Mahmud II (kwa Kituruki cha Kiosmani : محمود ثاني Mahmud-ı sānī) (20 Julai 1785 - 1 Julai 1839) alikuwa Sultani wa 30 wa Milki ya Osmani aliyetawala miaka 31 kuanzia 1808 hadi kifo chake. Mahmud alikuwa mwana wa Sultani Abdül Hamid I. Wakati wake kama sultani inakumbukwa kwa kutoka kwa Ugiriki na Serbia katika utawala wa Kiosmani, ongezeko la mamlaka ya mtawala wa Misri Muhamad Ali Pasha na kuanzishwa kwa matengenezo ya kisiasa, kisheria, kijeshi na kiuchumi kama jaribio la kupunguza udhaifu wa milki yake kulingana na mataifa ya Ulaya.

Mahmud II.

Alielewa umuhimu wa majaribio ya kubadilisha mfumo wa kijeshi wa Waosmani yaliyoanzishwa na Sultani Selim III, mtangulizi na binamu wake. Selim aliwahi kuuawa na wanajeshi wa Janisari. Wajanisari walikuwa kikosi cha jeshi waliowahi kuwa na sifa kubwa karne mbili zilizopita walipozawadishwa kwa haki nyingi na mapato makubwa; ila tu katika mazingira ya karne ya 18 na 19 uwezo wao wa kijeshi ulizidi kupotea. Waliangalia kila badiliko kama tishio kwa uwezo na heshima yao pia waliwahi kupindua masultani mbalimbali waliojaribu kupunguza haki zao na kutumia mapato kwa vikosi vilivyolingana na majeshi ya Ulaya. Mwaka 1826 alikuta tena upinzani wa Wajanisari dhidi ya kuanzishwa kwa vikosi vipya vya jeshi; hapo Mahmud aliamua kutumia nguvu yote akaangamiza makambi yao kwa mizinga ya kisasa; Wajanisari waliuawa kwa maelfu na kosi lote lilifutwa.

Mahmud alirithi vita dhidi ya Urusi ambako hatimaye Waosmani walishindwa, walilazimishwa kukabidhi maeneo ya Moldavia ya leo kwa Urusi.

Baada ya uvamizi wa Wasaudia katika Makka na Madina alimtuma gavana wa Misri kurudisha miji chini ya mamlaka yake na hadi mwaka 1818 emirati ya kwanza ya familia ya Saudi ilibomolewa.

Katika sehemu za Ulaya za milki yake aliona majaribio ya wakazi Wakristo kujitafutia uhuru wao. Baada ya vita kali alipaswa kuvumilia uhuru wa Ugiriki na nusu uhuru wa Serbia kwenye mwaka 1830. Wakati huohuo sultani alipaswa kukubali uvamizi wa Ufaransa katika Aljeria iliyokuwa na hali ya jimbo la kujitawala la Waosmani.

Tangu mwaka 1830 sultani alipambana na uasi wa Muhamad Ali Pasha, gavana na mtawala wa Misri. Kisheria alikuwa gavana wa sultani, hali halisi alitawala Misri kama ufalme wake. Aliwahi kutekeleza mabadiliko katika siasa, uchumi na jeshi, hivyo jeshi lake liliweza kushinda lile la sultani. Mwaka 1832 jeshi la Muhamad Ali Pasha lilivamia Anatolia na kuelekea Istanbul. Mahmud II aliokolewa tu kwa kuingilia kwa Urusi na Uingereza waliomlazimisha Mmisri kwa matishio kurudisha jeshi lake kwake.

Ushindi wa maadui dhidi yake ulimwonyesha udhaifu wa milki yake. Mahmud alianzisha mabadiliko mengi. Aliimarisha mamlaka ya serikali kuu juu ya magavana wa majimbo. Aliajiri mafundi kutoka Marekani ili watengeneze manowari na meli za kisasa katika Uturuki. Aliagiza matumizi ya vitabu vya mafundisho kutoka Uingereza katika shule za jeshi ambako maafisa wote walipaswa kusoma. Alialika washauri wanajeshi kutoka nchi mbalimbali za Ulaya.

Kaburi la Mahmud II mjini Istanbul.

Mahmud II alianza kutembelea mwenyewe majimbo ya milki yake, hatua ambayo haikutokea kabla yake.

Alianzisha posta. Aliunda idara ya sheria katika serikali maana hakuacha tena kazi yote ya mahakama mikononi mwa maimamu wa kidini. Alianzisha shule za kwanza zisizokuwa za kidini tu. Alianzisha pia vyuo vya watumishi wa serikali na matibabu.

Aliaga Dunia mwaka 1839, wakati ambako jeshi la Muhamad Ali Pasha wa Misri lilipigana tena na jeshi la sultani.

Tazama pia hariri

Marejeo hariri

  •   media kuhusu Mahmud II pa Wikimedia Commons
  • Levy, Avigdor. "The Officer Corps in Sultan Mahmud II's New Ottoman Army, 1826–39." International Journal of Middle East Studies (1971) 2#1 pp: 21-39. online
  • Levy, Avigdor. "The Ottoman Ulema and the military reforms of Sultan Mahmud II." Asian and African Studies 7 (1971): 13-39.
  • Levy, Avigdor. "The Ottoman Corps in Sultan Mahmud II New Ottoman Army." International Journal of Middle East Studies 1 (1971): pp 39+
  • Palmer, Alan. The Decline and Fall of the Ottoman Empire (1992) ch 6
  Makala hii kuhusu mwanasiasa fulani bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Mahmud II kama wasifu wake, habari za maisha au kazi yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.