Kairo

mji mkuu wa Misri
(Elekezwa kutoka Cairo)







Kairo (kwa Kiarabu القاهرة al-Qāhira – „mwenye ushindi“) ni mji mkuu wa Misri na mji mkubwa wa nchi zote za Kiarabu, pia moja kati ya majiji makubwa duniani.

Kairo

Bendera
Majiranukta: 30°03′N 31°22′E / 30.050°N 31.367°E / 30.050; 31.367
Nchi Misri
Mkoa Kairo
Tovuti:  www.cairo.gov.eg
Kairo jinsi inavyoonekana kutoka angani - njano ni rangi ya jangwa, kijani-nyeusi ni rangi ya mashamba kwenye bonde la Nile linalopanuka kuwa delta na rangi ya kijivu ni nyumba za Kairo

Kairo yenyewe inakadiriwa kuwa na wakazi 10,230,350 [1], kanda ya jiji pamoja na mitaa ya nje na mapembizo ni 15,628,325 [2].

Jiografia hariri

 
Sehemu ya kusini ya kisiwa cha Gezira kilichopo ndani ya mto Nile, Opera ya Kairo (jengo jeupe) na nyuma kitovu cha mji pamoja na meidani ya Tahrir ng'ambo ya mto.
 
Mto Nile unapita mjini Kairo.
 
Kisiwa cha Gezira katikati ya jiji.

Kairo iko kwenye sehemu ya kaskazini ya Misri, takriban kilomita 160 kusini kwa pwani ya bahari ya Mediteranea. Mji ulikua kando ya mto Nile, mahali ambako unatoka katika bonde unamovuka jangwa na kujigawa kuwa na delta pana hadi baharini.

Jinsi ilivyo kwenye majiji mengi makubwa, wenyeji hutofautisha kati ya mji asilia wenyewe na jiji kubwa kwa jumla. Mji wa Kairo wenyewe una eneo la km2 453 tu, uko upande wa mashariki wa mto pamoja na visiwa viwili ndani ya mto; jiji pamoja na vitongoji limepanuka pande zote mbili kuelekea ndani ya jangwa.[3][4]

Katika karne ya 19 mto Nile ulibanwa na handaki na mifereji. Hadi wakati ule mifuriko na mabadiliko kwenye mwendo wake walitokea mara kwa mara. Historia hii ya mabadilko ya mwendo wa mto ni sababu ya kwamba mitaa mipya ya mji iko karibu na mto wenyewe mahali ambako zamani wangeogopa kujenga, ni mitaa ya Garden City, Kairo mjini na Zamalek.[5]

Kusini mwa Kairo ya leo kuna Kairo ya Kale penye mabaki ya miji iliyotangulia hapa kama vile Babyloni ya Misri (enzi ya Bizanti, kabla ya uvamizi wa Waarabu Waislamu) na Fustat (mji mkuu wa kwanza wa Kiislamu nchini Misri).

Sehemu za Bulaq ziko leo upande wa kaskazini ya mji wenyewe zilianzishwa kama eneo la bandari ya mtoni mnamo karne ya 16. Boma la Kairo (ar. qale salah ad din) inaonyesha mahali ambako mji wa Kairo ulianzishwa na Wafatimi. Upande wa magharibi wa mji wa Kairo uliathiriwa na mpangilio wa jiji wa kimagharibi ukiwa na barabara pana, nyanja mbalimbali na nyumba za kisasa. Upande wa mashariki una zaidi mitaa midogomidogo, nyumba za kienyeji na kujaa watu wengi mno.

Tabianchi ya Kairo hariri

Kairo iko katika kanda yenye tabianchi ya nusutropiki. Tabianchi kwa jumla ni yabisi. Hata hivyo wakati mwingine hewa yenye unyevu inaweza kufika kwa sababu bahari iko karibu. Halijoto ya wastani mwakani ni sentigredi 21.7. Kiwango cha mvua ni milimita 24,7 pekee. Mwezi wenye joto zaidi ni Julai mwenye wastani wa sentigredi 28, na mwezi baridi ni Januari yenye wastani wa sentigredi 13,9.

Usimbishaji ni mdogo; wastani wa mwaka ni milimita 24,7 pekee unaotiririka katika miezi wa Novemba hadi Machi pekee.

Wakati wa Disemba 2013 Kairo iliona theluji mara ya kwanza baada ya miaka mingi sana[6].

Kanda ya Jiji hariri

Kanda ya Jiji inajumlisha Kairo pamoja na miji jirani, vitongoji na mapembizo. Idadi ya wakazi kwa jumla iko kati ya milioni 15 hadi 16. Kiutawala kanda ya jiji inajumlisha mkoa wa Kairo na sehemu ya mikoa miwili yaani Giza na Qalyubia.

