Malaria ni ugonjwa wa kuambukiza ambao unaenezwa na mbu wa jenasi Anopheles na kusababishwa na kidubini aina ya protisti Plasmodium.

Protista ya plasmodium jinsi inavyoonekana kwa hadubini: ndiyo inayosababisha malaria

Kutokana na uenezi wake katika nchi zinazotumia Kiswahili, mara nyingi ugonjwa huo huitwa "homa" tu, ingawa homa ni dalili yake mojawapo tu, pia kuna magonjwa mengi yanayosababisha homa.

Malaria inatokea katika maeneo ya kitropiki na yanayokaribia tropiki ikiwa ni pamoja na sehemu za Amerika, Asia na Afrika. Mwaka 2015 duniani kulikuwa na maambukizi milioni 214 ya malaria, [1] na watu 438,000 walikufa, wengi wao (90%) wakiwa barani Afrika, hasa watoto wachanga katika mataifa ya kusini kwa Sahara. [2]

Malaria ni mojawapo ya magonjwa yaliyoenea sana na ni tatizo kuu la afya ya umma. Kwa kawaida huhusishwa na umaskini, lakini pia ni sababu ya umaskini [3] na kikwazo kikubwa kwa maendeleo ya uchumi.

Spishi tano za vimelea vya Plasmodium huweza kumwambukiza binadamu; aina iliyo mbaya zaidi husababishwa na Plasmodium falciparum. Malaria inayosababishwa na Plasmodium vivax, Plasmodium ovale na Plasmodium malariae husababisha ugonjwa usio shadidi sana kwa binadamu na aghalabu haijui. Spishi ya tano, Plasmodium knowlesi, husababisha malaria kwa nyani aina ya makaku lakini inaweza pia kumwambukiza binadamu. Kundi hilo la spishi za Plasmodium linalosababisha ugonjwa kwa binadamu hujulikana kama vimelea vya malaria.

Kwa kawaida, watu hupata ugonjwa wa malaria kwa kung'atwa na mbu wa kike wa jamii ya Anopheles aliyeambukizwa. Mbu aina ya Anopheles pekee ndio wanaoweza kusambaza malaria, na ni lazima wawe wameambukizwa kupitia damu waliyofyonza kutoka kwa mtu aliyeambukizwa. Mbu akimng'ata mtu aliyeambukizwa, huchukua kiasi kidogo cha damu: damu hiyo huwa na vimelea vya malaria. Wiki moja baadaye, wakati mbu anapofyonza mlo wake mwingine wa damu, vimelea hivyo huchanganyika na mate ya mbu na kuingia katika mfumo wa damu ya anayeng'atwa.

Vimelea hivyo huzaa ndani ya seli nyekundu za damu, na kusababisha dalili kama vile anemia, maumivu kidogo ya kichwa, shida ya kupumua, takikadia, n.k., aidha kuna dalili nyingine za jumla kama vile homa, baridi, kichefuchefu, mafua, na katika hali mbaya zaidi kupoteza fahamu na hata kifo.

Maambukizi ya malaria yanaweza kupunguzwa kwa kuzuia kung'atwa na mbu kutumia vyandarua, dawa za kuzuia wadudu, au hatua za kudhibiti maenezi ya mbu kama vile kunyunyizia dawa za kuua wadudu ndani ya nyumba na kupiga mifereji kuondoa maji yaliyosimama ambapo mbu hutaga mayai yao.

Majaribio yamefanywa kuibuka na chanjo ya malaria bila mafanikio makuu, pamoja na kuibua mbinu za udhibiti wa kiajabu zaidi, kama vile kubadili viini tete vya mbu ili kuwafanya sugu kwa vimelea pia umefikiriwa. [4] Ingawa utafiti unaendelea, hakuna chanjo iliyopatikana hadi sasa inayotoa ulinzi wa hali ya juu dhidi ya malaria [5]; mwaka 2015 ile pekee iliyoruhusiwa kutumika nje ya majaribio ni RTS,S, ambayo inatolewa kwa kudunga sindano mara nne, na hata hivyo ina ufanisi mdogo (26%-50%) kulingana na chanjo nyingine. Hivyo dawa za kuzuia lazima zitumiwe bila kukoma ili kupunguza hatari ya kuambukizwa. Madawa hayo ya kuzuia maambukizi mara nyingi huwa ghali mno kwa watu wengi wanaoishi katika maeneo ambapo ugonjwa huu hupatikana kwa wingi.

Watu wazima wengi wanaoishi katika maeneo ambayo ugonjwa huo umeenea huwa na maambukizi ya muda mrefu ambayo hujitokeza mara kwa mara, na pia huwa na kinga kidogo; kinga hiyo hupunguka kadiri muda unavyosonga; watu wazima kama hao wanaweza kuambukizwa malaria kali ikiwa wameishi muda mrefu katika maeneo ambapo ugonjwa huo haujaenea. Wanashauriwa kuchukua tahadhari kamili wanaporejea katika maeneo ambapo ugonjwa huo umeenea.

Maambukizi ya malaria hutibiwa kwa kutumia dawa ya malaria, kama vile kwinini au vizalika vya atemisinin. Hata hivyo, vimelea vimekuwa sugu kwa nyingi ya dawa hizo. Kwa hiyo, katika baadhi ya maeneo ya dunia, dawa chache tu ndizo zilizo na uwezo wa kutibu malaria kwa ufanisi.

Ishara na dalili hariri

 
Dalili kuu za malaria.[6]

Dalili za malaria ni pamoja na homa, kutetemeka, athralgia (maumivu ya kifundo), kutapika, anemia (inayosababishwa na kuachana kwa chembechembe nyekundu za damu), hemoglobinuria, kuharibika kwa retina, [7] na mtukutiko wa maungo.

Dalili tambulika za malaria hutokea kwa namna ya mzunguko wa baridi ya ghafla ikifuatiwa na kutetemeka, kisha homa na kutokwa jasho kunakodumu kwa saa nne hadi sita: dalili hizo hujitokeza kila baada ya siku mbili kwa maambukizi ya P. vivax na P. ovale, huku ikijitokeza kila baada ya siku tatu kwa P. malariae. [8] P. falciparum yaweza kuwa na homa inayojitokeza kila baada ya saa 36-48 au homa isiyoshadidi lakini inayoendelea. Kwa sababu zisizofahamika vyema, lakini ambazo zinaweza kuhusiana na shinikizo ya hali ya juu katika fuvu la kichwa, watoto walio na malaria mara nyingi hudhihirisha mkao usiokuwa wa kawaida, ishara ya uharibifu wa ubongo. [9] Imegunduliwa kuwa malaria husababisha matatizo ya kutambua, hasa kwa watoto. Husababisha kuenea sana kwa anemia katika kipindi cha kukua haraka kwa ubongo na pia uharibifu wa moja kwa moja wa ubongo. Uharibifu huo wa kinurolojia hutokana na malaria ya ubongo ambayo ni hatari mno kwa watoto. [10] [11] malaria ya ubongo huhusishwa na weupe wa retina, [12] ambayo inaweza kuwa na manufaa kama ishara ya kutofautisha malaria na visababishi vingine vya homa. [13]

Spishi Mwonekano Dalili katika vipindi vinavyolingana Hudumu katika ini?
Plasmodium vivax
 
kila baada ya siku tatu ndio
Plasmodium ovale
 
Kila baada ya siku tatu ndio
Plasmodium falciparum
 
kila baada ya siku tatu hapana
Plasmodium malariae
 
kila baada ya siku nne hapana

Malaria kali husababishwa takriban kipekee na maambukizi ya P. falciparum: kwa kawaida hujitokeza kati ya siku 6-14 baada ya kuambukizwa. [14] Madhara ya ugonjwa wa malaria kali ni pamoja na kukosa fahamu na kifo ikiwa haitatibiwa-watoto wachanga na wanawake wajawazito hasa wamo hatarini. Splenomegali (kupanuka kwa wengu), maumivu makali ya kichwa, iskemia ya ubongo, hepatomegali (kupanuka kwa ini), hypoglisimia, na hemoglobinuria na kufeli kwa figo huweza kutokea. Kufeli kwa figo kunaweza kusababisha homa ya mkojo wa damu, ambapo hemoglobin kutoka katika chembechembe nyekundu za damu zilizosambaratika huvuja na kuingia katika mkojo. Malaria kali inaweza kuendelea kwa kasi na kusababisha kifo katika mudaa wa masaa kadhaa au masiku. [14] Katika hali mbaya zaidi ya ugonjwa huo viwango vya vifo vinaweza kuzidi 20%, hata kuwe na utunzi wa hali ya juu na matibabu. [15] Katika maeneo ambapo ugonjwa huo umeenea, mara nyingi matibabu si ya kuridhisha na kiwango cha jumla cha vifo vinavyosababishwa na malaria huwa kimoja kati visa kumi. [16] Baada ya muda mrefu, matatizo ya kukua yamerekodiwa kwa watoto ambao wameugua malaria kali. [17]

Malaria ya muda mrefu hutokana na P. vivax na P. ovale, lakini si katika P. falciparum. Hapa, ugonjwa huo unaweza kujitokeza tena miezi au miaka baada ya kuambukizwa kutokana na uwepo wa vimelea fiche katika ini. Kwa hivo, kueleza kuwa malaria imetibiwa kwa kutazama kutokuwepo kwa vimelea katika damu kunaweza kupotosha. Kipindi kirefu zaidi kati ya kuambukizwa vimelea na kujitokeza kwa dalili za ugonjwa kimeripotiwa kwa P. vivax kuwa miaka 30. [14] Inakadiriwa kuwa moja kati ya visa vitano vya malaria vinavyosababishwa na P. vivax katika maeneo ya hari huhusiana na kujihifadhi kwa vijimelea vya hipnoziti (yaani, dalili hujitokeza mwaka unaofuata kung'atwa na mbu). [18]

Sababu hariri

 
Spora ya Plasmodium huzunguka sitoplazimu ya seli epitheliumu ya utumbo wa kati ya mbu katika rangi hii bandia ya mikrografia eltroniki.

Vimelea vya malaria hariri

Vimelea vya malaria ni wa jenasi ya Plasmodium (Faila Apicomplexa). Katika binadamu malaria husababishwa na P. falciparum, P. malariae, P. ovale, P. vivax na P. knowlesi. [19] [20] P. falciparum ndiyo iliyoenea zaidi na huchangia takriban 80% ya maambukizi yote ya malaria, na pia inahusishwa na karibu 90% ya vifo vinavyotokana na malaria. [21] Vimelea vya spishi ya Plasmodium huambukiza pia ndege, mitambaazi, nyani, sokwe na panya. [22] Kumedhibitishwa maambukizi kadhaa ya wanadamu na spishi zinazoambukiza nyani malaria, yaani P. knowlesi, P. inui, P. cynomolgi, [23] P. simiovale, P. brazilianum, P. schwetzi na P. simium, hata hivyo, isipokuwa kwa P. knowlesi, hizo nyingine hazina umuhimu kwa afya ya umma. [24] Ingawa malaria ya ndege inaweza kuua kuku na batamzinga, ugonjwa huu hausababishi hasara kubwa kiuchumi kwa wafugaji wa kuku. [25] Hata hivyo, tangu kuingizwa kiajali na binadamu imeeneza ugonjwa na kuua idadi kubwa ya ndege wa Hawaii, ambao walikuwa wamekua katika mazingira bila kimelea hicho na kwa hivyo hawakuwa na kinga yoyote dhidi yake. [26]

Taratibu hariri

Mzunguko wa maisha ya Plasmodium na vekta wa mbu hariri

Kimelewa cha msingi (mahsusi) cha kimelea hicho na njia ya uenezi na vekta zake ni mbu jike wa jenasi ya Anopheles, binadamu na wanyama wengine wenye uti wa mgongo ni vimelewa wa ziada. Kwanza mbu wachanga humeza vimelea kwa kufyonza damu ya mwanadamu aliyeambukizwa kisha mbu huyo wa aina yaAnopheles hubeba mbegu za vimelea za Plasmodium katika matezi ya mate yao. Mbu huambukizwa baada ya kufyonza damu kutoka kwa binadamu aliyeambukizwa. Baada ya kumezwa, gameti za vimelea viliyofyonzwa pamoja na damu hujigawanya kwa msingi wa mbegu za kiume au za kike na kisha kuungana katika utumbo wa mbu. Hii hubuni ukineti inayopenya wambo wa utumbo wa mbu na kuzalisha uusisi katika ukuta wa utumbo. Uusisi inapopasuka, inatoa spora(sporozoites)vinayohama katika mwili wa mbu kuelekea katika matezi ya mate ya mbu, ambapo huwa tayari kumwambukiza binadamu mwingine. Aina hii ya maambukizi wakati mwingine hujulikana kama uhamisho kituo wa kabla(anterior station transfer). Spora huingizwa ndani ya ngozi, pamoja na mate, wakati mbu anapofyonza mlo wake mwingine wa damu.

Mbu jike tu ndio hufyonza damu, hivyo mbu wa kiume hawasambazi ugonjwa huo. Mbu jike wa jenasi ya Anopheles hupendelea kutafuta mlo usiku. Huanza kutafuta mlo giza linapoanza kuingia na kuendelea usiku kucha mpaka watakapopata mlo. Vimelea vya malaria pia vinaweza kuambukizwa kupitia kuongezwa damu, ingawa hii ni nadra.

Pathojenesisi hariri

 
Mzunguko wa maisha ya vimelea vya malaria katika mwili wa binadamu. Mbu anamwambukiza mtu kwa kufyonza mlo damu. Kwanza, spora huingia katika mfumo wa damu, na kuhamia ini. Huambukiza chembechembe za ini (hepatosaiti), ambapo huzaana kuwa merozoiti, kurarua chembe za ini, na kujipenyeza kurudi katika mfumo wa damu. Kisha, merozoiti huambukiza chembechembe nyekundu za damu, ambapo hukua katika umbo pete, kisha trofozoiti (awamu ya kula), kisha skizonti (awamu ya kula), kisha kurejea kuwa merozoitiVijiumbe vinayoitwa gameti pia huzalishwa, ambayo, kama ikivyonzwa na mbu, vitamwambukiza mdudu huyo na kuendelea na mzunguko wa uhai.

