Karama (kutoka neno la Kiarabu الكرامة) ni zawadi yoyote inayotokana na ukarimu wa Mungu kwa viumbe wake.

Mapokeo ya Kiislamu hariri

Karama inatazamwa kuwa kipaji cha pekee kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Katika surat 19 (Al Maryam) Mariamu analishwa kwa neema ya Allah: hii inatazamwa pia kama karama.

Karama inaweza kupatikana kama tabia au uwezo wa pekee, kama mtu mwenye kufanya miujiza kwa idhini ya Mungu. Mwenye kutoa karama ni Allah. Kwa sababu hiyo yeye anasifika kama Karimu. Katika Uislamu hilo ni mojawapo kati ya majina 99 ya kumsifia.

Katika Ukristo hariri

Katika Biblia karama kwa kawaida ni tafsiri ya neno la Kigiriki χάρισμα ("kharisma" kutokana na χάρις, "kháris" neema). Neno hilo limekuwa likitumika sana katika Kanisa kuanzia Pentekoste na katika barua za Mtume Paulo, kwa msisitizo kuwa karama zote zinamtegemea Roho Mtakatifu.

Karama si zile za kushangaza tu, tena zile muhimu zaidi si hizo, bali zile zinazojenga zaidi Kanisa, kama zile za uongozi: “Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za kuponya wagonjwa, na masaidiano, na maongozi, na aina za lugha” (1Kor 12:28). “Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbalimbali, kwa kadiri ya neema tuliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha, katika kufundisha kwake; mwenye kuonya, katika kuonya kwake; mwenye kukirimu, kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia, kwa bidii; mwenye kurehemu, kwa furaha” (Rom 12:6-8).

Karama nyingine muhimu zinawezesha kuishi kwa useja kama Yesu na Paulo, au kwa ndoa: “Nipendalo ni kwamba watu wote wawe kama mimi nilivyo; walakini kila mtu ana karama yake mwenyewe itokayo kwa Mungu, huyu hivi, na huyu hivi. Lakini nawaambia wale wasiooa bado, na wajane; ni heri wakae kama mimi nilivyo” (1Kor 7:7-8). “Si wote wawezao kulipokea neno hili, ila wale waliojaliwa” (Math 19:11). Tunavyoona katika historia ya watawa, mara nyingi karama ya useja inaendana na nyingine katika maisha ya sala, ya kijumuia na ya kitume. Hivyo Filipo “alikuwa na binti wanne, mabikira, waliokuwa wakitabiri” (Mdo 21:9).

Karama zinagawiwa na Roho Mtakatifu jinsi anavyotaka, si kwa sifa au faida ya binafsi, bali kwa ustawi wa taifa la Mungu. “Kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye... Je, wote ni mitume? Wote ni manabii? Wote ni waalimu? Wote wanatenda miujiza? Wote wana karama za kuponya wagonjwa? Wote wanena kwa lugha? Wote wafasiri?... Kwa kuwa mnatamani sana kuwa watu wenye karama za roho, takeni kwamba mzidi sana kuwa nazo ili kulijenga kanisa... Kwa maana Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani” (1Kor 12:11,29-30; 14:12,33). Kwa ajili hiyo mitume wa Yesu walipambanua na kuratibu karama katika ibada na katika maisha ya jumuia zisije zikavuruga Kanisa.

Karama za kushangaza zina hatari mbalimbali, hasa zikitiwa maanani mno. Hapo ni rahisi zilete majivuno, kijicho na mafarakano. “Ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je, si watu wa tabia ya mwili ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?... Mmekwisha kushiba, mmekwisha kupata utajiri, mmemiliki pasipo sisi. Naam, laiti mngemiliki... Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke” (1Kor 3:3; 4:8; 10:12). Katika mambo yasiyothibitika ni rahisi kudanganyika kuwa yametoka kwa Mungu, kumbe sivyo. Kisha kudanganyika ni vigumu kuachana nayo hata yakiwa na madhara kwa mhusika au kwa Kanisa. “Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani” (1Yoh 4:1).

“Pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule… Kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimwagia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye” (1Kor 12:4-11; taz. Rom 12:6-8). Mtume aliendelea kwa kuweka upendo juu kuliko karama hizo zote, “Takeni sana karama zilizo kuu. Hata hivyo nawaonyesha njia iliyo bora. Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi” (1Kor 12:31-13:2) kwa sababu hapo utashi wangu unaelekea kinyume cha matakwa ya Mungu.

