Wajita ni kabila la watu wa Tanzania wanaoishi hasa katika Mkoa wa Mara. Lugha yao ni Kijita.

Wajita wana muingiliano mkubwa na makabila kama Waha, Wahaya, Wanyankole, Wanyoro, Watoro, Wakerewe, Wahangaza, Wanyambo, Wazinza, Wakara, Wakabwa, Waruri, Wasweta, Wasimbiti, Wasubi, Wakwaya na kadhalika. Kulingana na historia yao wengi waweza kuitana wajomba. Bila kusahau Wajaluo ambao ni watani wao.

Wajita nao wana koo nyingi sana kama Abhajigabha, Abhegamba, Abhatata, Abhagaya, , Abhaanga, Abhalinga, Abhaila, Abhalaga, Abhatimba, Abhayango, Abhasyora, Abharungu, Abharamba, Abhakome, Abhagunda, Abhabhogo, Abhakima, Abhakumi na wengineo.

Wajita ni watu wachapakazi sana na wasiopenda dhihaka kwenye kazi, wenye msimamo sana na wenye kupenda utani na wapole, ila wakali sana wanapoonewa.

Tena Wajita wanapenda elimu na ndiyo maana tokea wamisionari walipofika eneo la Rusoli walijenga shule kisha kudahili wanafunzi wa kutosha.

Pia Wajita ni watu wenye ubunifu na uthubutu wa kufanya mambo yenye tija. Ni waasisi wa mabadiliko kifikra.

Historia ya Wajita hariri

Inasemekana makabila mengi ya mkoani Mara si Bantu asilia lakini walipofika huko wengine walichagua kuzungumza lugha ya Kijita inayojulikana kama Kisuguti na lugha nyingine za Mara, kwa mfano Eastearn Nyanza kuzungumzwa na Wakuria.

Inawezekana baadhi ya Wajita kuwa na asili toka Rwanda, Burundi, Uganda, Sudan kama Wanubi, Sudan Kusini na labda pia Niger na Nigeria. Mfano Wajita wengine wana asili ya Kinilo-Sahara kutoka kusini mwa Sudan. Jina Magoti ni kubwa sana katika watu wa jamii ya kabila la Wadinka. Mfano mwingine ni Maiga, jina kubwa sana toka zamani katika milki ya Songhai uko Niger. Kwa ufupi kabila hili limebeba mchanganyiko wa watu wenye asili mbalimbali.

Inasemekana pia jina la mkoa wa Mara linatokana na neno Jabar Mara, mlima mkubwa ulioko Darfur, si mbali na Kordofan ambayo ni magharibi mwa Sudan, kwenye jamii ya Wafur na nyinginezo zinazopatikana katika mlima Mara.

Kati ya vijiji vingi vya Wajita utavikuta pia Rwanda, Uganda, Burundi. Kati ya vijiji hivyo mfano ni Rusori, Buringa na vinginevyo vingi tu.

Wajita wengi nao wana koo zao ambao hata wakienda Rwanda, Uganda, Niger, Burundi ni rahisi kutambua koo zao kulingana na miiko yao. Kama jamii zingine zozote zilizoweza tambua ndugu zao kutokana na miiko, mfano ya nyama ama vyakula vingine. Mfano: Wajita wa koo za Rusori wengi kuna samaki hawali, ila kulingana na mazingira ya siku hizi watu kutoelewa wanajikuta wakila samaki. Mila hizo pia ziko kwa Wanyoro wengi, Watoro na Wanyambo. Wajita wengine hawawezi kuua chatu na ni mwiko kabisa kama vile kwa Wahausa, Waigbo, na pia wengine wanaheshimu sana chura kama ilivyo kwa koo nyingine nchini Rwanda.

Wajita wenye asili ya Kibantu ni wengi sana na wanatokea katika koo za Bahitira. Mfano Waruri wengi ni Wabantu na wanatokea Bururi na ni kabila ambalo pia liko Uganda.