Malaria katika binadamu hupevuka katika awamu mbili: awamu ya eksoirithasitika na erithrasiti. Awamu ya eksoirithasitika inahusisha maambukizi ya mfumo wa ini, huku awamu ya erithrasiti inahusisha maambukizo ya seli nyekundu za damu. Mbu aliyeambukizwa anapodunga ngozi ya binadamu kufyonza mlo wa damu, spora katika mate ya mbu huingia katika mfumo wa damu ya binadamu na kuhamia katika ini. Katika muda wa dakika 30 ya kuwa mwilini mwa binadamu, spora huambukiza seli za ini, kujizidisha kwa uzazi nafsi na bila kusababisha dalili za ugonjwa kwa muda wa kati ya siku 6 na 15. Mara zinapoingia katika ini viumbe hivyo huzaana kwa maelfu ya merozoiti, ambazo, baada ya kupasuka kwa seli ya kimelewa wao, hujipenyeza ndani ya damu na kuambukiza chembechembe nyekundu za damu, na hivyo kuanza awamu ya erithrasiti katika mzunguko wa maisha. [27] Vimelea hutoka katika ini bila kutambulika kwa kujizungusha kwenye kiwambo cha seli ya ini ya kimelewa aliyeambukizwa. [28]

Ndani ya chembechembe nyekundu za damu, vimelea huendelea kuongezeka, kwa uzazi nafsi, mara nyingine hujipenyeza nje ya chembe wenyeji na kuvamia chembechembe nyekundu zilizokuwa hazijaambukizwa. Mizunguko kadhaa kama hiyo ya kujiongezea nguvu hutokea. Kwa hivyo, maelezo yanayofahamika ya kukumbwa na homa ya ghafla hutokea wakati merozoiti wanapojipenyeza na kuambukiza chembechembe nyekundu za damu.

Baadhi ya spora za P. vivax na P. ovale hazikui moja kwa moja kuwa merozoiti katika awamu ya eksoirithasitika, badala yake huzalisha hipnozoiti zinazobakia bwete kwa kipindi cha kati ya miezi kadhaa (aghalabu miezi 6-12) hadi urefu wa mpaka miaka mitatu. Baada ya kipindi cha kuwa bwete, vimelea hivyo hujiamilisha na kuzalisha merozoiti. Hipnozoiti zanahusika na kipindi kirefu cha kati ya kuambukizwa na cha maradhi, na kurejea tena kwa ugonjwa katika aina hizi mbili za malaria. [29]

Kimelea cha malaria kwa kiwango fulani hulindwa dhidi ya kushambuliwa na mfumo wa kinga mwili kwa sababu katika kipindi cha mzunguko wa maisha kinapoishi katika mwili wa mwanadamu, hukaa ndani ya ini na chembechembe nyekundu za damu na haionekani kwa urahisi kwa ufuatiliaji wa kinga mwili. Hata hivyo, chembechembe za damu zilizoambukizwa na zilizo katika mzunguko wa damu huharibiwa katika wengu. Ili kuepuka hali hii vimelea vya P. falciparum hutandaza protini inayonata juu ya chembechembe za damu zilizoambukizwa, hii husababisha chembechembe hizo kukwama kwenye kuta za mishipa ndogo ya damu, hivyo basi kutenga vimelea hivyo na mzunguko wa jumla na wengu. [30] Hali hii ya "kunata" ni sababu kuu inayochangia matizo ya kutokwa damuwakati wa malaria. Vena ndogo za endotheliumu (matawi madogo kabisa katika mzunguko wa damu) zinaweza kuzibwa na mkusanyiko wa chembechembe hizo za damu zilizoambukizwa. Kuzibwa kwa mishipa hii husababisha dalili kama zinazohusishwa na malaria ya kondo ya nyuma na malaria ya ubongo. Katika malaria ya ubongo chembechembe nyekundu za damu zilizotengwa zinaweza kuvunja kizuizi cha damu na ubongo hali inayoweza kupelekea kukosa fahamu. [31]

Ingawa protini gandishi ya uso wa chembechebe nyekundu za damu (iitwayo PfEMP1, yaani Plasmodium falciparum erythrocyte membrane protini 1) ziko wazi kwa mfumo wa kinga, hazisaidii kama kinga nzuri kwa minajili ya chanjo kwa sababu ya utofauti wao uliokithiri; kuna angalau aina 60 za protini ndani ya kimelea kimoja na ina tofauti zaidi katika jamii ya vimelea. [30] Kimelea hicho hujigeuza kati ya mchanganyiko mkubwa wa protini gandishi za uso PfEMP1, hivyo basi kuwa hatua moja mbele ya mfumo wa kinga unaoitafuta.

Baadhi ya merozoiti hugeuka kuwa gameti za kiume au za kike. Mbu anapong'ata ngozi ya mtu aliyeambukizwa, mara moja huwa na uwezo kufyonza gameti zilizo damuni. Muunganiko wa mbegu za kiume na kike za vimelea hutokea katika utumbo wa mbu, na hivyo kumfanya mbu kuwa kimelea cha msingi wa ugonjwa huo. Spora mpya hukua na kusafiri kuelekekea katika tezi ya mate ya mbu, na hivyo kukamilisha mzunguko. Wanawake wajawazito hasa huwa kivutio kwa mbu, [32] malaria kwa wanawake wajawazito ni kisababishi kikuu cha uzazimfu, vifo vya watoto wachanga na uzaaji wa watoto wasio na uzito unaostahili, [33] hasa katika maambukizi ya P. falciparum, lakini pia kutokana na maambukizi ya spishi nyingine, kama vile P. vivax. [34]

Uaguzi hariri

 
Mpako wa damu kutoka P. falciparum iliyokuzwa (K1 Strain). Chembechembe kadhaa nyekundu za damu zilizo na awamu ya pete ndani yazo. Karibu katikati kuna schizont na kushoto kuna trofozoiti.

Tangu Charles Laveran alipokiona kwa mara ya kwanza kimelea cha malaria katika damu mwaka wa 1880, [35] msingi wa uaguzi wa malaria umekuwa uchunguzi wa damu kwa hadubini.

Homa na mshtuko wa mwili huchukuliwa kimakosa kama aina ya malaria kali sana barani Afrika kiasi cha kutoshughulikia magonjwa mengine hatari. Katika maeneo ambapo malaria imeenea uwepo wa vimelea damuni hakutoshi kutoa uaguzi wa malaria kali kwa sababu uwepo wa vimelea unaweza kusababishwa na maradhi mengine yanayolingana na malaria. Uchunguzi wa hivi karibuni unapendekeza kuwa upimaji mwanga katika retina ni njia bora ya kuagua malaria (uwezo wa kijumla wa kupitisha mwangaza wa 95% na uwezo wa bainifu wa 90%) zaidi ya mbinu za kutegemea dalili au maabara katika utofautishaji baina ya malaria na magonjwa mengine.{ {1/}

Ingawa damu ni sampuli inayotumiwa mara nyingi kufanya uaguzi, mate na mkojo vimechunguzwa kama sampuli mbadala, inayoingiwa na vimelea chache. [35]

Uaguzi wa dalili hariri

Maeneo yasiyoweza kumudu angaa vipimo sahili vya kimaabara aghalabu hutegemea historia ya dalili za homa ambazo mgonjwa ataeleza kuamua kutoa tiba ya malaria. Kwa kutumia damu iliyopakwa Gemsa kutoka kwa watoto nchini Malawi, utafiti ulionyesha kwamba wakati uaguzi wa dalili (joto la mjiko, weupe wa shina la ukucha, na kupanuka kwa wengu) zilipotumika kama ishara ya tiba, badala ya kutumia dalili anazoeleza mgonjwa,kiwango cha uaguzi sahihi kiliongezeka kutoka 21 % hadi 41% na kutoa matibabu ya malaria kusikohitajika kukapungua vikubwa. [36]

Uchunguzi hadubini wa filmu za damu hariri

Njia ya kiiktisadi zaidi, inayopendelewa, na ya kuaminika kwa uaguzi wa malaria ni uchunguzi hadubini wa filmu za damu kwa sababu kila moja ya spishi nne za vimelea huwa na sifa bainifu. Kwa kawaida, aina mbili za filmu ya damu hutumika. Filmu nyembamba ni sawa na filmu ya damu za kawaida na huruhusu utambulisho wa spishi kwa sababu mwonekano wa vimelea huhifadhiwa vyema katika maandalizi hayo. Filmu nzito humruhusu mhadubini kuchunguza kiasi kikubwa cha damu na ni karibu mara kumi na moja rahisi kuonekana kuliko filmu nyembamba, kwa hivyo kutambua viwango vya chini ya maambukizi ni rahisi kwa kutumia filmu nzito, lakini mwonekano wa vimelea huwa umepotoa zaidi na hivyo kutofautisha kati ya spishi mbalimbali kunaweza kuwa vigumu zaidi. Kwa kuzingatia faida na mapungufu ya filmu nzito na nyembamba, ni muhimu kutumia filmu hizi mbili wakati wa kutafuta uaguzi bainifu. [37]

Kutoka kwa filamu nzito, mhadubini anaweza kuchunguza viwango vya vimelea (au uwepo wa vimelea) hadi kiwango cha chini cha 0.0000001% cha chembechembe nyekundu za damu. Utambuzi wa spishi unaweza kuwa vigumu kwa sababu trofozoiti ("umbo pete") za mapema maishani mwa vimelea zote hufanana na kamwe haiwezekani kutambua spishi kwa msingi wa umbo pete moja; utambulisho wa spishi hutegemea trofozoiti kadhaa.

Uchunguzi nyanjani hariri

Katika maeneo ambapo uchunguzi hadubini haupatikani, au ambapo wafanyakazi wa maabara hawana uzoefu katika uaguzi wa malaria, kuna vipimo antijeni ambavyo vinahitaji tone tu la damu. [38] Vipimo vya imunokromatografia (pia huitwa: Uaguzi Haraka wa Malaria, Uchanganuzi wa Kukamata Antijeni au "Dipsticks") vimetengenezwa, kusambazwa na kujaribiwa nyanjani. Vipimo hivi hutumia damu inayotolewa kidoleni au damu ya vena, kipimo kamilufu huchukua jumla ya dakika 15-20, na maabara haihitajiki. Upeo chini wa vipimo vya uaguzi haraka upo katika vimelea 100 / μl ya damu ikilinganishwa na uchunguzi hadubini kutumia filmu nzito ambapo upeo huo ni 5. Vipimo vya uaguzi haraka vya kwanza vilitumia P. falciparum glutamate dehydrogenase kama antijeni. [39] Nafasi ya PGluDH ilichukuliwa na P.falciparum lactate dehydrogenase, aina moja ya 33 kDa oxidoreductase [EC 1.1.1.27]. Ndicho kimeng'enya cha mwisho katika njia ya glaikoliti, na ni muhimu kwa uzalishaji ATP na pia ni mojawapo ya kimeng'enya kinachopatikana kwa wingi katika P.falciparum. PLDH haiendelei kuwa katika damu bali humalizika karibu wakati mmoja na vimelea kufuatia matibabu yaliyofanikiwa. Kutokuwepo kwa antijeni baada ya tiba hufanya upimaji wa pLDH muhimu katika kutabiri ikiwa matibabu hayakufaulu. Kwa jinsi hii, pLDH ni sawa na pGluDH. Uchanganuzi wa OptiMAL-IT unaweza kutofautisha kati ya P. falciparum na P. vivax kwa sababu ya tofauti ya kiantijeni kati ya kimeng'enya chao pLDH.

Mbinu za kimolekyuli hariri

Mbinu za kimolekyuli hupatikana katika baadhi ya maabara za kimatibabu na asei za uchanganuzi wa papo kwa hapo (kwa mfano, QT-NASBA inayotumia mmenyuko endelevu wa polimeresi ) [40]zinaendelea kuandaliwa kwa matumaini ya kuzisambaza katika maeneo ambapo ugonjwa huo umeenea.

Vipimo haraka vya antijeni hariri

OptiMAL-IT inaweza kuchunguza kwa umadhubuti uwepo wa vimelea vya P. falciparum hadi chini ya 0.01% na vimelea visivyo falciparum hadi 0.1%. Para check-PF huweza kuchunguza vimelea chini ya 0.002% lakini haiwezi kutofautisha kati ya malaria inayoambukizwa na falciparum na isiyoambukizwa na falciparum. Asidi za viiniseli vya vimelea hugunduliwa kutumia mmenyuko endelevu wa polimeresi. Mbinu hii ni sahihi zaidi kuliko uchunguzi hadubini. Hata hivyo, ni ghali, na inahitaji maabara maalumu. Pia, uwepo wa vimelea si lazima uwiane na kukua kwa ugonjwa, hasa wakati kimelea kinaweza kujigandisha katika kuta za mishipa ya damu. Kwa hivyo, vifaa zaidi vilivyo na uwezo wa kupima mabadiliko madogo na visivyohitaji teknolojia ya hali ya juu vinafaa kubuniwa ili kugundua uwepo wa vimelea vya viwango vya chini nyanjani. [41]

Kuzuia hariri

 
Mbu aina ya Anopheles Albimanus afyonza mkono wa binadamu. Mbu huyu ni vekta wa malaria na udhibiti wa mbu ni njia madhubuti sana ya kupunguza matukio ya malaria.

Mbinu zinazotumiwa kuzuia kuenea kwa ugonjwa, au kulinda watu katika maeneo ambapo malaria imeenea ni pamoja na madawa ya kuzuia ugonjwa, kutokomeza mbu, na uzuiaji kung'atwa na mbu.

Kuendelea kuwepo kwa malaria katika eneo kunahitaji; mseto wa idadi kubwa ya binadamu, idadi kubwa ya mbu katika eneo moja, na viwango vya juu vya maambukizi kutoka kwa binadamu hadi kwa mbu na kutoka kwa mbu hadi kwa binadamu. Ikiwa hali hizi zote zitapunguzwa kwa viwango vya kutosha, bila shaka kimelea cha malaria kitatoweka kutoka katika eneo hilo, kama ilivyotokea Amerika ya Kaskazini, Ulaya sehemu kubwa ya Mashariki ya Kati. Hata hivyo, vimelea visipotokomezwa kutoka dunia nzima, vinaweza kujisitawisha tena ikiwa hali itarejea kuwa inayofaa kuzaana kwao. Nchi nyingi zinashuhudia ongezeko la idadi ya maambukizi ya malaria kutokana na usafiri na uhamaji mwingi.