Umbile na mgawanyo wa karama hizo kadiri ya Kanisa Katoliki hariri

Neema inayotia utakatifu na upendo vinatuunganisha na Mungu, lengo letu kuu; kwa hiyo ni bora kuliko karama, zilizo fadhili za pekee ambazo zinalenga hasa faida ya jirani, tena zinamuandaa tu kuongoka, bila kumshirikisha uzima wa Mungu. Karama ni ishara tu zinazothibitisha ama ufunuo wa Mungu uliotolewa kwa wote, ama utakatifu wa mtumishi wake.

Neema inayotia utakatifu inapita maumbile kwa namna tofauti na karama. Neema inayotia utakatifu inapita maumbile kwa sababu ni kushiriki uzima wa ndani wa Mungu; kwa hiyo haionekani wala haijulikani na maumbile. Kumbe hizo ishara zinazojulikana na maumbile haziyapiti kwa mfumo wake zenyewe, isipokuwa kwa namna zilivyotokea. Hivyo ufufuo wa maiti unamrudishia kwa njia ipitayo maumbile uhai wa kimwili bila kusababisha ndani yake uzima wa Mungu. Hivyo katika ishara hizo kinachopita maumbile ni cha nje na kidogo kuliko neema inayotolewa na ubatizo.

Kwa kawaida fadhili za pekee, ambazo pengine zinaendana na sala ya kumiminiwa, zinapangwa pamoja na karama hizo. Yohane wa Msalaba akianzia misimamo ya teolojia alitofautisha vizuri kuzama katika mafumbo kwa jumla katika giza na namna mbalimbali za ujuzi maalumu (mafunuo, njozi na maneno ya ndani): “Kuhusu ujuzi wa jumla katika giza hakuna mgawanyiko, ni kuzama katika mafumbo kwa imani: ndio lengo ambapo tuifikishe roho; ujuzi mwingine wowote unatakiwa kulichangia kuanzia wa awali, nayo roho inatakiwa kusonga mbele daima kwa kuachana na kila mmojawapo”.

Tutaeleza kwanza mafunuo, halafu tutaona namna maalumu ambazo yanapatikana. Tena kati ya fadhili hizo tutaeleza kwanza zile za nje zaidi, ambazo zinalenga hasa faida ya jirani na kuhusiana na karama. Halafu tutazingatia zile zinazolenga zaidi utakatifu wa mtu anayezipokea. Tukianzia mambo ya jumla kwenda yale maalumu, na kutoka yale ya nje kwenda yale ya ndani tutakwepa kujirudiarudia na tutaelewa zaidi kazi ya Mungu.

Mafunuo ya Kimungu hariri

Mafunuo ya Kimungu yanadhihirisha kwa namna ipitayo maumbile ukweli fulani uliofichika, yakitegemea karama ya unabii. Yenyewe ni ya hadhara ikiwa yalitolewa na manabii wa Agano la Kale, na Kristo na mitume wake na yanapendekezwa kwa wote na Kanisa ambalo linatunza hazina hiyo katika Maandiko na katika Mapokeo. Kumbe ni ya binafsi yakilenga faida ya watu kadhaa tu. Mafunuo ya binafsi, hata yale muhimu, hayadai tuyashike kwa imani ya Kikatoliki, ila baadhi yake yanaweza yakavuta watu wazingatie ibada fulani ambayo kwa umbile lake inawahusu waamini wote (k.mf. ibada kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu) na Kanisa likishachunguza hoja za kutetea ibada hiyo linaweza likaihamasisha na kuiweka rasmi bila kudai imani kwamba ufunuo wa binafsi ulioisababisha umetoka kwa Mungu.

