnamo 1960, Jimbo la Afrika Mashariki, lililojumuisha Kenya na Tanganyika, liliundwa. Jimbo la Afrika Mashariki liligawiwa kuwa Kenya na Tanzania, mnamo 1970 na jimbo la Tanzania liliundwa na John Sepeku kama askofu mkuu wa kwanza.

Zanzibar hariri

 
Mwonekano wa kanisa kuu la Christ Church, Zanzibar.

Dayosisi ya Zanzibar ilianzishwa mnamo 1892, na iliendelezwa kuwa dayosisi ya pekee. Tofauti na lile la Afrika ya Ikweta ya Mashariki, ambalo lilienezwa na wamisionari wenye mwelekeo wa Kiinjili, Zanzibar iliongozwa na wamisionari wa mweleko wa Anglikana-Katoliki.

Maeneo ya Bara na Zanzibar yaliungana wakati Jimbo la Afrika Mashariki lilipoundwa.

Askofu wa kwanza wa Zanzibar alikuwa Charles Smythies, ambaye alihamishwa kutoka wadhifa wake wa awali kama Askofu wa Nyasaland mnamo 1892. Kanisa kuu la Zanzibar, lililoko Mji Mkongwe, Jiji la Zanzibar, ni jengo maarufu lililopokewa katika orodha ya urithi wa Dunia. Kihistoria dayosisi hiyo ilijumuisha pia maeneo ya bara katika Tanganyika. Mnamo mwaka 1963 ilibadilishwa jina kuwa Dayosisi ya Zanzibar na Dar es Salaam. Miaka miwili baadaye, mnamo 1965, Dar es Salaam ikawa dayosisi tofauti, na ile ya asili ikapewa tena jina la Dayosisi ya Zanzibar na Tanga. Mnamo 2001 sehemu zote za bara zilitengwa, na jina likarejeshwa kuwa Dayosisi ya Zanzibar. Dayosisi hiyo inaendelea kujumuisha kisiwa jirani cha Pemba . Kumekuwa na maaskofu kumi kutoka 1892 hadi 2020.

Maaskofu wakuu hariri

Mkuu wa kanisa la kitaifa ni Askofu Mkuu wa Tanzania. Makao ya askofu mkuu yalikuwa awali jijini Dodoma, lakini sasa yapo kwenye makao ya askofu yeyote atakayechaguliwa kuwa askofu mkuu. Askofu yeyote anayechaguliwa kama mkuu bado ni askofu wa dayosisi yake, pamoja na kuwa Askofu Mkuu wa Tanzania. Kumekuwa na maaskofu wakuu saba tangu Jimbo la Afrika Mashariki lilipogawanywa katika Majimbo ya Kenya na Tanzania mnamo 1970. [3]

Uanachama hariri

Leo, kuna Waanglikana wasiopungua 2,500,000 nchini Tanzania.

Vyama vya kujitegemea ndani ya kanisa ni pamoja na Umoja wa Akina Mama (MU), Shirika la Vijana la Anglikana Tanzania (TAYO) na Chama cha Uinjilisti cha Anglikana (AEA).

Taasisi za elimu zinazotawaliwa na Kanisa Anglikana ni Chuo Kikuu cha Mtakatifu Yohane kilichopo Dodoma, na Vyuo vya Theolojia St Phillip's kilichopo Kongwa, na St Mark's jijini Dar es Salaam.

Central Tanganyika Press (CTP) na Shirika la Fasihi (SKM, pia inajulikana kama Jumba la Vitabu la Dar es Salaam), ni taasisi za kanisa zinazojitegemea na zina jukumu kubwa katika maisha ya Kanisa Anglikana.

Dayosisi hariri

Mwaka 2020 jimbo la Tanzania lilikuwa na dayosisi 28. (Namba katika mabano inaonyesha mwaka wa kuanzishwa kwa dayosisi husika).

  1. Dayosisi ya Zanzibar (1892)
  2. Dayosisi ya Masasi (1926)
  3. Dayosisi ya Central Tanganyika (1927)
  4. Dayosisi ya South West Tanganyika (1952)
  5. Dayosisi ya Victoria Nyanza (1963)
  6. Dayosisi ya Morogoro (1965)
  7. Dayosisi ya Dar es Salaam (1965)
  8. Dayosisi ya Western Tanganyika (1966)
  9. Dayosisi ya Ruvuma (1971)
  10. Dayosisi ya Mount Kilimanjaro (1982)
  11. Dayosisi ya Kagera (1985)
  12. Dayosisi ya Mara (1985)
  13. Dayosisi ya Tabora (1989)
  14. Dayosisi ya Ruaha (1990)
  15. Dayosisi ya Mpwapwa (1991)
  16. Dayosisi ya Rift Valley (1991)
  17. Dayosisi ya Southern Highlands (1999)
  18. Dayosisi ya Tanga (2000)
  19. Dayosisi ya Kondoa (2001)
  20. Dayosisi ya Biharamulo
  21. Dayosisi ya Kibondo
  22. Dayosisi ya Kiteto (2009)
  23. Dayosisi ya Lake Rukwa (2010)
  24. Dayosisi ya Lweru (2006)
  25. Dayosisi ya Newala (2010)
  26. Dayosisi ya Rorya (2010)
  27. Dayosisi ya Shinyanga (2005)
  28. Dayosisi ya Tarime (2010)

Mafundisho na mapokeo hariri

Kanisa Anglikana la Tanzania linakubali ngazi tatu za utumishi: shemasi, kasisi na askofu. Hutumia nakala ya kitaifa ya Book of Common Prayer.