Kwa sasa, hakuna kinga inayozuia malaria lakini utafiti unaendelea.

Watafiti wengi wanasema kuwa kinga ya malaria inaweza kuwa nafuu zaidi kuliko tiba ya ugonjwa huo kwa muda mrefu, lakini mtaji unaohitajika ni wa juu sana kwa watu wengi maskini duniani. Mshauri wa kiuchumi Jeffrey Sachs anakadiria kwamba malaria inaweza kudhibitiwa kwa msaada wa dola za Amerika bilioni 3 kila mwaka. Imesemekana kuwa, ili kufikia Malengo ya Maendeleo ya Milenia, pesa lazima zielekezwe kutoka katika juhudi za kutibu VVU / UKIMWI na kuelekezwa kuzuia malaria, ambayo kwa kiasi sawa cha fedha kutakuwa na manufaa makubwa kwa chumi za Afrika. [42]

Usambazaji wa ufadhili inatofautiana miongoni mwa mataifa. Nchi zenye idadi kubwa ya watu hazipokei kiasi sawa cha msaada. Nchi 34 zilizopokea msaada wa chini ya $ 1 kwa kila mtu kila mwaka ni baadhi ya mataifa maskini zaidi barani Afrika.

Brazili, Eritrea, India na Vietnam, tofauti na nchi nyingine zinazoendelea, zimefanikiwa kupunguza tatizo la malaria. Sababu zilizopelekea mafanikio katika mataifa hayo ni pamoja na mazingira mazuri ya nchi, mpangilio mahususi wa kiufundi unaotumia zana faafu kuwafikia walengwa, kufanya uamuzi kwa misingi ya utafiti, uongozi tendaji katika ngazi zote za serikali, kushirikisha jamii, ugatuzi wa utekelezaji na udhibiti wa fedha, wafanyikazi wa kiufundi na wa usimamizi wenye ujuzi katika ngazi ya taifa na nyanjani, kujishughulisha moja kwa moja kiufundi na kivitendo kwa mashirika wafadhili na fedha za kutosha na zinazopatikana kwa urahisi. [43]

Udhibiti Vekta hariri

Juhudi za kukomesha malaria na kutokomeza mbu zimefanikiwa katika baadhi ya maeneo. Kitambo malaria ilikuwa ugonjwa wa kawaida Amerika na Ulaya kusini lakini juhudi za kudhibiti vekta, pamoja na matibabu na ufuatiliaji wa binadamu walioambukizwa, ulikomesha ugonjwa huo katika maeneo hayo. Katika baadhi ya maeneo, kukomesha mitiririsho kwenye maeneo chepechepe ambapo mbu huzaliana na kuimarisha usafi kuliwezesha hali hiyo. Malaria ilitokomezwa kutoka kaskazini mwa Marekani mapema katika karne ya 20 kwa mbinu kama hizo, na matumizi ya kiuadudu cha DDT yaliutokomeza kutoka Kusini kufikia mwaka wa 1951. [44] Katika mwaka wa 2002, kuliripotiwa matukio 1059 ya malaria nchini Amerika, ikiwa ni pamoja na vifo vinane, lakini kati ya hayo yote, matukio matano tu ya ugonjwa huo yaliambukizwa ndani ya Amerika.

Kabla ya kuvumbuliwa kwa kiuadudu cha DDT,maeneo kadhaa ya kitropiki pia yalitokomeza au kudhibiti malaria kwa kuondoa au kusumisha maeneo ya mbu kuzaliana au maji ambamo lava huishi, kwa mfano kwa kumwaga au kujaza mafuta mahali maji yamesimama. Mbinu hizi hazijatumika vilivyo barani Afrika kwa zaidi ya nusu karne. [45] Katika miaka ya 1950 na 1960 kulikuwa na juhudi kubwa za afya ya umma kutokomeza ugonjwa wa malaria duniani kwa kulenga maeneo ambako malaria ilikuwa imeenea. [46] Hata hivyo, juhudi hizi hazijafaulu kutokomeza malaria katika sehemu nyingi zinazoendelea duniani, tatizo hilo limeenea zaidi barani Afrika.

Mbinu ya kutasisha mdudu inajitokeza kama mbinu ya kudhibiti mbu. Maendeleo kuelekea transijeni, au wadudu waliogeuzwa vinasaba, zinaonyesha kwamba mbu mwitu wanaweza kubadilishwa kuwa sugu kwa malaria. Watafiti katika Imperial College London walibuni mbu wa kwanza wa malaria ulimwenguni aliyegeuzwa vinasaba, [47] huku spishi wa kwanza sugu kwa Plasmodium akizinduliwa na watafiti kutoka Case Western Reserve University Ohio mwaka wa 2002. [48] Mafanikio ya kubadilisha kizazi cha sasa na kizazi kilicho na vinasaba vipya, yanategemea mfumo kadhaa, kama vile vipengele vinavyoweza kubadilishwa kuruhusu nadharia nyingine za jenetikia mbali na ya Mendel. Hata hivyo, mbinu hii ina matatizo mengi na mafanikio yako mbali mno. [49] Mbinu nyingine ya usoni zaidi ya kudhibiti vekta ni uwezekano wa kutumia mwanga wa leza kuua mbu wanaoruka. [50]Pia inadaiwa kuwa harufu ya ndege wafugwao ikiwapo kuku huweza kuwafukuza wadudu warukao ikiwamo mbu wa malaria[51]

Madawa ya kuzuia hariri

Madawa mengi ambayo hutumiwa kutibu malaria, yanaweza kutumika kuzuia. Kwa ujumla, dawa hizi hutumiwa kila siku au kila wiki, katika kipimo cha chini kuliko inavyofaa kutumiwa kutibabu mtu ambaye kweli ameambukizwa ugonjwa huo. Matumizi ya madawa ya kuzuia ni nadra kwa wakazi wa maeneo ambapo malaria imeenea, matumizi hayo kawaida huwa kwa wageni wa muda mfupi na wasafiri wanaotembelea maeneo ya malaria. Hii ni kutokana na gharama ya madawa hayo, athari mbaya kutokana na matumizi ya muda mrefu, na kwa sababu baadhi ya madawa madhubuti ya kupambana na malaria hayapatikani kwa rahisi nje ya mataifa tajiri.

Kwinini ilianza kutumika kama dawa ya kuzuia malaria (profilaksis) katika karne ya 17. Kubuniwa kwa madawa mbadala fanisi zaidi kama vile kwinakrini, klorokwini na primakwini katika karne ya 20, kulipunguza kutegemewa kwa kwinini. Siku hizi, kwinini bado inatumiwa katika kutibu malaria sugu inayoambukizwa na Plasmodium falciparum pamoja na kutibu malaria ya ubongo, lakini kwa kawaida haitumiki kama kizuia malaria.

Madawa ya kisasa yanayotumiwa kuzuia ni pamoja na mefloqine (Lariam), [[doxycycline/0} (inapatikana kwa urahisi), na mchanganyiko wa atovaquone na proguanil hydrochloride ya {0{/0} (Malarone).|doxycycline/0} (inapatikana kwa urahisi), na mchanganyiko wa atovaquone na proguanil hydrochloride ya {0{/0} (Malarone). Chaguo la dawa gani litumike hutegemea vimelea vilivyo sugu katika eneo hilo, athari ya dawa hiyo na maswala mengine. Dawa ya prophylactic haianzi kufanya kazi mara moja baada ya kumezwa, kwa hivyo watu wanaopanga kutembelea maeneo ambapo malaria imeenea kawaida huanza kutumia dawa hiyo wiki moja au mbili kabla ya kutembelea sehemu hizo na ni lazima waendeleae kuzitumia kwa wiki 4 baada ya kuondoka (isipokuwa atovaquone proguanil inayohitaji kuanza kutumiwa siku 2 kabla ya kusafiri na kuendelea siku 7 baadaye ya kuondoka).

Matumizi ya madawa ya kuzuia malaria katika maeneo ambapo mbu wanaoambukiza malaria wanapatikana yanaweza kufanya mwili kuwa sugu katika kupata malaria. [52]

Unyunyizaji majumbani hariri

Unyunyizaji majumbani (IRS) ni hali ya kunyunyizia viuadudu kwenye kuta za ndani ya nyumba katika maeneo yaliyoathirika na malaria. Baada ya kufyonza, spishi nyingi za mbu hupumzika juu ya kitu kilicho karibu huku akimeng'enya mlo wake wa damu, kwa hivyo iwapo kuta za majumba zitanyunyuziwa viuadudu, mbu wanaopumzika huenda wakauawa kabla kumng'ata mhasiriwa mwingine, na kumhamishia vimelea vya malaria

Kiuadudu cha kwanza kilichotumika katika unyunyizaji majumbani (IRS) kilikuwa DDT. [44] Ingawa awali kilitumika kupambana na malaria pekee, matumizi yake yalienea kwa haraka na kuingia katika kilimo. Baada ya muda, dawa ya DDT ilianza kutumika hasa kwa lengo la kudhibiti wadudu kuliko kama dawa ya kuzuia ugonjwa kuenea na kutokana na matumizi haya makubwa katika kilimo kulizuka mbu sugu katika maeneo mengi. Usugu wa mbu wa aina ya Anopheles dhidi ya DDT unaweza kufananishwa na usugu wa bakteria kwa viuavijasumu. Matumizi ya kupindukia ya sabuni za kuua bakteria na viuavijasumu dhidi ya bakteria yalisabisha usugu kwa bakteria kwa viuavijasumu, sawa na jinsi unyunyizaj wa DDT wa kupundukia kwa mimea ulipelekea usugu wa mbu wa Anopheles kwa DDT. Katika miaka ya 1960, uenezaji wa habari kuhusu madhara ya matumizi ya kiholela ya DDT uliongezeka, jambo ambalo lilipelekea matumizi ya DDT katika kilimo kupigwa marufuku katika nchi nyingi katika miaka ya 1970. Kwa kuwa matumizi ya DDT katika kilimo yamepungua au kupigwa marufuku kwa muda, DDT sasa inaweza kuwa njia ya kufaa kama hatua ya kudhibiti ugonjwa.

Ingawa matumizi ya DDT kudhibiti malaria hayajawahi kupigwa marufuku na kwamba kuna viuadudu vingine vingi vinavyoweza kutumika kunyunyiza, baadhi ya wanaharakati wamedai kwamba marufuku haya yamesababisha vifo vya mamilioni ya watu katika nchi za kitropiki ambapo DDT iliwahi kuwa madhubuti katika kudhibiti malaria. Fauka ya hayo, matatizo mengi yanayokurubishwa na matumizi ya DDT yanatokana na matumizi yake kwa viwango pana katika kilimo, wala si matumizi yake katika afya ya umma. [53]

Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa sasa linashauri matumizi ya aina 12 tofauti za viuadudu katika operesheni za kunyunyiza. Hizi ni pamoja na matumizi ya DDT na msururu wa vibadala (kama vile pyrethroids Permethrin na deltamethrin), ili kupambana na malaria katika maeneo ambapo mbu wamekuwa sugu kwa DDT ili kupunguza kasi ya mabadiliko kuelekea usugu. [54] Matumizi haya ya viwango vidogo vya DDT katika afya ya umma yanaruhusiwa chini ya Mkataba wa Stolckholm wa Usimamizi wa Taka za Kemikali Zinazodumu katika Mazingira kwa Muda Mrefu (POPs), ambao unapiga marufuku matumizi ya DDT katika kilimo. [55] Hata hivyo, kwa sababu ya historia yake, nchi nyingi zilizoendelea zimewekea vikwazo matumizi ya DDT hata kwa viwango vidogo. [56] [57]

Tatizo mojawapo la aina zote za unyunyizaji wa viuadudu majumbani ni usugu unaotokana na mabadiliko ya mbu. Kulingana na utafiti uliochapishwa kuhusu Mosquito Behavior and Vector Control, spishi wa mbu wanaoathiriwa na IRS ni wale wanaopumzika na kuishi majumbani (endophilic), kutokana na mwasho unasababishwa na dawa za kunyunyizia, vizazi vyao wanabadilika kuelekea spishi wanaopumzika na kuishi nje (exophilic), kumaanisha hawaathiriki - ikiwa wanaathirika kwa vyovyote - na IRS, na kufanya mbinu hii kuwa isiyofaa kwa kiasi fulani katika kujilinda.

Vyandarua vya mbu na matandiko hariri

Makala kuu: Chandarua

Vyandarua vya mbu husaidia kutenga watu na mbu na kupunguza maambukizi na usambazaji wa malaria kwa kiwango kikubwa. Vyandarua si vizuizi kamilifu na mara nyingi hutiwa kiuadudu kilichotengenezwa kuua mbu kabla apate muda wa kutafuta upenyu wa kuingia ndani ya chandarua. Vyandarua vilivyotiwa dawa (Insectcide-Treated-Neta;ITN) vinakadiriwa kuwa na ufanisi mara mbili zaidi ya vyandarua visivyotiwa dawa, [42] na hutoa ulinzi zaidi ya 70% ikilinganishwa na kutotumia chandarua. [58]. Ingawa vyandarua vilivyotiwa dawa, ITN vimedhibitishwa kuwa na ufanisi dhidi ya malaria, chini ya 2% ya watoto katika miji ya mataifa ya Afrika iliyo Kusini kwa Sahara wanalindwa na ITN. Kwa sababu mbu wa Anopheles hufyonza damu usiku, njia inayopendekezwa ni kuning'iniza neti katikati ya kitanda hivi kwamba inafunika kitanda chote.

Usambazaji wa vyandarua vilivyotiwa viuadudu kama vile Pamethrin au deltamethrin umeonyesha kuwa ni mbinu madhubuti mno katika kuzuia malaria, na pia ni mojawapo ya mbinu yenye gharama nafuu zaidi. Vyandarua hivi vinaweza kupatikana kwa dola zipatazo 2,50-$ 3,50 (kati ya euro 2-3 ) kutoka kwa Umoja wa Mataifa, Shirika la Afya Duniani (WHO) na mashirika mengine. Vyandarua vilivyotiwa dawa (ITN) vimedhibitishwa kuwa mbinu yenye gharama nafuu zaidi katika kuzuia malaria na ni sehemu ya Malengo ya Maendeleo ya Milenia (Millennium Development Goals;MDGs) za WHO.