Kwa hakika wale waliojaliwa mafunuo ya Kimungu yaliyopimwa na kutambuliwa na wenye mamlaka wanatakiwa kuinamia kwa heshima tokeo hilo la Mungu. Kanisa linapokubali mafunuo ya binafsi linataka kutamka tu kwamba hayapingani na imani na hivyo yanaweza kupendekezwa kwa waamini wayapokee kwa msingi fulani. Lakini hata katika yale yaliyokubaliwa hivyo unaweza ukajitokeza udanganyifu fulani kwa sababu watakatifu wenyewe wanaweza wakadhani kitu kilichotokea ndani mwao kimesababishwa na Roho Mtakatifu, kumbe sivyo, au wanaweza wakatafsiri vibaya ufunuo wa Kimungu, kama lilivyoeleweka vibaya neno la Yesu kuhusu urefu wa maisha ya Mtume Yohane. Uwezekano wa kudanganyika unatokana na kwamba karama ya unabii ina ngazi nyingi, kuanzia hisi tu hadi ufunuo kamili. Kama ni hisi ya kinabii tu, maana sahihi na vilevile asili ya Kimungu ya mafunuo vinaweza vikabaki vimefichika au havieleweki; ndivyo Kayafa alivyotabiri bila kujitambua akisema, “Yafaa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu, wala lisiangamie taifa zima” (Yoh 11:50).

Mtu aliyeangazwa kweli na Mungu kabla hajapanga la kufanya kufuatana na ufunuo huo aombe shauri la kiongozi wake au la mtu mwingine mwenye elimu na busara ambaye achunguze jambo lenyewe upande wa imani, wa teolojia na wa busara, hasa kwa sababu ni rahisi kudanganyika katika kutafsiri mafunuo. Dalili mojawapo ya asili ya Kimungu ya ufunuo fulani ni unyenyekevu na usahili ambao aliyefadhiliwa anaupokea na kumshirikisha kiongozi wake kwa maneno machache, asishikamane nao zaidi na akimtii kikamilifu wakili wa Kristo. Lakini kwa nadra karama ya unabii inapatikana hata katika watu wasio na sifa hizo.

Kuhusu hamu ya kupata mafunuo, Yohane wa Msalaba, ambaye mara nyingi alialika wanasala watamani kwa unyenyekevu lakini pia kwa tumaini na ari kuzama katika mafumbo ya imani ili kuungana na Mungu, alilaumu kwa nguvu hamu hiyo. Alionyesha kwamba anayetamani mafunuo anampa shetani nafasi ya kumdanganya kwa udadisi huo na kwamba elekeo hilo linachafua usafi wa imani, linalemea roho, linaonyesha utovu wa unyenyekevu, linaingiza katika hatari nyingi, tena ni kumkosea heshima Yesu aliyetupatia ukamilifu wa ufunuo katika Injili. Pengine Mungu anawajalia fadhili hizo walio dhaifu bado, au wenye nguvu wanaotakiwa kutimiza utume wa pekee kati ya matatizo makubwa; lakini kuzitaka ni dhambi walau nyepesi, hata kama lengo ni jema. Zinasaidia tu zikisababisha unyenyekevu na upendo wa Mungu. Hivyo linaeleweka kosa la viongozi wasio na busara wanaowadodosa waliojaliwa njozi na mafunuo. Upotovu huo unasababisha udanganyifu, unaondoa utulivu na kusogeza mbali na unyenyekevu kutokana na kufurahia bure njia za pekee.

Hatimaye alisisitiza kwamba hamu ya mafunuo inasogeza mbali na sala ya kumiminiwa, “Inadhaniwa kwamba limetokea jambo kubwa, kwamba Mungu mwenyewe amesema: kumbe ni kitu kidogo au hakuna kitu au hata chini ya hapo. Kwa kuwa kinaweza kusaidia nini kinachokosa unyenyekevu, upendo, ufishaji, usahili mtakatifu, kimya n.k.? Kwa hiyo natamka kwamba aina hizo za udanganyifu zinazuia sana muungano na Mungu, kwa sababu mtu akizizingatia, jambo hilo tu linatosha kumsogeza mbali sana na kilindi cha imani… Roho Mtakatifu anaangaza akili iliyojikusanya kadiri ilivyojikusanya, na kujikusanya kikamilifu kunafanyika kwa imani… Upendo wa kumiminiwa unawiana na usafi wa roho katika imani kamili: kadiri upendo huo ulivyo na nguvu, Roho Mtakatifu anaiangaza na kuishirikisha zawadi zake”.