Miji ya pekee muhimu zaidi katika kanda hii ni

Kuna mipango ya kujenga jiji jipya upande wa mashariki wa Kairo litakalokuwa mji mkuu mpya wa Misri.[7]

Usafiri hariri

 
Metro ya Kairo
 
Barabara Kuu mjini
 
Mabasi ya manispaa
 
Kituo cha Metro Ramses

Usafiri ndani ya Kairo na kanda ya jiji huenda kwa kutumia barabara, njia za reli, reli ya chini ya ardhi inayoitwa "metro" na feri kwenye mto. Kuna magari mengi ya binafsi, teksi na mabasi ambayo ni ya umma au ya binafsi. Njia nyingi za mabasi na reli ya metro zinakutana kwenye Midan Ramses [8] Usafiri ndani ya Kairo ni mashuhuri kwa ugumu wake kutokana na wingi wa watu na magari.[9]

 
Ramani ya Metro ya Kairo

Metro ya Kairo ("مترو") ni jina la reli ya chini ya ardhi. Ni usafiri wa haraka pale njia zake zinapofika. Mabehewa yake yanaweza kujaa mno wakati wa saa za kwenda kazini na kurudi. Kila treni ya metro huwa na magari wawili yaliyotengwa kwa ajili ya wanawake pekee, ni gari la nne na la tano, lakini hata hivyo wakinamama wako huru kupanda kila behewa wanapotaka. Metro hii ina njia tatu zenye urefu wa kilomita 77.9 na kuna vituo 61 zinazohudumiwa[10].

Kuna tramu katika sehemu za (Heliopolis na mji wa Nasr) lakini ile katika Kairo mjini ilifungwa miaka mingi iliyopita.

Kuna mtandao mkubwa wa barabara kati ya Kairo mjii, sehemu nyngine za kanda ya jiji na miji ya nje. Kuna barabara ya duara inayopita nje ya jiji. Madaraja mengi yanalenga kurahisisha mwendo ndani ya jiji ingawa kwenye saa za msongamano watu hukaa sana kwenye foleni za magari.

Dini hariri

Zamani Kairo ilikuwa mji wenye wakazi wengi wa tamaduni na dini mbalimbali; hadi leo nyumba zao za ibada ni kama kumbukubu ya historia hiyo. Maelfu ya Wagiriki wa Misri waliondoka nchini baada ya mapinduzi ya mwaka 1952. Wayahudi pia walianza kuona ubaguzi mkali na madhulumu tangu vita ya Israeli na Waarabu wa 1948 wakaondoka. Leo hii kuna Wayahudi chini ya 100 waliobaki Misri baada ya historia ya miaka 2,500.

Siku hizi wakazi walio wengi ni Waislamu Wasunni (takriban 90%). Wengine ni hasa Wakristo Wakopti.

Upande wa Uislamu kuna misikiti mingi na idadi yake inaendelea kuongezeka. Chuo Kikuu cha Al-Azhar kinapatikana mjini tangu mwaka 969: ni taasisi ambayo utalaamu wake unaheshimiwa na kuangaliwa kati wa Wasunni wengi duniani.

Upande wa Wakopti kiongozi wao Papa Pope Tawadros II anakaa Kairo. Kanisa la Mtakatifu Marko mjini Kairo ni kanisa kubwa la pili kwenye bara la Afrika.

Masingagogi ya Kiyahudi yanaweza kutembelewa na watalii lakini hakuna tena ibada ya kawaida kutokana na idadi ndogo ya Wayahudi waliobaki.

Vurugu za kisiasa za miaka iliyopita ilileta pia magongano kati ya wafuasi wa dini, hasa kati ya Waislamu wenye itikadi kali na Wakristo. [11]

Tazama pia hariri

Mji mingine mikubwa ya Afrika hariri

Marejeo hariri

  1. Walikuwa 7,902,085 mwaka 2011 wakati wa sensa, taz. Al-Qāhirah (Governorate) 2011
  2. Wakazi wa Kairo Kubwa walihesabiwa katika sensa ya 2011 kuwa 15,628,325.
  3. Cairo Maps. Cairo Governorate. Jalada kutoka ya awali juu ya 2009-04-19. Iliwekwa mnamo 10 September 2009.
  4. Brinkhoff, Thomas. Egypt: Governorates & Cities. City Population. Iliwekwa mnamo 12 September 2009.
  5. Amanda Briney (20 February 2011). Ten Facts about Cairo, Egypt. Geography of Cairo. About.com. Jalada kutoka ya awali juu ya 2012-03-28. Iliwekwa mnamo 14 July 2012.
  6. Samenow, Jason (13 December 2013). "Biblical snowstorm: Rare flakes in Cairo, Jerusalem paralyzed by over a foot". The Washington Post.
  7. "Egypt unveils plans to build new capital east of Cairo". BBC News. 13 March 2015. Retrieved 14 March 2015.
  8. Travel Cairo. MobileReference. 2007. ISBN 978-1-60501-055-7. Archived from the original on 2016-03-02. Retrieved 2016-05-06. 
  9. Al-Ahram Weekly | Features | Reaching an impasse. Weekly.ahram.org.eg (1 February 2006). Jalada kutoka ya awali juu ya 18 May 2009. Iliwekwa mnamo 5 May 2009.
  10. Tovuti rasmi. Jalada kutoka ya awali juu ya 2018-09-23. Iliwekwa mnamo 2016-05-06.
  11. Égypte : 24 coptes tués par les forces de l'ordre au Caire – Le Point. Lepoint.fr. Iliwekwa mnamo 12 March 2013.

Viungo vya nje hariri

 
WikiMedia Commons
Wikimedia Commons ina media kuhusu:
  Makala hii kuhusu maeneo ya Afrika bado ni mbegu.
Je unajua kitu kuhusu Kairo kama historia yake, biashara, taasisi zilizopo, watu au utamaduni?
Labda unaona habari katika wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.