Kwa ufanisi zaidi, vyandarua lazima vitiwe viuadudu kila baada ya miezi sita. Mchakato huu hukumbwa na tatizo la ukosefu wa vifaa muhimu katika maeneo ya vijijini. Kuna teknolojia mpya kama Olyset au DawaPlus inayowezesha neti kudumu kwa muda mrefu(Long- Lasting Insecticide nets;LLIN),ambapo vyandarua hivyo hutoa viuadudu kwa takriban miaka 5, [59] na hugharimu takribani US $ 5.50. Vyandarua hivi huwalinda wanaovotumia na kuua mbu wanaogusa chandarua hicho. Watu wanaolala katika chumba kimoja na hawajajifunika kwa chandarua pia hupata ulinzi wa kiasi fulani.

Huku usambazaji wa vyandarua vya mbu ukiwa sehemu muhimu ya mbinu za kuzuia malaria, uelimishaji na uhamasishaji wa jamii kuhusu hatari za ugonjwa wa malaria huambatanishwa na kampeni za usambazaji ili kuhakikisha kuwa watu wanaopokea vyandarua wanajua jinsi ya kuvitumia. Kampeni za "Hang Up" kama zinazofanywa na wanaojitolea kuhudumu na shirika la Kimataifa la Red Cross na la Red Crescent Movement hushirikisha kutembelea miji ambayo ilipokea vyandarua ifikapo mwisho wa kampeni au kabla tu ya msimu wa mvua kuhakikisha kwamba chandarua kinatumika vizuri na kwamba watu walio hatarini zaidi ya kuambukizwa, kama watoto wachanga na wazee, wanalala chini neti. Utafiti uliofanywa na CDC nchini Sierra Leone ulionyesha ongezeko la asilimia 22 katika utumiaji wa chandarua kufuatia kutembelewa kibinafsi na mtu wa kujitolea anayeishi katika jamii hiyo. Utafiti nchini Togo ulionyesha hali bora sawa na hukSierra Leoneo. [60]

Gharama ya kutibu malaria huwa juu ikilinganishwa na mapato ya mgonjwa,na basi ugonjwa huo husababisha hali ya mtu kupoteza riziki yake. Mara nyingi vyandarua huwa ghali kwa watu katika nchi zinazoendelea, hasa kwa wengi walio hatari ya kuambukizwa. Mtu 1 tu katiya watu 20 huwa na chandarua cha mbu barani Afrika. [42] Vyandarua pia husambazwa wakati wa kampeni za kutoa chanjo kwa kutumia vocha za ruzuku, kama vile wakati wa kampeni za kuwachanja watoto dhidi ya surua.

Utafiti uliofanywa miongoni mwa wakimbizi wa Afghanistani nchini Pakistan ulibainisha kuwa kutia dawa ya permethrin kwenye matandiko na buibui (pamoja na hijabu) huwa na athari sawa na hali ya kutumia chandarua kilichotiwa dawa, lakini bei yake ni nafuu. [61] Mbinu nyingine mbadala hutumia spora za kuvu Beauveria bassiana kunyunyizia kuta na vyandarua ili kuua mbu. Japo baadhi ya mbu wamekua sugu kwa kemikali, haijapatikana kuwa wamekuwa sugu kwa maambukizi ya kuvu. [62]

Chanjo hariri

Makala kuu: Chanjo ya Malaria

Kingamaradhi (au, kwa usahihi zaidi, kuhimili malaria) hutokea kawaida, lakini baada ya maambukizi yaliyorudiwarudiwa na aina nyingi za malaria. [63]

Chanjo ya malaria inaendelea kufanyiwa utafiti na, hakuna chanjo madhubuti iliyopatikana hadi sasa. Ufafiti wa kwanza ulioonyesha uwezekano wa kupatikana kwa chanjo ya malaria ulifanyika mwaka wa 1967 kwa kumchanja panya na spora hai zilizodhoofishwa kwa mnunurisho, na ilitoa kinga kwa takriban 60% ya panya baadaye walipodungwa kwa spora hai zinazoweza kuambukiza. [64] Tangu 1970, kumekuwa na juhudi za kubuni chanjo kwa binadamu kutumia mikakati sawa na hiyo. Ilibainishwa kwamba mtu anaweza kupata kinga dhidi ya maambukizo ya P. falciparum ikiwa atang'atwa zaidi ya mara 1,000 na mbu walioambukizwa, ambao pia wamenunurishwa. [65]

Imekubaliwa kwa ujumla kwamba ni vigumu kutumia mkakati kama huo kutoa chanjo kwa watu walio hatarini kuambukizwa. Badala yake, kazi nyingi zimefanywa kujaribu kuelewa michakato ya kiimyunolojia inayotoa kinga baada ya kuchanjwa kwa spora iliyonunurishwa. Baada ya utafiti wa chanjo kwa panya mwaka wa 1967, [64] ilichukuliwa kinadharia kwamba spora zilizodungwa zilikuwa zikitambuliwa na mfumo wa kingamwili, ambao kwa upande wake ulikuwa ukiunda mazindikomwili (antibodies) dhidi ya vimelea. Ilidhibitishwa kwamba mfumo wa kingamwili ulikuwa ukibuni mazindikomwili dhidi ya protini ya circumsporozoite (CSP) iliyokuwa imeizunguka spora. [66] Aidha, mazindikomwili dhidi ya CSP yalizuia spora kuzivamia seli za ini (hepatocytes). [67] Hivyo basi CSP ilichaguliwa kama protini iliyokuwa na uwezekano zaidi wa kubuni chanjo dhidi ya spora ya malaria. Ni kwa sababu hizi za kihistoria ambapo chanjo zilizo na msingi katika CSP ni nyingi miongoni mwa chanjo za malaria.

Kwa sasa, kuna aina tofauti za chanjo zinazokaguliwa. Chanjo inayolenga vimelea kabla havijafikia damu (pre-erythrocytic), hasa chanjo ambazo misingi yake ni CSP, huchangia pakubwa la tafiti za chanjo ya malaria. Aina nyingine za tafiti za chanjo zinajumuisha: zile zinazotafuta kuweka kinga katika awamu ya kuambukizwa kwa damu; zinazotafuta kuepuka pathologia kali zaidi ya malaria kwa kuzuia kushikamana kwa vimelea katika mishipa ya damu au na chanjo dhidi ya uenezi utakaokomesha kukua kwa vimelea mwilini mwa mbu baada ya mbu kufyonza damu ya mtu aliyeambukizwa. [68] Inatarajiwa kwamba matokeo ya utafiti wa mpangilio wa jinomu ya P. falciparum uliomalizika mwaka wa 2002 [69], yatatoa mwelekeo kuhusu dawa au chanjo mpya. [70]

Chanjo ya kwanza ambayo imebuniwa na kufanyiwa majaribio nyanjani, ni SPf66, iliyoandaliwa na Manuel Elkin Patarroyo mwaka 1987. Inatoa mchanganyiko wa mazindikomwili chanjo kutoka kwa spora (kutumia marudio ya CS) na vimelea vya merozoiti. Katika awamu ya kwanza ya majaribio umadhubuti wa 75% ulipatikana na chanjo ikaonekana kuhimiliwa vizuri na watafitiwa na ilikuwa na uwezo wa kuanzisha kingamwili. Awamu za IIb na III ya majaribio haikuridhisha sana, umadhubuti ulishuka kwa kiwango cha kati ya 38.8% na 60.2%. Jaribio lilifanyika Tanzania mwaka wa 1993 na kuonyesha umadhubuti wa 31% baada ya kufuatilia wahusika kwa mwaka, hata hivyo hivi karibuni (ingawa kuna utata) utafiti uliofanywa nchini Gambia haukuonyesha madhara yoyote. Licha ya muda mrefu na tafiti nyingi zilizofanywa, bado haijulikani jinsi chanjo ya SPf66 hutoa kinga; kwa hivyo inawezekana isiwe ufumbuzi wa tatizo la malaria.

CSP ndiyo chanjo nyingine iliyobuniwa na ilionekana kuwa ingepitia majaribio. Pia msingi wake ni protini inayozunguka spora (circumsporoziote), lakini zaidi ya hivyo imeunganika na protini (Asn-Ala-Pro15Asn-Val-ASP-Pro) 2-Leu-arg (R32LR) kwa kufungamanisha elekroni pamoja na Pseudomonas aeruginosa tovin(A9) iliyosafishwa. Hata hivyo katika hatua za awali ukosefu kamili wa kinga kwa waliochanjwa ulidhihirika miongoni mwa waliochanjwa. Kundi la watafitiwa lililopewa dawa ya majaribio nchini Kenya lilikuwa na kiwango cha matukio ya maambukizi cha 82% huku kundi ambalo halikupewa chanjo likiwa na kiwango cha maambukizi cha 89%. Chanjo hiyo ililenga kuongeza seli za limfosayti T kwa waliochanjwa, hali ambayo haikutokea.

Umadhubuti wa chanjo ya Patarroyo umetiliwa shaka huku baadhi ya wanasayansi wa Marekani wakiandika katika The Lancet (1997) kwamba "chanjo hiyo si madhubuti na ni lazima itupiliwe mbali" huku raia huyo wa Kolombia akiwatuhumu kuwa na "kiburi" na kupuuzilia mbali madai yao na kuongeza kuwa wanafanya hivyo kwa sababu yeye anatoka katika taifa linaloendelea.

RTS, S/AS02A ni chanjo ambayo imebuniwa kwa ubia kati ya Mchakato wa PATH wa kutafuta Chanjo ya Malaria (PATH Malaria Vaccine Initiative) (unaofadhiliwa na Wakfu wa Gates, kampuni ya GlaxoSmithKline, na Walter Reed Army Institute of Research [71] Katika chanjo hiyo, sehemu ya CSP imeunganishwa na "S antigen" ya Virusi vya homa ya manjano B; {0 protini hii ya {0} mseto hudungwa pamoja na ajuvanti AS02A. [68] Mnamo Oktoba 2004, watafiti wa RTS, S/AS02A walitangaza matokeo ya Awamu ya majaribio ya IIb, iliyoonyesha chanjo hiyo ilipunguza hatari ya maambukizi kwa takribani 30% na ukali wa maambukizi kwa zaidi ya 50%. Utafiti huo uliwahusisha zaidi ya watoto 2,000 wa Msumbiji. [72] Majaribio yaliyofuata ya chanjo ya RTS, S/AS02A yalilenga usalama na umadhubuti wa kutoa chanjo hiyo kwa watoto. Katika mwezi wa Oktoba 2007, watafiti walitangaza matokeo ya awamu ya majaribio ya I / IIb yaliofanywa kwa watoto 214 wa Msumbiji wa kati ya umri wa miezi 10 na miezi 18 ambao walipokea vipimo kamili vitatu vya chanjo iliyopunguza maambukizi kwa 62% bila madhara makubwa isipokuwa tu uchungu wa kudungwa sindano. [73]

Njia nyinginezo hariri

Elimu kuhusu utambuaji dalili za malaria umepunguza idadi ya maambukizi katika baadhi ya maeneo ya nchi zinazoendelea kwa hadi kiasi cha 20%. Kutambua ugonjwa huo katika hatua za mapema pia kunaweza kuondoa hatari ya ungonjwa huo. Elimu pia inaweza kuwafundisha watu kufunika maeneo ambapo maji yamesimama, kwa mfano tangi ya maji ambayo ni sehemu bora ya kuzaliana kwa vimelea na mbu, hivyo kupunguza hatari ya maambukizi kwa watu. Hii hasa hutekelezwa katika maeneo ya miji ambako kuna sehemu kubwa zilizo na idadi ya watu wengi wanaoishi pamoja, kuna uwezekano wa maambukizi kutokea katika maeneo hayo.

Mradi wa Kudhibiti Malaria sasa unatumia muda ambapo watu hujitolea kote duniani wanapokuwa hawafanyi kazi (tazama Volunteer computing and BOINC) ili kujaribu modeli za madhara ya kiafya na mienendo ya maambukizi ili kupata njia bora au mchanganyiko wa mbinu kudhibiti malaria. Mbinu hii ya kuchanganua modeli hutegemea utumizi mpana wa kompyuta kwa sababu ya idadi kubwa ya watu kutoka sehemu mbalimbali walio na vigezo anuwai vya kibayolojia na sababu za kijamii zinazoathiri kuenea kwa ugonjwa. Inatarajiwa kuwa itachukua miezi michache kutumia nguvu za waliojitolea wanaotumia kompyuta ikilinganishwa na miaka 40 ambayo ingechukua kutumia rasilimali walizonazo sasa wanasayasi waliobuni mpango huo. [74]

Mfano wa umuhimu wa modeli za kompyuta katika kupangilia michakato ya kutokomeza ugonjwa wa malaria ni ulio katika chapisho la Aguas na wengine. Walibainisha kuwa kutokomeza malaria kunategemea sana kupata na kutibu idadi kubwa ya watu katika maeneo ambapo malaria imeenea na malaria isiyoonyesha dalili za ugonjwa (asymptomatic), ambayo huwa kama hifadhi ya maambukizi. [75] Vimelea vya malaria haviathiri wanyama na hivyo kutokomeza ugonjwa huo kutoka kwa binadamu kunatarajiwa kufanikiwa .

Hatua nyingine kwa ajili ya kudhibiti ugonjwa wa malaria ni pamoja na kutoa dawa kwa waathiriwa wengi na kinga ya muda.

