Kaunti za Kenya

maeneo ya Kwanza ya kiutawala
(Elekezwa kutoka Magatuzi ya Kenya)

Kaunti za Kenya (en: Counties of Kenya) ni maeneo ya kiutawala ya Kenya tangu kuadhimishwa kwa katiba ya mwaka 2010[1].

Kaunti za Kenya.

Katiba hiyo inaeleza kuwepo kwa kaunti 47 nchini katika mafungu 191 na 192, pamoja na ‘County Governments Act of 2012”. Kaunti hizi zilichukua nafasi za Mikoa ya Kenya. Mipaka ya kaunti iliwekwa kulingana na mipaka ya wilaya za kenya zilizokuwa zimeanzishwa kisheria mwaka wa 1992.

Mipaka ya kaunti hizo ni pia msingi wa maeneo ya uchaguzi wa mwakilishi mwanamke wa kaunti, seneta na gavana. [2][3]

Serikali hariri

Utendaji katika Kaunti hariri

Utendaji wa kaunti una wajibu wa kutekeleza madaraka ya serikali ya kaunti. Gavana ndiye mtendaji mkuu na husaidiwa na naibu wa gavana. Kila kaunti ina kamati ya utendaji iliyoundwa na[4]:

  • Gavana
  • Naibu wa gavana
  • Kamati ya watu wasiozidi thuluthi ya wabunge wa kaunti au watu kumi, ambapo bunge la kaunti lina watu zaidi ya 30
  • Katibu wa kaunti

Kazi ya utendaji ni:

  • Kutekeleza sheria za bunge la kaunti
  • Kutekeleza sheria za kitaifa ndani ya mipaka ya kaunti
  • Kuendesha na kuratibu shughuli za utawala wa kaunti na idara zake
  • Kutayarisha miswada ya sheria na kuzipeleka katika bunge la kaunti
  • Kuwajibika kwa bunge la kaunti na wananchi wa kaunti

Bunge la Kaunti hariri

Kila kaunti ina bunge. Wajumbe huchaguliwa kutoka wadi za kaunti katika uchaguzi mkuu. Pia, kuna wajumbe wa kuteuliwa ambao huwakilisha vikundi vilivyotengwa, vijana na kwa ajili ya kusawazisha uwakilishi wa jinsia. Wajumbe hutumikia kwa muhula wa miaka mitano. Bunge huongozwa na spika ambaye hafai kuwa mjumbe.

Majukumu yake ni:

  • kuchuja na kuthibitisha waliopendekezwa kuteuliwa katika ofisi za umma katika kaunti
  • Kutengeneza sheria za kaunti
  • kuthibitisha bajeti na matumizi ya serikali ya kaunti
  • kuthibitisha mikopo ya kaunti
  • kuthibitisha mipango ya maendeleo ya kaunti
  • kuwajibisha utendaji wa kaunti

Orodha ya Kaunti za Kenya hariri

Namba Kaunti Mkoa wa zamani Eneo
(km2)
Wakazi
(Sensa 2009)
Makao Makuu
1 Mombasa (Kaunti) Pwani 212.5 939,370 Mombasa (Jiji)
2 Kwale Pwani 8,270.3 649,931 Kwale
3 Kilifi Pwani 12,245.9 1,109,735 Kilifi
4 Tana River Pwani 35,375.8 240,075 Hola
5 Lamu Pwani 6,497.7 101,539 Lamu
6 Taita–Taveta Pwani 17,083.9 284,657 Mwatate
7 Garissa Kaskazini-Mashariki 45,720.2 623,060 Garissa
8 Wajir Kaskazini-Mashariki 55,840.6 661,941 Wajir
9 Mandera Kaskazini-Mashariki 25,797.7 1,025,756 Mandera
10 Marsabit Mashariki 66,923.1 291,166 Marsabit
11 Isiolo Mashariki 25,336.1 143,294 Isiolo
12 Meru Mashariki 6,930.1 1,356,301 Meru
13 Tharaka-Nithi Mashariki 2,409.5 365,330 Chuka
14 Embu Mashariki 2,555.9 516,212 Embu
15 Kitui Mashariki 24,385.1 1,012,709 Kitui
16 Machakos Mashariki 5,952.9 1,098,584 Machakos
17 Makueni Mashariki 8,008.9 884,527 Wote
18 Nyandarua Kati 3,107.7 596,268 Ol Kalou
19 Nyeri Kati 2,361.0 693,558 Nyeri
20 Kirinyaga Kati 1,205.4 528,054 Kerugoya / Kutus
21 Murang'a Kati 2,325.8 942,581 Murang'a
22 Kiambu Kati 2,449.2 1,623,282 Kiambu
23 Turkana Bonde la Ufa 71,597.8 855,399 Lodwar
24 West Pokot Bonde la Ufa 8,418.2 512,690 Kapenguria
25 Samburu Bonde la Ufa 20,182.5 223,947 Maralal
26 Trans-Nzoia Bonde la Ufa 2,469.9 818,757 Kitale
27 Uasin Gishu Bonde la Ufa 2,955.3 894,179 Eldoret
28 Elgeyo-Marakwet Bonde la Ufa 3,049.7 369,998 Iten
29 Nandi Bonde la Ufa 2,884.5 752,965 Kapsabet
30 Baringo Bonde la Ufa 11,075.3 555,561 Kabarnet
31 Laikipia Bonde la Ufa 8,696.1 399,227 Rumuruti
32 Nakuru Bonde la Ufa 7,509.5 1,603,325 Nakuru
33 Narok Bonde la Ufa 17,921.2 850,920 Narok
34 Kajiado Bonde la Ufa 21,292.7 687,312 Kajiado
35 Kericho Bonde la Ufa 2,454.5 752,396 Kericho
36 Bomet Bonde la Ufa 1,997.9 730,129 Bomet
37 Kakamega Magharibi 3,033.8 1,660,651 Kakamega
38 Vihiga Magharibi 531.3 554,622 Vihiga
39 Bungoma Magharibi 2,206.9 1,375,063 Bungoma
40 Busia Magharibi 1,628.4 743,946 Busia
41 Siaya Nyanza 2,496.1 842,304 Siaya
42 Kisumu Nyanza 2,009.5 968,909 Kisumu (Jiji)
43 Homa Bay Nyanza 3,154.7 963,794 Homa Bay
44 Migori Nyanza 2,586.4 917,170 Migori
45 Kisii Nyanza 1,317.9 1,152,282 Kisii
46 Nyamira Nyanza 912.5 598,252 Nyamira
47 Nairobi (Kaunti) Nairobi (Mkoa) 694.9 3,138,369 Nairobi (Jiji)
581,309.0 38,610,097 Nairobi