Pia wapo ambao wana asili ya Kush. Mfano: inaaminika Wajita wa kwanza kufika Musoma na wanaojiita Original ni wale wenye asili ya Warusori; mpaka sasa wao ni weupe na warefu sana, wapo na pua zao za kuchongoka. Yasemekana hao si Wabantu, wana asili ya Kinubi na Ethiopia na wengine pia wanatokea Bunyoro na wengine wakaenda Rwanda na Burundi.

Wajita wengi wenye asili ya Banyoro ni warefu sana, ingawa wengine ni weusi siku hizi kutokana na mchanganiko. Wenye asili ya Nubia na hao Banyoro zamani walikuwa kama Waarabu kwa mbali, ambao wengi wasemekana ni hao Warusori.

Pia Wapo ambao wametokea Ethiopia na Sudani, wana asili ya Kushi na wana mwingiliano wa karibu na Watsi, ni Watimba. Watimba ndio ukoo mkubwa katika kabila la Wajita, ambao asili yao walitokea Hemit, Ethiopia.

Wajita pia walikuwa na utawala wao, ambapo watemi wao walikuwa wa ukoo wa Bhatimba,ambao ni Kusaga, Majinge na wengineo. Walitawala kuanzia eneo la Suguti hadi kurudi Busekera, ma makao yao yalikuwa Majita, kijiji cha Bwasi.

Dini hariri

Wajita wengi ni washika dini. Kati ya madhehebu ambayo yameenea sana kati ya Wajita ni Wasabato. Hao walifika Ujita muda mrefu kueneza imani ya Kikristo pamoja na kujenga shule. Shule za Bwasi, Kasoma, Rusoli zimejengwa na wamisionari wa Kisabato na zilisaidia sana kuwafanya Wajita wengi kwenda shule.

Mila na utamaduni hariri

Wajita ni kabila linalofuata mfumo dume (patriarchy) hivyo watoto hupata urithi wao upande wa baba na ujulikana kwa jina la baba, watoto wa kiume hupewa kipaumbele kuliko wa kike. Tofauti na Wakurya, Wajita hawana utamaduni wa kukeketa watoto wa kike, ila toka zamani ni jadi yao kufanya tohara kwa watoto wa kiume.

Watu maarufu kutoka kabila la Wajita hariri

  1. Chinuno Magoti, PhD, daktari wa binadamu
  2. Wilson Mkama, aliwahi kuwa Katibu Mkuu wa CCM
  3. Bitta John Musiba, aliwahi kuwa mchezaji wa Simba Sports Club na Taifa Stars
  4. Isaac Muyenjwa Gamba, mtangazaji wa DW, Bonn, Ujerumani
  5. Kangi Alphaxard Lugola, aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi
  6. Munasa Sabi Munasa, kada wa CCM
  7. Sospeter Gomborojo Massambu, mwanasiasa
  8. Aristablus Musiba, mwandishi wa riwaya
  9. Charles Majinge Kusaga, mkurugenzi wa hospitali ya Bugando, mwenyekiti wa bodi ya wadhamini hospitali ya Muhimbili
  10. Joseph Kusaga, mkurugenzi na mmliki wa Clouds Media
  11. Dan Petro Mapigano, jaji mstaafu wa mahakama kuu
  12. John Nyaindi, Mkuu wa Utumishi na Mafunzo, NBC Bank
  13. Riziki S. Majinge, mwandishi wa vitabu vya sheria Ulaya, pia mwanaharakati
  14. Bellen Manyama, Mchumi Mwandamizi, UNDP Tanzania
  15. Masau Bwire, Msemaji wa klabu Ruvu Shooting
  16. Sadock Magai Nyakai, wakili
  17. Alphaxad Gomborojo Massambu, mtaalamu wa masuala ya uwekezaji
  18. Ezekiel Gomborojo Massambu, rubani wa ndege
  19. Nyamburi Mashauri, mpambe wa Rais Samia Suluhu Hassan
  20. Joseph Kingo Chikaka, mwandishi wa vitabu
  21. Sixtus Sabilo, mchezaji wa Namungo F.C.
  Makala hii kuhusu utamaduni wa Tanzania bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Wajita kama historia yake au mahusiano yake na mada nyingine?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.