Tiba hariri

Maambukizi ya P. falciparum hai ni hali ya dharura ya kiafya inayomhitaji muathiriwa kulazwa hospitalini. Maambukizi ya P. vivax, P. ovale au P. malariae mara nyingi huweza kutibiwa huku mgonjwa akiruhusiwa kurudi nyumbani. Matibabu ya malaria hujumlisha utoaji wa huduma za kiusaidizi pamoja na madawa maalum ya malaria. Mgonjwa wa malaria akitibiwa vizuri, anaweza kupata afueni kamili. [76]

Madawa ya malaria hariri

Makala kuu: Dawa za malaria

Kuna aina kadhaa ya madawa yanayotumika kutibu malaria. {0Aina ya Chloroquine{/0} ina bei nafuu sana, hadi hivi majuzi, ilikuwa madhubuti sana, jambo lililoifanya kuwa dawa ya malaria iliyopendelewa na wengi kwa miaka mingi katika sehemu nyingi za dunia. Hata hivyo, usugu wa Plasmodium falciparum kwa dawa ya Chloroquine kumeenea hivi karibuni kutoka Asia hadi Afrika, na kuifanya isiweze kutibu aina nyingi za Plasmodium hatari katika maeneo mengi ya dunia yaliyoathirika. {1/ Katika maeneo ambapo klorokwini bado ni madhubuti kuponyesha inabakia kuwa chaguzi ya kwanza. Kwa bahati mbaya, usugu dhidi ya chloroquine unahusishwa na usugu kwa madawa mengine kama quinine na amodaquine. [77]

Kuna dutu nyingine kadhaa zinatumiwa kutibu, na kwa kiasi, kuzuia (Prophylaxis). Madawa mengi yanaweza kutumiwa kwa madhumuni hayo mawili; dozi kubwa hutumiwa kutibu malaria. Kutolewa kwao kunategemea sana marudio ya matukio ya vimelea kuwa sugu katika eneo ambapo dawa inatumika. Dawa moja inayochunguzwa kwa madhumuni ya kutumiwa kama dawa ya malaria, hasa kutibu vimelea sugu ni beta blocker propranolol. Propranolol imepatikana kuwa na uwezo wa kuzuia Plasmodium kuingia katika chembechembe nyekundu za damu na kuanzisha maambukizi, vilevile huzuia vimelea kuzaana. Utafiti wa Desemba 2006 uliofanywa na Chuo Kikuu cha Northwestern ulipendekeza kuwa propranolol inaweza kupunguza dozi za dawa zinazotumika sasa kuwa na udhibiti mkuu dhidi ya P. falciparum kwa kiwango cha 5 - hadi 10, na kupendekeza jukumu la dawa mchanganyiko. [78]

Madawa ya malaria yanayopatikana kwa sasa ni pamoja na: [79]

Utengenezaji wa madawa uliwezeshwa na kufanikiwa kwa ukuzaji wa vimelea vya Plasmodium falciparum. [80] Hii ilifanikisha kujaribiwa kwa madawa mapya maabarani.

Dutu kutoka katika mmea Artemisia annua, ulio na msombo wa artemisinin au vizalika sanisi vyake (dutu isiyohusiana na kwinini), hutoa umadhubuti wa zaidi ya 90%, lakini kutolewa kwao hakutimizi mahitaji. [81] Utafiti mmoja nchini Rwanda ulionyesha kuwa watoto waliokuwa na maambukizi yasiyo kali ya P. falciparum walionyesha dalili na ishara chache za kuwa na vimelea katika siku ya 28 ya baada ya matibabu wakati walipopewa mchanganyiko wa amodiaquine na artesunate, badala ya kutolewa pekee (AU = 0.34). Hata hivyo, kuongezeka kwa usugu dhidi ya amodiaquine katika kipindi hiki cha utafiti pia ulibainisha. [82]

Kuanzia mwaka wa 2001, Shirika la Afya Duniani limependekeza kutumiwa kwa dawa mseto ya artemisinin combination therapy (ACT) kama tiba ya kwanza kwa malaria isiyo kali katika maeneo ambapo kuna usugu kwa madawa ya awali. Hivi karibuni WHO imetoa miongozo ya tiba ya malaria inayopendekeza aina nne tofauti za ACT. Ijapokuwa nchi nyingi, zikiwa ni pamoja na mataifa mengi ya Afrika, zimejumuisha mabadiliko hayo katika sera zao rasmi kuhusu matibabu ya malaria, gharama kubwa bado ni kikwazo katika utekelezaji wa ACT. Kwa sababu ACT hugharamu hadi mara ishirini ya dawa za zamani, zimebakia ghali kwa nchi nyingi ambako maleria imeenea. Kuna utata kuhusu sehemu ambayo artemisisn hulenga, ingawa tafiti za hivi karibuni zinadokeza kwamba SERCA, aina ya kalsiamu ambayo huelekezwa katika endoplasmic reticulum inaweza kuhusishwa na usugu wa artemisinin. [83] Vimelea vya malaria vinaweza kuwa sugu dhidi ya artemisinin na usugu unaweza kuletwa na mgeuko palepale wa SERCA. [84] Hata hivyo, tafiti nyingine zinadokeza kuwa mitokondria ndiyo inayolengwa sana na artemisinin na analogi zake. [85]

Ingawa kuna dawa madhubuti za malaria, ugonjwa huo unaendelea kuwa tishio kwa watu wanaoishi katika maeneo ambapo umeenea na wasioweza kupata dawa hizo madhubuti vyema mapema. Upatikanaji wa madawa na vituo vya afya, pamoja na gharama ya madawa, ni pingamizi kubwa. Médecins Sans Frontières inakadiria kwamba gharama ya kutibu mtu aliyeambukizwa malaria katika nchi ambapo ugonjwa huo umeenea ilikuwa kati ya $ 0.25 na 2.40 $ kwa kila dozi katika mwaka 2002. [86] Karibu watu milioni moja hufa kila mwaka kwa sababu ya kutoweza kununua dawa sahihi za malaria. [87]

Madawa ghushi hariri

Madawa ghushi changamano yamepatikana katika nchi kadhaa za Asia kama vile Kambodia, [88] Uchina, [89] Indonesia, Laos, Thailand, Vietnam na yametuhumiwa kusababisha vifo vingi ambavyo vingeepukwa katika nchi hizo. {3/ WHO imesema kwamba tafiti zimeonyesha kuwa hadi 40% ya madawa ya malaria yaliyo na msingi wa artesunate ni bandia, hasa katika kanda ya Greater Mekong na kuanzisha mpango wa kutoa onyo haraka kupitia habari kuhusu madawa ghushi kuripotiwa kwa kasi kwa mamlaka husika katika nchi shiriki. [90] Hakuna njia ya kuaminika kwa madaktari au watu wa kawaida kugundua dawa bandia bila msaada wa maabara. Makampuni yanajaribu kukabiliana na kuendelea kuwepo kwa dawa ghushi kwa kutumia teknolojia mpya kutoa usalama kutoka uzalishaji hadi usambazaji.

Uenezi hariri

 
Vifo kutokana na malaria mwaka 2012 (asilimilioni)
     0-0     1-2     3-54     55-325     326-679     680-949     950-1,358

Malaria husababisha karibu visa milioni 250 vya homa na takriban vifo nusu milioni kila mwaka. [91] Idadi kubwa ya visa hutokea kwa watoto chini ya umri wa miaka 5; [92] wanawake wajawazito hasa pia huwa hatarini. Licha ya jitihada za kupunguza maambukizi na kuongeza matibabu, kumekuwa na mabadiliko madogo katika maeneo ambapo hatari ya ungojwa huu upo tangu mwaka 1992. [93] Kwa hakika, ikiwa maambukizi ya malaria yataendelea kuongezeka kama ilivyo sasa, kiwango cha vifo kinaweza kuongezeka mara mbili katika miaka ishirini ijayo. [94] Takwimu sahihi hazijulikani kwa sababu kesi nyingi hutokea katika maeneo ya vijijini ambako watu hawana huduma za hospitali au pesa za kuwawezesha kupata huduma za afya. Kwa sababu hiyo, visa vingi havijarekodiwa.. [94]

Ingawa maambukizi ya pamoja ya VVU na malaria husababisha ongezeko la vifo, hili si tatizo kuu likilinganishwa na maambukizi ya pamoja ya VVU/kifua kikuu, kwa sababu magonjwa hayo mawili huathiri rika mbili tofauti, huku malaria ikiwa imeenea miongoni mwa watoto ,kifua kikuu kimeenea miongoni mwa watu wazima. [95] Ingawa maambukizi ya pamoja ya VVU/malaria huleta dalili zisizo kali zaidi zikilinganishwa na maambukizi ya pamoja ya VVU na TB, VVU na malaria huchangia kuenea kwa kila mmojawapo. Athari hii hutokana na malaria kuongeza wingi wa virusi mwilini huku VVU ikiongeza uwezekano wa mtu kuambukizwa malaria. [96]

Kwa sasa malaria imeenea katika ukanda wote wa ikweta, katika maeneo ya Amerika, sehemu nyingi za Asia, na sehemu kubwa ya Afrika, hata hivyo, ni katika mataifa ya Afrika kusini kwa Sahara ambapo 90% ya vifo vya malaria hutokea. [97] Usambaaji kijiografia wa malaria ndani ya maeneo makubwa ni changamano, maeneo yaliyo na malaria na yasiyo na malaria aghalabu hupakana.[98] Katika maeneo kame, mikurupuko ya malaria inaweza kutabiriwa kwa kiasi cha usahihi kwa kutazama ramani ya mvua. [99] Malaria imeenea zaidi katika maeneo ya vijijini kuliko miji; hii ni tofauti na homa ya kidingapopo ambayo inaenea zaidi katika mijini.[100] Kwa mfano, miji ya Vietnam, Laos na Kambodia kimsingi haina malaria, lakini ugonjwa huo upo katika maeneo mengi vijijini. [101] Tofauti na hivyo,katika Afrika malaria ipo katika maeneo ya mijini na vijijini, ingawa hatari yake ni ndogo katika miji. [102] Uenezi wa malaria duniani haujakadiriwa tangu miaka ya 1960. Hata hivyo, wakfu wa Wellcome Trust, ya Uingereza, umefadhili mradi waMalaria Atlas Project [103] kurekebisha hili, inatoa njia ya kisasa na imara zaidi ya kutathmini [[]]madhara/0} ya ugonjwa wa malaria sasa na baadaye .

Historia hariri

Malaria imewaambukiza binadamu kwa zaidi ya miaka 50,000, na Plasmodium huenda imekuwa kijasumu kwa binadamu tangu spishi hiyo ilipoanza kuishi. [104] Vimelea vinavyohusiana kwa karibu na vimelea vya malaria kwa binadamu vinapatikana miongoni mwa sokwe kwa wingi. [105] Maelezo kuhusu homa za kipekee za malaria yamenakiliwa katika maandiko ya kihistoria, kuanzia mwaka 2700 KK huko Uchina. [106] Neno malaria lina usuli wake katikaKiitaliano cha enzi ya kati: mala aria - "hewa mbaya"; ugonjwa huo zamani uliitwa ague au Marsh fever kutokana na ukuruba wake na mabwawa na maeneo ya kinamasi. [107] Kuna nyakati ambapo visa vya malaria vilikuwa vingi Ulaya na Amerika Kaskazini, ambako sasa ugongwa huo haujaenea [108] ingawa unaweza kuletwa na mgeni aliyesafiri kutoka nchi nyingine .

Tafiti za kisayansi kuhusu malaria zilipata mafanikio muhimu ya kwanza mwaka 1880, wakati daktari wa jeshi la Ufaransa Constantine Alphonse Laveran aliyekuwa akifanya kazi katika hospitali ya kijeshi nchini Algeria alipotambua kwa mara ya kwanza vimelea ndani ya chembechembe nyekundu za damu ya watu waliokuwa wakiugua malaria. Kwa hiyo, alipendekeza kwamba ugonjwa wa malaria unasababishwa na kiumbe huyo, mara ya kwanza kabisa ambapo kijiumbe mwenye seli moja (Protista) alitambuliwa kusababisha ugonjwa. [109] Kwa sababu hii na vumbuzi nyingine za baadaye , alipokea Tuzo ya Nobel ya Tiba mwaka 1907. Kimelea cha malaria kiliitwa Plasmodium na wanasayansi wa Kiitalia Ettore Marchiafava na Angelo Celli. [110] Mwaka mmoja baadaye, Carlos Finlay, daktari wa Kuba aliyekuwa akitibu wagonjwa wa homa ya manjano huko Havana, alitoa ushahidi madhubuti kuwa mbu walihusika katika kusambaza ugonjwa huo miongoni mwa binadamu. [111] Kazi hii ilifuata mapendekezo ya awali ya Yosia C. Nott, [112] na Patrick Manson kuhusu maambukizi ya homa ya mitoki. [113]

Hata hivyo, ilikuwa Mwingereza Sir Ronald Ross aliyekuwa akifanya kazi katika Presidency General Hospital Calcutta, ambaye hatimaye katika mwaka wa 1898 alidhibitisha kuwa malaria inasambazwa na mbu. Alifanya hivyo kwa kuonyesha kwamba spishi fulani za mbu husambaza malaria kwa ndege na kuchuja vimelea vya malaria kutoka katika matezi ya mate ya mbu ambao walikuwa wamefyonza ndege waliokuwa wameambukizwa. [114] Kwa kazi hii Ross alipokea Tuzo ya Nobel ya Tiba mwaka wa 1902. Baada ya kujiuzulu kutoka Indian Medical Service, Ross alifanya kazi katika chuo kilichokuwa kipya cha Liverpool School of Tropical Medicine na kuelekezwa juhudi za kudhibiti malaria katika nchi za Misri, Panama, Ugiriki na Morishash. [115] Matokeo ya Ross na Finlay baadaye yalithibitishwa na bodi ya matibabu iliyoongozwa na Walter Reed mwaka 1900, na mapendekezo yake kutekelezwa na William C. Gorgas katika hatua za kiafya zilizorchukuliwaatibiwa wakati wa ujenzi wa Mfereji wa Panama. Kazi hii ya afya ya umma iliokoa maisha ya maelfu ya wafanyakazi na ikasaidia kubuni mbinu zilizotumika katika kampeni za afya ya umma dhidi ya ugonjwa huu baadaye .