Kitovu cha mafundisho katika Kanisa la Anglikana la Tanzania ni maisha na ufufuo wa Yesu Kristo. Mafundisho ya msingi ya kanisa, au katekisimu, ni pamoja na:

Vyanzo vitatu vya mamlaka katika Kanisa Anglikana ni hasa maandiko, yakisaidiwa na mapokeo na akili. Vyanzo hivyo vitatu vinashikilia na kukosoana kwa nguvu. Usawa huu wa maandiko, mapokeo na akili unafuatana na kazi ya Richard Hooker, mtheolojia wa karne ya 16. Katika mafundisho ya Hooker, maandiko ndiyo njia kuu ya kufika kwenye mafundisho na mambo yaliyotajwa wazi katika maandiko yanakubaliwa kama ya kweli. Masuala ambayo ni tata yakiweza kusomwa kwa maana zaidi ya moja, yanatambuliwa kwa kutumia mapokeo ya kanisa, ambayo hukaguliwa kwa kutumia akili. [4]

Mahusiano ya Kiekumene hariri

Kama makanisa mengine mengi ya Anglikana, Kanisa Anglikana la Tanzania ni mshiriki wa Halmashauri ya Kiekumeni ya Makanisa Duniani. [5] Linashiriki pia katika umoja wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT).

Nafasi ya ACT ndani ya farakano la jumuiya ya Kianglikana hariri

Mnamo Desemba 2006 ACT ilijitangaza kuwa katika "ushirikiano usio kamili" na Kanisa Anglikana la Marekani (Episcopal Church of America) juu ya kuwekwa wakfu kwa watu wenye mapenzi ya jinsia moja wasio waseja na kuhusu kubariki ndoa za jinsia moja. ACT ilijiunga na dayosisi na majimbo katika jumiya Anglikana ambayo yanapinga kukubaliwa kwa nafasi ya wapendanao wa jinsia moja katika kanisa wakikutana kwenye mkutano ya GAFCON. Askofu Mkuu Valentino Mokiwa alihudhuria mkutano wa GAFCON huko Yerusalemu mnamo Juni 2008 akaunga mkono kutambua "Kanisa la Anglikana katika Amerika Kaskazini" lililojitenga na Kanisa Anglikana la Marekani, mnamo Juni 2009. Alifuatwa na Askofu Mkuu Jacob Chimeledya aliyesogea zaidi upande wa "upatanisho" uliofuatwa na Askofu Mkuu wa Canterbury Justin Welby. Mwaka 2016 maaskofu wa Tanzania waliamua kujiunga tena na mwelekeo wa kupinga mabadiliko hayo ya maadili. [6]

Tawi rasmi la GAFCON Tanzania lilizinduliwa tarehe 14 Agosti 2019, katika mkutano uliofanyika Dar es Salaam, uliowaunganisha maaskofu 10 wa jimbo hilo, pamoja na Askofu Mkuu wa zamani Jacob Chimeledya, na kuungwa mkono na askofu mkuu mstaafu Donald Mtetemela. Maaskofu hao walipatana kutohudhuria Mkutano wa Lambeth (unaokutanisha maaskofu wote wa Kiaglikana kila baada ya miaka 10) mnamo 2020 kwa sababu Askofu Mkuu wa Canterbury hakuadhibu majimbo ambayo yamekataa azimio la Lambeth la mwaka 1998 juu ya ujinsia wa binadamu. Askofu Mwita Akiri alichaguliwa kuwa mwenyekiti wa tawi katika hafla hiyo. Askofu Mkuu wa sasa Maimbo Mndolwa, licha ya kusaini Azimio la Yerusalemu, bado hajatangaza kujiunga rasmi na GAFCON Tanzania. [7]

Marejeo hariri

  1. "I will be Maimbo" - New Primate of Tanzania honours past as he ushers in new era, Anglican Communion News Service, 21 May 2018
  2. Markham, Ian S.; Barney Hawkins, IV, J.; Terry, Justyn; Nuñez Steffensen, Leslie (2013). The Wiley-Blackwell Companion to the Anglican Communion. John Wiley & Sons. ku. 255–. ISBN 978-1-118-32086-0. 
  3. Markham, Ian S.; Hawkins, J. Barney; Terry, Justyn; Steffensen, Leslie Nuñez (2013). The Wiley-Blackwell Companion to the Anglican Communion. John Wiley and Sons. ISBN 9781118320860. Iliwekwa mnamo 28 November 2014.  Check date values in: |accessdate= (help)
  4. Anglican Listening Archived 5 Julai 2008 at the Wayback Machine. Detail on how scripture, tradition, and reason work to "uphold and critique each other in a dynamic way".
  5. http://www.oikoumene.org/?id=3587 World Council of Churches
  6. Tanzania rejoins GAFCON, Anglican Ink, 19 April 2016
  7. Communiqué from Gafcon Tanzania, 14 August 2019, GAFCON Official Website

Viungo vya nje hariri