Lakini tutofautishe aina mbili za mafunuo ya binafsi: 1) Mafunuo hasa, yanayotufunulia siri fulani kuhusu Mungu au kazi yake, yanaweza yakaendana na udanganyifu kwa urahisi mkubwa zaidi. Bila shaka yeye anaweza akawafunulia watu muda uliowabakia kuishi, majaribu yatakayowapata, na mambo yatakayotokea kwa taifa au mtu fulani. Lakini shetani anaweza kuyaghushi kwa urahisi, tena kwa kuthibitisha uongo wake anatanguliza habari ambazo zinawezekana au ni nusu kweli. “Kwa jinsi yule Mwovu anavyoweza kujitwalia sura ya ukweli na kuithibitisha, karibu haiwezekani kukwepa ujanja wake tusipokataa mara” (Yohane wa Msalaba).

2) Mafunuo upande, yanayotufanya tuelewe zaidi kweli zipitazo maumbile zilizokwishajulikana kwa imani, yanafanana na hali ya kuzama katika mafumbo, hasa yasipoishia jambo maalumu, bali yanamhusu Mungu mwenyewe na kuchimba kwa dhati hekima, wema au uweza wake usio na mipaka. “Aina hizo za ujuzi wa juu unaotegemea upendo zinapatikana tu na mtu katika hali ya muungano na Mungu; zenyewe ndio muungano huo kwa kuwa zinatokana na fungamano maalumu la roho na umungu. Ni Mungu mwenyewe ambaye anahisiwa na kuonjwa. Bila shaka Mungu hahisiwi bayana na wazi kabisa kama katika utukufu, ila fungamano hilo ni hai na bora kwa ujuzi na mvuto hivi kwamba linapenya undani wa roho. Shetani hawezi kujiingiza humo na kudanganya kwa kughushi; hakuna cha kufanana nalo, hakuna cha kukaribia raha na nderemo za namna hiyo. Hizo zina ladha ya umungu na ya uzima wa milele, naye shetani hawezi kughushi mambo ya juu hivyo. Kuhusu hisi nyingine tulisema mtu aachane nazo, lakini wajibu huo unakoma mbele ya hizo zilizo matokeo ya muungano ambao tunajitahidi kufikishia roho. Yale yote tuliyowahi kuyafundisha kuhusu kujinyima na kujibandua kabisa yanalenga muungano huo, na fadhili za Kimungu zinazotokana nao ni matunda ya unyenyekevu, ya hamu ya kuteseka kwa upendo wa Mungu, kwa uvumilivu na bila kutarajia tuzo” (Yohane wa Msalaba).

Aina mbalimbali za njozi zipitazo maumbile hariri

Mafunuo ya Kimungu yanatokea kwa namna ya njozi au ya maneno. Njozi zinaweza kupitia hisi, ubunifu au akili. Njozi za kihisi au za kimwili za Mwokozi, za Bikira Maria na za watakatifu zinaweza zikatolewa kwa wanaoanza ili kuwabandua na malimwengu. Zikichangwa na idadi kubwa ya watu, ni dalili ya kwamba ni za nje, lakini si hakika ya kwamba zimetoka kwa Mungu. Zikiwa za mtu binafsi, ni lazima kuchunguza kwa uangalifu hali ya ndani ya mtu anayejishuhudia kuwa nazo, halafu kuendelea kwa busara kubwa. Kiongozi ataweza kutambua kama hizo ni fadhili za Mungu kwa kuzingatia zinavyolingana na mafundisho ya Kanisa na zinavyozaa matunda rohoni mwa mhusika. Huyo atapaswa kuonyesha uaminifu katika kuchuma utakatifu uliokusudiwa na Mungu akitoa fadhili hizo.

Njozi zinazohusisha ubunifu zinasababishwa na Mungu au malaika katika kipawa hicho mtu akiwa ama macho ama usingizini. Mara kadhaa Yosefu alielekezwa na Mungu katika ndoto. Ingawa ni vigumu kutambua asili ya Kimungu ya ndoto, kwa kawaida tukimtafuta kwa bidii anajua kujitambulisha kwetu ama kwa hisi ya amani ya dhati ama kwa matukio yanayothibitisha ndoto. Hivyo mkosefu anaweza akaonywa katika ndoto kuhusu haja ya kuwahi kuongoka. Njozi hizo zinaweza zikapatwa na udanganyifu wa ubunifu na wa shetani. Zile zinazotoka kwa Mungu zinatambulishwa na dalili tatu: 1) tusipoweza kuzisababisha wala kuziondoa tunavyotaka, bali zinatokea ghafla na kudumu muda mfupi; 2) zikiacha rohoni amani kubwa; 3) zikizaa matunda ya uadilifu, unyenyekevu na udumifu katika kutenda mema. Njozi ya namna hiyo ikitolewa mtu akiwa macho, karibu kila mara inaendana na hali ya kutoka nje ya nafsi walau kiasi.