Tiba ya kwanza madhubuti dhidi ya malaria ilitoka katika gome ya mti wa mkwinini ambayo ina kwinini. Mti huu hukua kwenye miteremko ya Andes, hasa Peru. Dawa iliyoundwa kutokana na bidhaa hii asili ilitumiwa na wenyeji wa Peru kudhibiti malaria, Wajesuti walieneza matumizi haya hadi Ulaya katika miaka ya 1640, ambapo ilikubalika kwa haraka. [116] Hata hivyo, ilikuwa hadi 1820 ambapo kiambato tendi, kwinini, ilipofyonzwa kutoka gome ya mti, kuchujwa na kupewa jina na wanakemia wa Kifaransa Pierre Joseph Pelletier na Joseph Bienaimé Caventou. [117]

Mapema katika karne ya 20, kabla viuavijasumu kuvumbuliwa, Julius Wagner-Jauregg aligundua kwamba wagonjwa wa kaswende wangeweza kutibiwa kwa kuambukizwa kimakusudi kwa vimelea vya malaria; homa iliyosababishwa iliua spirochete za malaria, hatimaye kwinini ingetolewa kudhibiti malaria. Ingawa baadhi ya wagonjwa walikufa kutokana na malaria, hii ilidhaniwa kuwa afadhali kuliko kifo ambacho hakinge epukika kutokana na kaswende. [118]

Ingawa awamu ya maisha ya kimelea katika damu na katika mbu katika hatua ya mzunguko wa maisha ya kimelea cha malaria iligunduliwa karne ya 19 na mapema karne ya 20, ilikuwa katika miaka ya 1980 ambapo awamu fiche ya kimelea hicho katika ini ilipoonekana. [119] [120] Ugunduzi huu wa awamu fiche ya kimelea hatimaye ulieleza kwa nini watu wangeweza kuonekana wamepona malaria lakini wakaugua tena miaka baada ya vimelea kutoweka katika mfumo wa damu.

Shinikizo la kubadilisha jeni za malaria hariri

Makala kuu: Mageuko ya spishi

Malaria inakisiwa kuwa nashinikizo kubwa kwa jieni ya binadamu katika siku za hivi karibuni. [121] Hii ni kutokana na vifo vingi na maradhi yanayosababishwa na malaria, hasa spishi ya P. falciparum.

Ugonjwa wa seli mundu hariri

 
Matukio na vyanzo vya visa vya malaria mwaka 1996. [122]

Athari iliyotafitiwa sana ya vimelea vya malaria kwa jinomu ya binadamu ni ya ugonjwa wa damu wa kinasaba yaani ugonjwa wa seli mundu. Seli mundu husababisha ugonjwa, lakini hata walioathirika kwa kiwango kidogo kwa seli mundu huwa na kinga ya kutosha dhidi ya malaria.

Katika maradhi ya seli mundu, kuna mabadiliko katika jeni ya HBB, ambayo husimba viwango vidogo vya haemoglobin viitwavyo beta-globini. Aleli ya kawaida husimba glutamate katika sehemu ya sita ya protini ya beta-globini, ilihali aleli ya seli mundu husimba valine. Mabadiliko haya kutoka asidi amino inayoyeyuka majini hadi isiyoyeyuka majini husababisha kushikana kwa molekyuli za hemoglobini na upolimishaji wa hemoglobini ambao husababisha kuharibika kwa maumbo ya chembechembe nyekundu za damu kuwa katika umbo la "mundu". Chembe chembe kama hizo zilizoharibika umbo huondolewa haraka kutoka kwa damu, hasa katika wengu, ambapo huharibiwa na kuchakatwa tena.

Katika hatua ya merozoiti kwenye mzunguko wa uhai wao, vimelea vya malaria huishi ndani ya chembechembe nyekundu za damu, na umetaboli wavyo hubadili kemia ya ndani ya chembe chembe nyekundu za damu. Seli zilizoambukizwa kwa kawaida huishi hadi vimelea vizaane, lakini, ikiwa chembechembe nyekundu zina mchanganyiko wa mundu na hemoglobini ya kawaida, kuna uwezekano wa seli hizo kuangamizwa kabla vimelea kuzaa. Hivyo basi, watu walio na maumbo ya aina mbili ya seli nyekundu lakini moja ndiyo inayotambaa yaani aleli iliyogeuka, ijulikanayo kama seli mundu, wanaweza kuwa na kiwango cha chini cha anemia kisicho na athari kubwa, lakini pia uwezekano wa wao kuambukizwa na malaria huwa umepunguzwa kwa kiwango kikubwa. Huu ni mfano wa kipekee wa faida inayotokana na hali ya kuwa na namna mbili za jeni moja (heterozygote).

Watu walio na jeni ya aina moja ya damu iliyobadilika kabisa (Homozygous) huwa na ugonjwa kamili wa seli mundu ambao ni nadra kuishi zaidi ya umri wa kubaleghe. Hata hivyo, katika maeneo ambapo malaria imeenea, maenezi ya jeni inayosababisha seli mundu ni takribani 10%. Uwepo wa jeni nne zinazotoshelezana kwa pamoja (haplotype) za hemoglobini mundu unaashiria kwamba kumekuwa na mabadiliko ya kujitegemea ya jeni angalau mara nne katika maeneo ambayo malaria imeenea, hii inaonyesha faida ya mabadiliko katika maeneo hayo yaliyoathiriwa. Aidha kuna mabadiliko mengine ya jeni ya HBB yanayosababisha molekyuli za hemoglobini zilizo na uwezo wa kutoa kinga sawa na hiyo dhidi ya maambukizi ya malaria. Mabadiliko hayo husababisha hemoglobini ya aina za HbE na HbC, ambazo kwa kawaida hupatikana Kusini Mashariki mwa Asia na Afrika Magharibi, kwa usanjari huo.

Thalasemia hariri

Mabadiliko mengine yaliyothibitishwa yanayopatikana katika jinomu ya binadamu yanayohusiana na ugonjwa wa malaria ni yanayohusika katika kusababisha matatizo ya damu yajulikanayo kama thalasemia. Utafiti uliofanywa Sardinia na Papua New Guineaumeonyesha kwamba ueneaji wa jeni ya β-thalasemia unahusiana na kiwango cha kuenea kwa malaria miongoni mwa watu wa eneo fulani. Utafiti uliofanyiwa watoto zaidi ya 500 nchini Liberia ulibainisha kwamba wale waliokuwa na β-thalasemia walikuwa kiwango cha 50% cha kinga dhidi ya dalili za malaria. Tafiti nyingine kama hizo zimegundua uhusiano baina ya maenezi ya jeni na ueneaji wa malaria katika aina ya α + ya α-thalasemia. Inakadiriwa kuwa jeni hizi pia zimechaguliwa katika mfululizo wa mabadiliko ya binadamu.

Antijeni za Duffy hariri

Antijeni za Duffy ni antijeni zinazopatikana kwenye chembechembe nyekundu za damu na seli nyingine katika mwili na hufanya kazi kama kipokezi cha kemokini. Antijeni hiyo ya Duffy hudhihirika kwenye chembechembe za damu kwa kusimbwa na jeni za Fy (Fya, Fyb, Fyc nk). Kimelea cha malaria cha Plasmodium vivax hutumia antijeni za Duffy kuingia kwenye seli za damu. Hata hivyo, antijeni za Duffy zisidhihirike kwenye chembechembe nyekundu za damu (Fy-/Fy-). Aina hizi za muundojeni hutoa kinga kamili dhidi ya maambukizi ya kimelea cha P. vivax. Muundojeni huu ni nadra sana miongoni mwa wakazi wa Ulaya, Asia na Marekani, lakini hupatikana katika takribani wakazi wote wa kiasili wa Afrika Magharibi na Kati. [123] Hii inafikiriwa kusababishwa na kukumbana sana na vimelea vya P. vivax katika Afrika vikwi vichache vilivyopita.

G6PD hariri

Glucose-6-phosphate dehydrogenase (G6PD) ni kimeng'enya ambacho huzuia athari za msongo unaotokana na uoksidishaji chembechembe nyekundu za damu. Hata hivyo, upungufu wa kimeng'enya hicho kwa sababu za kijenetiki huongeza kinga dhidi ya malaria kali.

HLA na interleukin-4 hariri

HLA-B53 inahusishwa na kupunguzwa kwa hatari ya malaria kali. Molekyuli ya MHC hii huwawasilisha hatua ya ini na antijeni za spora kwa seli za T Interleukin-4, inayosimbwa na IL4, huzalishwa na seli za T zinazochochewa na hukuza kuzaana na utofautishaji seli B ambazo huzalisha zindikomwili. Utafiti uliofanywa miongoni mwa jamii ya Fulani wa Burkina Faso, ambao huwa na visa vya maambukizi ya malaria vichache na viwango vya juu vya zindikomwili dhidi ya malaria kuliko jamii jirani, uligundua kuwa aleli ya IL4-524 T inahusishwa na viwango vya juu vya zindikomwili dhidi ya antijeni za malaria, hali ambayo inaongeza uwezakano hii inaweza kuwa sababu ongezeko la kinga dhidi ya malaria. [124]

Usugu Kusini mwa Asia hariri

Vilima vya chini ya Mlima Himalaya na mabonde ya Terai ama ya Doon nchini Nepal na India huwa na visa vingi vya malaria kutokana na hali ya hewa ya joto na vinamasi vinavyohimiliwa wakati wa kiangazi na chemichemi inayotiririka kutoka vilima vya juu. Misitu iliyokuwa na malaria ilitunzwa kimakusudi na watawala wa Nepal kama mbinu ya kujihami. Binadamu waliojaribu kuishi katika eneo hili walikufa kwa wingi kuliko katika nyanda za juu zaidi au sehemu kame Tambarare za Ganges, hata hivyo, wenyeji wa Tharu walikuwa wameishi katika eneo hili kwa muda mrefu kiasi cha kuwa na kinga kupitia kwa mabadiliko katika jeni nyingi. Ndoaza tabaka au kabila zilionekana kufungia hali hiyo mingoni mwa wenyeji wa Tharu. Vinginevyo jeni hizi pengine zingekuwa zimesambaa karibu kote Kusini mwa Asia na kwingineko kwa sababu ya thamani yao dhahiri na kutokuwa na madhara ikilinganishwa na Anemia ya Seli Mundu.

Jamii na utamaduni hariri

 
Kliniki ya Malaria nchini Tanzania.

Malaria si ungonjwa unaohusishwa tu na umaskini bali pia husababisha umaskini na ni kikwazo kikubwa kwa maendeleo ya kiuchumi. Maeneo ya hali ya joto yameathirika zaidi, hata hivyo kiwango cha athari kamili ya malaria hufika katika baadhi ya maeneo yenye joto la wastani na misimu isiyotabirika Ugonjwa huu umehusishwa na athari mbaya za kiuchumi katika maeneo ambayo umeenea sana. Mwishoni mwa karne ya 19 na mapema katika karne ya 20, ugonjwa huu ndio uliosababisha kudorora kwa uchumi kwa majimbo ya kusini mwa Marekani. [125]. Ulinganisho wa Pato wastani la Taifa kwa kila mtu mnamo mwaka 1995, iliyorekebishwa kuzingatia tofauti za uwezo wa kununua, kati ya nchi zilizo na zisizo na malaria ulionyesha tofauti za aina tano($ 1.526 dola dhidi ya $ 8.268 USD). Katika nchi ambazo malaria inapatikana kwa wingi, Pato Wastani la Taifa kwa kila mtu limeongezeka (kati ya 1965 na 1990) kwa 0.4% tu kwa kila mwaka, ikilinganishwa na 2.4% kwa kila mwaka katika nchi nyingine. [126] Umaskini ni kisababishi na athari, hata hivyo, kwa sababu maskini hawana uwezo wa kifedha kuzuia au kutibu ugonjwa huo. Watu wa pato la chini nchini Malawi katika mwaka wa (1994) walitumia 32% ya pato lao la kila mwaka katika kugharamia ugonjwa huu ikilinganishwa na 4% ya watu wa pato la chini. Kijumla, athari ya kiuchumi ya malaria kwa Afrika inakadiriwa kugharimu dola za kimarekani $ billion 12 kila mwaka. Athari za kiuchumi ni pamoja na gharama za huduma za afya, siku za kazi kupotea kutokana na ugonjwa huu, siku kupotezwa katika elimu, uzalishaji kupungua kutokana na uharibifu wa ubongo kufuatia malaria ya ubongo, na hasara ya uwekezaji na utalii. [92] Katika baadhi ya nchi zilizo athiriwa sana na malaria, ugonjwa huu hugharimu hadi 40% ya fedha zilizotengwa kwa matumizi ya afya ya umma, kati ya 30-50% ya wagongwa waliolazwa, na hadi 50% ya wagonjwa wanaotibiwa na kuruhusiwa kurudi nyumbani. [127]