Kazi ya Serikali hariri

Serikali za kaunti zina wajibu wa kutunga sheria katika mabunge ya kaunti na utendaji katika kaunti. Kazi ya kaunti kulingana na kiambatisho cha nne cha katiba ni:

  1. Ukulima, ikiwa ni pamoja na:
    • mimea na ufugaji wa wanyama
    • maeneo ya uuzaji wa mifugo
    • vichinjio vya kaunti
    • udhibiti wa magonjwa ya wanyama na mimea
    • uvuvi
  2. Huduma za afya
    • vifaa vya afya vya kaunti na maduka ya dawa
    • huduma za ambulensi
    • ukuzaji wa huduma msingi za afya
    • utoaji leseni na udhibiti wa shughuli zinazohusu uuzaji wa vyakula kwa umma
    • huduma za afya ya mifugo
    • makaburi, mochari na vifaa vya uchomaji maiti
    • kuondoa taka na maeneo ya kutupia taka
  3. Udhibiti wa uchafuzi wa hewa, kelele, kero zinginezo kwa umma na matangazo ya nje
  4. Shughuli za kitamaduni, burudani za umma na maeneo ya umma, ikiwa ni pamoja na:
    • kamari, kasino na aina nyingineyo ya kamari
    • mbio
    • utoaji leseni za pombe
    • sinema
    • maonyesho ya video na ukodishaji wake
    • maktaba
    • makumbusho
    • shughuli za michezo na utamaduni na maeneo yake
    • bustani, fuko na maeneo ya starehe
  5. Usafiri katika kaunti, ikiwa ni pamoja na:
    • barabara za kaunti
    • mataa ya barabarani
    • trafiki na maegesho
    • usafiri wa umma barabarani
    • feri na bandari, isipokuwa udhibiti wa mambo yanayohusiana na usafiri wa meli wa kitaifa na kimataifa .
  6. Udhibiti wa wanyama na ustawi wao, ikiwa ni pamoja na:
    • kutoa leseni za mbwa
    • maeneo ya malazi, utunzaji na uzikaji wa wanyama
  7. Uendelezaji wa biashara na udhibiti wake, ikiwa ni pamoja na:
    • masoko
    • kutoa leseni za biashara (isipokuwa udhibiti wa wataalamu)
    • shughuli za biashara zilizo haki
    • utalii wa ndani kwa ndani
    • vyama vya ushirika
  8. Upangaji wa kaunti na uendelezaji, ikiwa ni pamoja na:
    • takwimu
    • usoroveya wa ardhi na uchoraji ramani
    • mipaka na nyua
    • makazi
    • maelekezo ya usambazaji wa umeme na gesi na udhibiti wa nishati
  9. Elimu ya chekechea, vyuo vya ufundi vijijini, vituo vya ufundi na maeneo ya malezi ya watoto
  10. Utekelezaji wa sera maalum za serikali ya kitaifa kuhusu raslimali za kiasili na uhifadhi wa mazingira, ikiwa ni pamoja na:
    • uhifadhi wa udongo na maji
    • misitu
  11. Huduma za kaunti kwa umma, ikiwa ni pamoja na:
    • mifumo ya kudhibiti maji kutokana na kibunga
    • huduma za maji na usafi
  12. Huduma za zimamoto na udhibiti wa majanga
  13. Udhibiti wa dawa za kulevya na ponografia
  14. Kuhakikisha na kuratibu ushiriki wa jamii na kata katika utawala katika ngazi za mashinani na kusaidia jamii na kata zipate uwezo wa kitawala kwa sababu ya utekelezaji wenye ufanisi wa nguvu na kazi na ushiriki katika utawala katika ngazi za mashinani.

Marejeo hariri

  1. Article 6, Devolution and access to Services, The 2010 Constitution of Kenya
  2. Article 98, (1) (a), Membership of the Senate, the 2010 Constitution of Kenya
  3. Article 97, (1) (b) Membership of the National Assembly, The 2010 Constitution of Kenya
  4. "179. County executive committees". Kenya Law Reform Commission. 29 August 2012.