Njozi zinayohusisha akili zinaionyesha kwa hakika jambo fulani pasipo kutumia kwa wakati huo vitu vinavyofikiwa na hisi. Pengine njozi hizo zina giza na si wazi, pengine ni angavu na wazi. Zikitoka kwa Mungu zinatambulishwa na matokeo yake: amani ya ndani, furaha takatifu, unyenyekevu wa dhati, ambatano la moja kwa moja na maadili. Hata njozi bora zaidi, kwa sababu ni za chini kuliko heri ya mbinguni, haziweki kuufikia umungu ulivyo, ila kwa namna fulani ya kuona kupitia mawazo ya kumiminiwa.

Aina mbalimbali za maneno yapitayo maumbile hariri

Maneno yapitayo maumbile ni matokeo ya wazo la Mungu yanayosikika ama katika hisi za mwili, ama katika hisi za nafsi, ama katika akili moja kwa moja.

Maneno yapitayo maumbile yanayosikika masikioni ni mawimbi yanayoundwa na malaika hewani. Maneno ya namna hiyo yanaweza kuwa madanganyifu sawa na njozi za kimwili, hivyo ni lazima tuyachambue kwa kanuni zilezile.

Maneno mengine yapitayo maumbile yanahusisha ubunifu wa mtu akiwa macho au usingizini. Yanaonekana yametoka pengine juu mbinguni, pengine ndani mwa moyo. Yanaeleweka kikamilifu ingawa hayasikiki kimwili. Hayasahauliki kwa urahisi na hasa yale yanayoleta utabiri fulani yanajichapa katika kumbukumbu. Tunayatofautisha na yale yanayotungwa na roho yetu kwa sababu hatuwezi kuyasikia tunavyotaka na kwa sababu ni maneno na matendo kwa wakati mmoja; k.mf. yakilaumu kasoro zetu, yanabadili papo hapo misimamo yetu ya ndani na kutuwezesha kukabili lolote kwa ajili ya utumishi wa Mungu: hapo ni rahisi kuyapambanua. Yakitokana na shetani, yanasababisha mabaya: mara nyingi ni rahisi kuyatambua mapema kwa sababu yanafanana na yale halisi kama kioo na almasi tu.

Maneno yanayohusisha akili yanasikika katika kipawa hicho moja kwa moja, bila kupitia hisi wala ubunifu, kama malaika wanavyoshirikishana mawazo na matakwa yao. “Ni usemi usio na maneno, ambao ndiyo lugha ya kwetu mbinguni” (Teresa wa Yesu).

Miguso ya Kimungu hariri

“Mara nyingi” sala ya kumiminiwa ya hali ya juu inaendana na aina nyingine ya fadhili, yaani “miguso ya Kimungu” ambayo inafanyika katika utashi na kuwa na “matokeo katika akili… inaipenyeza ndani ya Mungu kwa namna ya juu na tamu sana”. Haitegemei utendaji wa roho, wala tafakuri zake, ingawa kwa njia hiyo roho inajiandaa kuipokea. Pengine ni ya dhati na ya nguvu hivi kwamba inaonekana imefanyika “katika undani wenyewe wa roho”. Undani huo hauwezi kutenda, kusikia, kuhisi wala kupenda usipopitia vipawa vyake; ndiyo maana ulipewa vipawa hivyo. Katika hilo unatofautiana na Mungu ambaye peke yake katika usahili wake anatenda mwenyewe moja kwa moja asihitaji vipawa. Yeye, akiwa ndani ya roho kuliko roho yenyewe kwa sababu ndiye anayeidumisha, anaweza kugusa (Kiroho, si kimwili) na kusukuma toka humo undani wa vipawa hivyo hata roho itende matendo ya dhati isiyoweza kuyasababisha yenyewe. “Kukubali kwa unyenyekevu bila kutenda ndio msimamo unaompasa mtu; Mungu anajalia fadhili hizo kadiri ya matakwa yake, akipendelea watu wanyenyekevu waliojibandua na yote” (Yohane wa Msalaba).