Marejeo hariri

  1. Malaria Facts. Centers for Disease Control and Prevention.
  2. "Malaria Fact sheet N°94". WHO. Retrieved 2 February 2016.
  3. Malaria: Disease Impacts and Long-Run Income Differences (PDF). Institute for the Study of Labor. Iliwekwa mnamo 2008-12-10.
  4. Yoshida S, Shimada Y, Kondoh D, et al. (2007). "Hemolytic C-type lectin CEL-III from sea cucumber expressed in transgenic mosquitoes impairs malaria parasite development". PLoS Pathog. 3 (12): e192. PMID 18159942. doi:10.1371/journal.ppat.0030192. 
  5. RTS,S vaccine protection rate
  6. WebMD Dalili za malaria Ilisashishwa Mwisho: 16 Mei 2007
  7. Beare NA, Taylor TE, Harding SP, Lewallen S, Molyneux ME (1 Novemba 2006). "Malarial retinopathy: a newly established diagnostic sign in severe malaria". Am. J. Trop. Med. Hyg. 75 (5): 790–7. PMC 2367432. PMID 17123967.  Unknown parameter |day= ignored (help); Check date values in: |date= (help)
  8. Malaria life cycle & pathogenesis. Archived 18 Januari 2008 at the Wayback Machine. Malaria katika Armenia. Ilitumiwa 31 Oktoba 2006.
  9. Idro, R; Otieno G, White S, Kahindi A, Fegan G, Ogutu B, Mithwani S, Maitland K, Neville BG, Newton CR. "Decorticate, decerebrate and opisthotonic posturing and seizures in Kenyan children with cerebral malaria". Malaria Journal 4 (57): 57. PMC 1326205. PMID 16336645. doi:10.1186/1475-2875-4-57. Retrieved 2007-01-21. 
  10. Boivin MJ (Oktoba 2002). "Effects of early cerebral malaria on cognitive ability in Senegalese children". J Dev Behav Pediatr 23 (5): 353–64. PMID 12394524. Archived from the original on 2011-07-18. Retrieved 2009-11-19.  Check date values in: |date= (help)
  11. Holding PA, Snow RW (2001). "Impact of Plasmodium falciparum malaria on performance and learning: review of the evidence". Am. J. Trop. Med. Hyg. 64 (1-2 Suppl): 68–75. PMID 11425179.  - Orodha tafuta))
  12. Maude RJ, Hassan MU, Beare NAV (Jun 2009). "Severe retinal whitening in an adult with cerebral malaria". Am J Trop Med Hyg 80 (6): 881 Extra |pages= or |at= (help). PMID 19478242.  Unknown parameter |day= ignored (help);
  13. Beare NAV, Taylor TE, Harding SP, Lewallen S, Molyneux ME (2006). "Malarial retinopathy: a newly established diagnostic sign in severe malaria". Am J Trop Med Hyg 75 (5): 790–797. PMID 17123967. 
  14. 14.0 14.1 14.2 Trampuz A, Jereb M, Muzlovic I, Prabhu R (2003). "Clinical review: Severe malaria". Crit Care 7 (4): 315–23. PMC 270697. PMID 12930555. doi:10.1186/cc2183. 
  15. Kain K, Harrington M, Tennyson S, Keystone J (1998). "Imported malaria: prospective analysis of problems in diagnosis and management". Clin Infect Dis 27 (1): 142–9. PMID 9675468. doi:10.1086/514616. 
  16. Mockenhaupt F, Ehrhardt S, Burkhardt J, Bosomtwe S, Laryea S, Anemana S, Otchwemah R, Cramer J, Dietz E, Gellert S, Bienzle U (2004). "Manifestation and outcome of severe malaria in children in northern Ghana". Am J Trop Med Hyg 71 (2): 167–72. PMID 15306705. 
  17. Carter JA, Ross AJ, Neville BG, Obiero E, Katana K, Mung'ala-Odera V, Lees JA, Newton CR (2005). "Developmental impairments following severe falciparum malaria in children". Trop Med Int Health 10 (1): 3–10. PMID 15655008. doi:10.1111/j.1365-3156.2004.01345.x. 
  18. Adak T, Sharma V, Orlov V (1998). "Studies on the Plasmodium vivax relapse pattern in Delhi, India". Am J Trop Med Hyg 59 (1): 175–9. PMID 9684649. 
  19. Mueller I, Zimmerman PA, Reeder JC (Juni 2007). "Plasmodium malariae and Plasmodium ovale--the "bashful" malaria parasites". Trends Parasitol. 23 (6): 278–83. PMID 17459775. doi:10.1016/j.pt.2007.04.009.  Check date values in: |date= (help)
  20. Singh B, Kim Sung L, Matusop A, et al. (Machi 2004). "A large focus of naturally acquired Plasmodium knowlesi infections in human beings". Lancet 363 (9414): 1017–24. PMID 15051281. doi:10.1016/S0140-6736(04)15836-4.  Check date values in: |date= (help)
  21. Mendis K, Sina B, Marchesini P, Carter R (2001). "The neglected burden of Plasmodium vivax malaria" (PDF). Am J Trop Med Hyg 64 (1-2 Suppl): 97–106. PMID 11425182. Archived from the original on 2009-03-26. Retrieved 2009-11-19. 
  22. Escalante A, Ayala F (1994). "Phylogeny of the malarial genus Plasmodium, derived from rRNA gene sequences". Proc Natl Acad Sci USA 91 (24): 11373–7. PMID 7972067. doi:10.1073/pnas.91.24.11373. 
  23. Garnham, PCC (1966). Malaria parasites and other haemosporidia. Oxford: Blackwell Scientific Publications. 
  24. Collins, WE; Barnwell, JW (2009). "Plasmodium knowlesi: Finally being recognized". J Infect Dis 199 (8): 1107–1108. PMID 19284287. doi:10.1086/597415.  More than one of |author1= and |last1= specified (help); More than one of |author2= and |last2= specified (help)
  25. Investing in Animal Health Research to Alleviate Poverty. Taasisi ya Utafiti wa Mifugo ya kimataifa. Permin A. na Madsen M. (2001) Appendix 2: review on disease occurance and imparct (smallholder poultry). Archived 18 Julai 2011 at the Wayback Machine. Ilitumika 29 Oktoba 2006
  26. Atkinson CT, Woods KL, Dusek RJ, Sileo LS, Iko WM (1995). "Wildlife disease and conservation in Hawaii: pathogenicity of avian malaria (Plasmodium relictum) in experimentally infected iiwi (Vestiaria coccinea)". Parasitology. 111 Suppl: S59–69. PMID 8632925. doi:10.1017/S003118200007582X. 
  27. Bledsoe, GH (
  28. Sturm A, Amino R, van de Sand C, Regen T, Retzlaff S, Rennenberg A, Krueger A, Pollok JM, Menard R, Heussler VT (2006). "Manipulation of host hepatocytes by the malaria parasite for delivery into liver sinusoids". Science 313 (5791): 1287–1490. PMID 16888102. doi:10.1126/science.1129720. 
  29. Cogswell FB (Januari 1992). "The hypnozoite and relapse in primate malaria". Clin. Microbiol. Rev. 5 (1): 26–35. PMC 358221. PMID 1735093.  Check date values in: |date= (help)[dead link]
  30. 30.0 30.1 Chen Q, Schlichtherle M, Wahlgren M (Julai 2000). "Molecular aspects of severe malaria". Clin. Microbiol. Rev. 13 (3): 439–50. PMC 88942. PMID 10885986. doi:10.1128/CMR.13.3.439-450.2000.  Check date values in: |date= (help)[dead link]
  31. Adams S, Brown H, Turner G (2002). "Breaking down the blood-brain barrier: signaling a path to cerebral malaria?". Trends Parasitol 18 (8): 360–6. PMID 12377286. doi:10.1016/S1471-4922(02)02353-X. 
  32. Lindsay S, Ansell J, Selman C, Cox V, Hamilton K, Walraven G (2000). "Effect of pregnancy on exposure to malaria mosquitoes". Lancet 355 (9219): 1972. PMID 10859048. doi:10.1016/S0140-6736(00)02334-5. 
  33. van Geertruyden J, Thomas F, Erhart A, D'Alessandro U (1 Agosti 2004). "The contribution of malaria in pregnancy to perinatal mortality". Am J Trop Med Hyg 71 (2 Suppl): 35–40. PMID 15331817. Archived from the original on 2010-04-03. Retrieved 2009-11-19.  Unknown parameter |day= ignored (help); Check date values in: |date= (help)
  34. Rodriguez-Morales AJ, Sanchez E, Vargas M, Piccolo C, Colina R, Arria M, Franco-Paredes C (2006). "Pregnancy outcomes associated with Plasmodium vivax malaria in northeastern Venezuela". Am J Trop Med Hyg 74 (5): 755–757. PMID 16687675. 
  35. 35.0 35.1 Sutherland CJ, Hallett R, CJ; Hallett, R (2009). "Detecting malaria parasites outside the blood". J Infect Dis 199 (11): 1561–1563. PMID 19432543. doi:10.1086/598857.  More than one of |last1= and |author= specified (help)
  36. Redd S, Kazembe P, Luby S, Nwanyanwu O, Hightower A, Ziba C, Wirima J, Chitsulo L, Franco C, Olivar M (2006). "Clinical algorithm for treatment of Plasmodium falciparum malaria in children". Lancet 347 (8996): 80. PMID 8551881. doi:10.1016/S0140-6736(96)90404-3. 
  37. Warhurst DC, Williams JE (1996). "Laboratory diagnosis of malaria". J Clin Pathol 49 (7): 533–38. PMID 8813948. doi:10.1136/jcp.49.7.533. 
  38. Pattanasin S, Proux S, Chompasuk D, Luwiradaj K, Jacquier P, Looareesuwan S, Nosten F (2003). "Evaluation of a new Plasmodium lactate dehydrogenase assay (OptiMAL-IT) for the detection of malaria". Transact Royal Soc Trop Med 97 (6): 672–4. PMID 16117960. doi:10.1016/S0035-9203(03)80100-1. 
  39. Ling IT., Cooksley S., Bates PA., Hempelmann E., Wilson RJM. (1986). "Antibodies to the glutamate dehydrogenase of Plasmodium falciparum". Parasitology 92,: 313–24. PMID 3086819. doi:10.1017/S0031182000064088. 
  40. Mens PF, Schoone GJ, Kager PA, Schallig HDFH., PF; Schoone, GJ; Kager, PA; Schallig, HD (2006). "Detection and identification of human Plasmodium species with real-time quantitative nucleic acid sequence-based amplification". Malaria Journal 5 (80): 80. PMID 17018138. doi:10.1186/1475-2875-5-80.  More than one of |last1= and |author= specified (help)
  41. Redd S, Kazembe P, Luby S, Nwanyanwu O, Hightower A, Ziba C, Wirima J, Chitsulo L, Franco C, Olivar M (2006). "Clinical algorithm for treatment of Plasmodium falciparum malaria in children". Lancet 347 (8996): 80. PMID 8551881. doi:10.1016/S0140-6736(96)90404-3. 
  42. 42.0 42.1 42.2 Hull, Kevin. (2006) "Malaria: Fever Wars". PBS Documentary[dead link]
  43. Barat L (2006). "Four malaria success stories: how malaria burden was successfully reduced in Brazil, Eritrea, India, and Vietnam". Am J Trop Med Hyg 74 (1): 12–6. PMID 16407339. 
  44. 44.0 44.1 http://www.cdc.gov/malaria/history/eradication_us.htm Centers for Disease Control. Eradication of Malaria in the United States (1947-1951) 2004.
  45. Killeen G, Fillinger U, Kiche I, Gouagna L, Knols B (2002). "Eradication of Anopheles gambiae from Brazil: lessons for malaria control in Africa?". Lancet Infect Dis 2 (10): e192. PMID 12383612. doi:10.1016/S1473-3099(02)00397-3. 
  46. Gladwell, Malcolm.. "The Mosquito Killer", The New Yorker, 2001-07-02. 
  47. Imperial College, London, "Scientists create first transgenic malaria mosquito", Archived 26 Septemba 2006 at the Wayback Machine. 2000/06/22.
  48. Ito J, Ghosh A, Moreira LA, Wimmer EA, Jacobs-Lorena M (2002). "Transgenic anopheline mosquitoes impaired in transmission of a malaria parasite". Nature 417 (6887): 387–8. PMID 12024215. doi:10.1038/417452a. 
  49. Knols et al., 2007
  50. Robert Guth. Rocket Scientists Shoot Down Mosquitoes With Lasers. WSJ.com. Iliwekwa mnamo 8 Julai 2009.
  51. HANS, RAPHAEL, "HARUFU YA KUKU HUFUKUZA MALARIA", A-Z 360 (in en-US), retrieved 2018-10-27 
  52. Roestenberg M, et al.Protection against a Malaria Challenge by Sporozoite Inoculation. New England J. Med. 361:468, 30 Julai 2009
  53. Tia E, Akogbeto M, Koffi A, et al. (2006). "[Pyrethroid and DDT resistance of Anopheles gambiae s.s. (Diptera: Culicidae) in five agricultural ecosystems from Côte-d'Ivoire]". Bulletin de la Société de pathologie exotique (1990) (in French) 99 (4): 278–82. PMID 17111979. 
  54. Indoor Residual Spraying: Use of Indoor Residual Spraying for Scaling Up Global Malaria Control and Elimination. Shirika la Afya Duniani, 2006.
  55. 10 Things You Need to Know about DDT Use under The Stockholm Convention
  56. The Stockholm Convention on persistent organic pollutants
  57. Rosenberg, Tina. ""What the world needs now is DDT"", New York Times, 2007-04-11. Retrieved on 2008-11-03. 
  58. Bachou H, Tylleskär T, Kaddu-Mulindwa DH, Tumwine JK (2006). "Bacteraemia among severely malnourished children infected and uninfected with the human immunodeficiency virus-1 in Kampala, Uganda". BMC Infect. Dis. 6: 160. PMC 1660577. PMID 17090299. doi:10.1186/1471-2334-6-160. 
  59. New Mosquito Nets Could Help Fight Malaria in Africa
  60. International Federation of Red Cross and Red Crescent Societies (200) "The winning formula - World Malaria Day Report 2009". Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-08-09. Iliwekwa mnamo 2009-11-19.
  61. Rowland M, Durrani N, Hewitt S, Mohammed N, Bouma M, Carneiro I, Rozendaal J, Schapira A (1999). "Permethrin-treated chaddars and top-sheets: appropriate technology for protection against malaria in Afghanistan and other complex emergencies". Trans R Soc Trop Med Hyg 93 (5): 465–72. PMID 10696399. doi:10.1016/S0035-9203(99)90341-3. 
  62. "Fungus 'may help malaria fight'", BBC News, 2005/06/09
  63. Färnert A, Williams TN, Mwangi TW, et al., A; Williams, TN; Mwangi, TW; Ehlin, A; Fegan, G; Macharia, A; Lowe, BS; Montgomery, SM; Marsh, K (2009). "Transmission‐dependent tolerance to multiclonal Plasmodium falciparum infection". J Infect Dis 200 (7): 1166–1175. PMID 19702508. doi:10.1086/605652.  More than one of |last1= and |author= specified (help)
  64. 64.0 64.1 Nussenzweig R, Vanderberg J, Most H, Orton C (1967). "Protective immunity produced by the injection of x-irradiated sporozoites of plasmodium berghei". Nature 216 (5111): 160–2. PMID 6057225. doi:10.1038/216160a0. 
  65. Hoffman SL, Goh LM, Luke TC, et al. (2002). "Protection of humans against malaria by immunization with radiation-attenuated Plasmodium falciparum sporozoites". J. Infect. Dis. 185 (8): 1155–64. PMID 11930326. doi:10.1086/339409. 
  66. Zavala F, Cochrane A, Nardin E, Nussenzweig R, Nussenzweig V (1983). "Circumsporozoite proteins of malaria parasites contain a single immunodominant region with two or more identical epitopes". J Exp Med 157 (6): 1947–57. PMID 6189951. doi:10.1084/jem.157.6.1947.  Unknown parameter |i pmid= ignored (help)
  67. Hollingdale M, Nardin E, Tharavanij S, Schwartz A, Nussenzweig R (1984). "Inhibition of entry of Plasmodium falciparum and P. vivax sporozoites into cultured cells; an in vitro assay of protective antibodies". J Immunol 132 (2): 909–13. PMID 6317752. 
  68. 68.0 68.1 Matuschewski K (2006). "Vaccine development against malaria". Curr Opin Immunol 18 (4): 449–57. PMID 16765576. doi:10.1016/j.coi.2006.05.004. 
  69. http://www.nature.com/nature/journal/v419/n6906/full/nature01097.html
  70. Gardner M, Hall N, Fung E, et al. (2002). "Genome sequence of the human malaria parasite Plasmodium falciparum". Nature 370 (6906): 1543. PMID 12368864. doi:10.1038/nature01097. 
  71. Heppner DG, Kester KE, Ockenhouse CF, et al. (2005). "Towards an RTS,S-based, multi-stage, multi-antigen vaccine against falciparum malaria: progress at the Walter Reed Army Institute of Research". Vaccine 23 (17-18): 2243–50. PMID 15755604. doi:10.1016/j.vaccine.2005.01.142. 
  72. Alonso PL, Sacarlal J, Aponte JJ, et al. (2004). "Efficacy of the RTS,S/AS02A vaccine against Plasmodium falciparum infection and disease in young African children: randomised controlled trial". Lancet 364 (9443): 1411–20. PMID 15488216. doi:10.1016/S0140-6736(04)17223-1. 
  73. Aponte JJ, Aide P, Renom M, et al. (Novemba 2007). "Safety of the RTS,S/AS02D candidate malaria vaccine in infants living in a highly endemic area of Mozambique: a double blind randomised controlled phase I/IIb trial". Lancet 370 (9598): 1543–51. PMID 17949807. doi:10.1016/S0140-6736(07)61542-6.  Check date values in: |date= (help)
  74. What is Malariacontrol.net. AFRICA@home. Jalada kutoka ya awali juu ya 2007-03-15. Iliwekwa mnamo 2007-03-11.
  75. Águas R, White LJ, Snow RW, Gomes MG (2008). "Prospects for malaria eradication in sub-Saharan Africa". PLoS ONE 3 (3): e1767. PMC 2262141. PMID 18335042. doi:10.1371/journal.pone.0001767. 
  76. [156] ^ If I get malaria, will I have it for the rest of my life? uchapishaji la CDC, Ilitumika 14 Novemba 2006
  77. Tinto H, Rwagacondo C, Karema C, et al., H; Rwagacondo, C; Karema, C; Mupfasoni, D; Vandoren, W; Rusanganwa, E; Erhart, A; Van Overmeir, C; Van Marck, E (2006). "In-vitro susceptibility of Plasmodium falciparum to monodesethylamodiaquine, dihydroartemsinin and quinine in an area of high chloroquine resistance in Rwanda". Trans R Soc Trop Med Hyg 100 (6): 509–14. PMID 16337665. doi:10.1016/j.trstmh.2005.09.018.  More than one of |last1= and |author= specified (help)
  78. Murphy S, Harrison T, Hamm H, Lomasney J, Mohandas N, Haldar K (Desemba 2006). "Erythrocyte G protein as a novel target for malarial chemotherapy". PLoS Med 3 (12): e528. PMID 17194200. doi:10.1371/journal.pmed.0030528.  Check date values in: |date= (help)
  79. Prescription drugs for malaria Ilipatikana 27 Februari 2007.
  80. Trager W, Jensen JB (1976). "Human malaria parasites in continuous culture". Science 193 (4254): 673–5. PMID 781840. doi:10.1126/science.781840. 
  81. Senior K (2005). "Shortfall in front-line antimalarial drug likely in 2005". Lancet Infect Dis 5 (2): 75. PMID 15702504. 
  82. Rwagacondo C, Karema C, Mugisha V, Erhart A, Dujardin J, Van Overmeir C, Ringwald P, D'Alessandro U (2004). "Is amodiaquine failing in Rwanda? Efficacy of amodiaquine alone and combined with artesunate in children with uncomplicated malaria". Trop Med Int Health 9 (10): 1091–8. PMID 15482401. doi:10.1111/j.1365-3156.2004.01316.x. 
  83. Eckstein-Ludwig U, Webb R, Van Goethem I, East J, Lee A, Kimura M, O'Neill P, Bray P, Ward S, Krishna S (2003). "Artemisinins target the SERCA of Plasmodium falciparum". Nature 424 (6951): 957–61. PMID 12931192. doi:10.1038/nature01813. 
  84. Uhlemann A, Cameron A, Eckstein-Ludwig U, Fischbarg J, Iserovich P, Zuniga F, East M, Lee A, Brady L, Haynes R, Krishna S (2005). "A single amino acid residue may determine the sensitivity of SER`CAs to artemisinins". Nat Struct Mol Biol 12 (7): 628–9. PMID 15937493. doi:10.1038/nsmb947. 
  85. Li W, Mo W, Shen D, Sun L, Wang J, Lu S, Gitschier J, Zhou B (2005). "Yeast model uncovers dual roles of mitochondria in action of artemisinin". PLoS Genet 1 (3): e36. PMID 16170412. doi:10.1371/journal.pgen.0010036. 
  86. Médecins Sans Frontières, "What is the Cost and Who Will Pay?"[dead link]
  87. Millions die because of high malaria drug prices - Yahoo! News.
  88. Lon CT, Tsuyuoka R, Phanouvong S, et al. (2006). "Counterfeit and substandard antimalarial drugs in Cambodia". Trans R Soc Trop Med Hyg 100 (11): 1019–24. PMID 16765399. doi:10.1016/j.trstmh.2006.01.003. 
  89. U. S. Pharmacopeia (2004). Fake antimalarials found in Yunan province, China (PDF). Jalada kutoka ya awali juu ya 2006-09-09. Iliwekwa mnamo 2006-10-06.
  90. Jane Parry (2005). WHO combats counterfeit malaria drugs in Asia. Iliwekwa mnamo 2008-07-19.
  91. WHO 2005 World Malaria Report 2008
  92. 92.0 92.1 Greenwood BM, Bojang K, Whitty CJ, Targett GA (2005). "Malaria". Lancet 365 (9469): 1487–1498. PMID 15850634. doi:10.1016/S0140-6736(05)66420-3. 
  93. Hay S, Guerra C, Tatem A, Noor A, Snow R (2004). "The global distribution and population at risk of malaria: past, present, and future". Lancet Infect Dis 4 (6): 327–36. PMID 15172341. doi:10.1016/S1473-3099(04)01043-6. 
  94. 94.0 94.1 Breman J (1 Januari 2001). "The ears of the hippopotamus: manifestations, determinants, and estimates of the malaria burden". Am J Trop Med Hyg 64 (1-2 Suppl): 1–11. PMID 11425172. Archived from the original on 2010-07-08. Retrieved 2009-11-19.  Unknown parameter |day= ignored (help); Check date values in: |date= (help)
  95. Korenromp E, Williams B, de Vlas S, Gouws E, Gilks C, Ghys P, Nahlen B (2005). "Malaria attributable to the HIV-1 epidemic, sub-Saharan Africa". Emerg Infect Dis 11 (9): 1410–9. PMID 16229771. 
  96. Abu-Raddad L, Patnaik P, Kublin J (2006). "Dual infection with HIV and malaria fuels the spread of both diseases in sub-Saharan Africa". Science 314 (5805): 1603–6. PMID 17158329. doi:10.1126/science.1132338. 
  97. Layne SP. Principles of Infectious Disease Epidemiology / (PDF). EPI 220. UCLA Department of Epidemiology. Jalada kutoka ya awali juu ya 2006-02-20. Iliwekwa mnamo 2007-06-15.
  98. Greenwood B, Mutabingwa T (2002). "Malaria in 2002". Nature 415 (6872): 670–2. PMID 11832954. doi:10.1038/415670a. 
  99. Grover-Kopec E, Kawano M, Klaver R, Blumenthal B, Ceccato P, Connor S (2005). "An online operational rainfall-monitoring resource for epidemic malaria early warning systems in Africa". Malar J 4: 6. PMC 548290. PMID 15663795. doi:10.1186/1475-2875-4-6. 
  100. Van Benthem B, Vanwambeke S, Khantikul N, Burghoorn-Maas C, Panart K, Oskam L, Lambin E, Somboon P (1 Februari 2005). "Spatial patterns of and risk factors for seropositivity for dengue infection". Am J Trop Med Hyg 72 (2): 201–8. PMID 15741558.  Unknown parameter |day= ignored (help); Check date values in: |date= (help)
  101. Trung H, Van Bortel W, Sochantha T, Keokenchanh K, Quang N, Cong L, Coosemans M (2004). "Malaria transmission and major malaria vectors in different geographical areas of Southeast Asia". Trop Med Int Health 9 (2): e473. PMID 15040560. doi:10.1046/j.1365-3156.2003.01179.x. 
  102. Keiser J, Utzinger J, Caldas de Castro M, Smith T, Tanner M, Singer B (1 Agosti 2004). "Urbanization in sub-saharan Africa and implication for malaria control". Am J Trop Med Hyg 71 (2 Suppl): 118–27. PMID 15331827.  Unknown parameter |day= ignored (help); Check date values in: |date= (help)
  103. Hay SI, Snow RW (2006). "The Malaria Atlas Project: Developing Global Maps of Malaria Risk". PLoS Medicine 3 (12): e473. PMC 1762059. PMID 17147467. doi:10.1371/journal.pmed.0030473. 
  104. Joy D, Feng X, Mu J, et al. (2003). "Early origin and recent expansion of Plasmodium falciparum". Science 300 (5617): 318–21. PMID 12690197. doi:10.1126/science.1081449. 
  105. Escalante A, Freeland D, Collins W, Lal A (1998). "The evolution of primate malaria parasites based on the gene encoding cytochrome b from the linear mitochondrial genome". Proc Natl Acad Sci USA 95 (14): 8124–9. PMID 9653151. doi:10.1073/pnas.95.14.8124. 
  106. Cox F (2002). "History of human parasitology". Clin Microbiol Rev 15 (4): 595–612. PMC 126866. PMID 12364371. doi:10.1128/CMR.15.4.595-612.2002. 
  107. From Shakespeare to Defoe: Malaria in England in the Little Ice Age. Paul Reiter. Centers for Disease Control and Prevention, San Juan, Puerto Rico.
  108. Vector- and Rodent-Borne Diseases in Europe and North America. Norman G. Gratz. World Health Organisation, Geneva.
  109. Biography of Alphonse Laveran. The Nobel Foundation. Iliwekwa mnamo 2007-06-15. Nobel foundation. Ilitumika 25 Oktoba 2006
  110. Ettore Marchiafava. Iliwekwa mnamo 2007-06-15.
  111. Tan SY, Sung H (Mei 2008). "Carlos Juan Finlay (1833–1915): of mosquitoes and yellow fever" (PDF). Singapore Med J 49 (5): 370–1. PMID 18465043.  Check date values in: |date= (help)
  112. Chernin E (Novemba 1983). "Josiah Clark Nott, insects, and yellow fever". Bull N Y Acad Med 59 (9): 790–802. PMC 1911699. PMID 6140039.  Check date values in: |date= (help)
  113. Chernin E (Septemba 1977). "Patrick Manson (1844–1922) and the transmission of filariasis". Am. J. Trop. Med. Hyg. 26 (5 Pt 2 Suppl): 1065–70. PMID 20786.  Check date values in: |date= (help)[dead link]
  114. Biography of Ronald Ross. The Nobel Foundation. Iliwekwa mnamo 2007-06-15.
  115. Ross and the Discovery that Mosquitoes Transmit Malaria Parasites. CDC Malaria website. Iliwekwa mnamo 2007-06-15.
  116. Kaufman T, Rúveda E (2005). "The quest for quinine: those who won the battles and those who won the war". Angew Chem Int Ed Engl 44 (6): 854–85. PMID 15669029. doi:10.1002/anie.200400663. 
  117. Kyle R, Shampe M (1974). "Discoverers of quinine". JAMA 229 (4): e320. PMID 4600403. doi:10.1001/jama.229.4.462. 
  118. Raju T (2006). "Hot brains: manipulating body heat to save the brain". Pediatrics 117 (2): e320–1. PMID 16452338. doi:10.1542/peds.2005-1934. 
  119. Krotoski W, Collins W, Bray R, et al. (1982). "Demonstration of hypnozoites in sporozoite-transmitted Plasmodium vivax infection". Am J Trop Med Hyg 31 (6): 1291–3. PMID 6816080. 
  120. Meis J, Verhave J, Jap P, Sinden R, Meuwissen J (1983). "Malaria parasites--discovery of the early liver form". Nature 302 (5907): 424–6. PMID 6339945. doi:10.1038/302424a0. 
  121. Kwiatkowski DP (Agosti 2005). "How malaria has affected the human genome and what human genetics can teach us about malaria". Am J Hum Genet. 77 (2): 171–92. PMC 1224522. PMID 16001361. doi:10.1086/432519.  Check date values in: |date= (help)
  122. Http://www3.chu-rouen.fr/Internet/services/sante_voyages/pathologies/paludisme/monde/frequence/ Archived 19 Juni 2010 at the Wayback Machine. CHU Hôpitaux de Rouen. Fréquence et tillhörighet des cas de paludisme.
  123. Carter R, Mendis KN (2002). "Evolutionary and historical aspects of the burden of malaria". Clin. Microbiol. Rev. 15 (4): 564–94. PMID 12364370. doi:10.1128/CMR.15.4.564-594.2002. Archived from the original on 2009-01-16. Retrieved 2009-11-19. 
  124. Verra F, Luoni G, Calissano C, Troye-Blomberg M, Perlmann P, Perlmann H, Arcà B, Sirima B, Konaté A, Coluzzi M, Kwiatkowski D, Modiano D (2004). "IL4-589C/T polymorphism and IgE levels in severe malaria". Acta Trop. 90 (2): 205–9. PMID 15177147. doi:10.1016/j.actatropica.2003.11.014. 
  125. Humphreys, M (2001). Malaria: Poverty, Race, and Public Health in the United States. Johns Hopkins University Press. pp. 256. ISBN 0-8018-6637-5. 
  126. Sachs J, Malaney P (2002). "The economic and social burden of malaria". Nature 415 (6872): 680–5. PMID 11832956. doi:10.1038/415680a. 
  127. Roll Back Malaria WHO partnership. Economic costs of malaria. WHO. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-12-29. Iliwekwa mnamo 2009-09-18.

Viungo vya nje hariri