Karama nyingine za pekee hariri

Kuelea hewani hariri

Ni tukio la mwili kuinuka juu mbali na ardhi bila sababu yoyote ya kueleweka, hivi kwamba unabaki hewani pasipo kutegemezwa na kitu chochote, ilivyokuwa ikimtukia Yosefu wa Copertino. Kinyume chake kuna matukio ya mwili kuwa na uzito mkubwa usio wa kawaida. Udanganyifu wa wenye matatizo ya nafsi haujawahi kusababisha mwili wao uelee hewani.

Papa Benedikto XIV alidai kwanza tukio liwe limethibitika, ili kukwepa ujanja wowote. Halafu alionyesha kwamba tukio hilo halielezeki kisayansi kwa sababu ya elekeo la mvutano, lakini halipiti uwezo wa kuinua miili walionao malaika na shetani; kwa hiyo ni lazima kulichunguza vizuri upande wa mwili, maadili na dini lisiwe limesababishwa na ibilisi; mambo yote yakilingana tunaweza na kupaswa kuliona limesababishwa na Mungu au na malaika kwa kuijalia miili ya watakatifu utangulizi fulani wa wepesi wa miili mitukufu.

Kuangaza hariri

Pengine waliozama katika mafumbo wanapata uangavu wa pekee: mwili wao unazungukwa na nuru, hasa usoni. Tukio hilo ni la kulichunguza sawa na lile la kuelea hewani, isipoelezeka kisayansi: kama linatokea mchana au usiku; kama nuru hiyo inapita mianga mingine yote; kama tukio linadumu muda mrefu na kujirudiarudia. Pia ni lazima kulizingatia kwa makini upande wa maadili na wa dini: kama linatukia wakati wa mahubiri, wa sala, wa kutoka nje ya nafsi; kama linasababisha matokeo ya neema, k.mf. uongofu wa kudumu; kama mhusika ni mwadilifu. Ikiwa masharti hayo yote yametimia na kuthibitika, tunaweza kuliona tukio hilo la pekee kama utangulizi fulani wa uangavu wa miili mitukufu.

Kunukia hariri

Pengine miili ya watakatifu inanukia wakiwa hai au kisha kufa. Daima waamini wameona hiyo ni ishara ya harufu nzuri ya maadili yao. Ili kuhakikisha tukio hilo linatoka kwa Mungu ni lazima tuchunguze kama harufu nzuri ni ya kudumu, kama karibu na mwili huo kuna kitu kinachoweza kuisababisha kimaumbile, na kama tukio hilo la pekee linasababisha neema fulani.

Kufunga chakula kwa muda mrefu hariri

Kuna watu, hasa kati ya wenye madonda matakatifu, walioishi miezi au miaka bila kula chochote isipokuwa ekaristi takatifu. Ni lazima tulichunguze kwanza tukio hilo kwa makini, kwa muda mrefu, pasipo nafasi katikati, kwa kutumia mashahidi wengi wenye uerevu wa kugundua udanganyifu na ujanja wowote. Ni lazima kuona kama mtu amefunga chakula chochote hata cha majimaji kwa muda mrefu na wakati huohuo anaendelea na shughuli zake. Hapo tukio halielezeki kimaumbile. Ni vilevile kuhusu kuacha usingizi kwa muda mrefu.

Katika hayo matukio mbalimbali ya pekee, baada ya uchunguzi wa makini wa tukio lenyewe, wa nafasi zake za kimwili, za kiadili na za kidini, mwili unaonekana kutolemea roho (inavyotokea mara nyingi) bali kuwa chombo chake kinachoiacha ionyeshe uzuri wake wa ndani, uangavu wa kumiminiwa na upendo motomoto. Mara kadhaa tunapewa ishara hizo za nje ili kuonyeshwa upande wa hisi kuwa maisha kamili ya Kikristo ni utangulizi wa uzima wa milele.

Tazama pia hariri

Viungo vya nje hariri

  Makala hii kuhusu mambo ya dini bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu mada hii kama historia yake au uenezi wake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.