Wikipedia ya Kiswahili

toleo la lugha ya Wikipedia

Wikipedia ya Kiswahili (au Wikipedia kwa Kiswahili) ni toleo la kamusi elezo ya Wikipedia kwa lugha ya Kiswahili.

Wikipedia ya Kiswahili

Wikipedia ya Kiswahili ilianzishwa tarehe 8 Machi 2003, na tarehe 20 Aprili, 2024, imefikia makala zipatazo 79,969, idadi inayoifanya iwe Wikipedia ya 82 (kati ya 326 zilizo hai) kwa hesabu ya makala zote.[1].

Mwaka 2019 Wikipedia ya Kiswahili iliangaliwa mara 65,856 kwa siku, mwaka 2020 mara 73,056 na mwaka 2021 (Januari-Oktoba) 83,595 ambayo inakaribia kuwa sawa na mara 3,500 kwa saa. Mwaka huo kurasa zilizotazamwa zilikuwa 70,419,110, sawa na 192,929 kwa siku na 8,038 kwa saa. Mwaka 2022 idadi iliongezeka zaidi kwa kuwa kwenye mwezi Mei 2022 kurasa zetu zilifunguliwa mara 240,641 kwa siku[2].

Karibu nusu ya wasomaji wetu wako Tanzania[3], halafu Kenya, Marekani na sehemu nyingine duniani, kama India, Urusi na Nigeria[4].

Wikipedia ya Kiswahili ilikuwa inafunguliwa na 0,01% ya wanaofungua Wikipedia duniani kote mwezi Septemba 2018, ikiwa katika nafasi ya 65 kati ya lugha zote. Takwimu husika zinacheza kirahisi kama, kwa mfano, kutokana na habari zinazotangazwa na vyombo vya habari, watu wengi wanatafuta habari zaidi kwenye intaneti, maana Waswahili walioko Marekani si wengi sana, lakini wana urahisi wa kutumia intaneti, hivyo wanaweza wakawazidi watumiaji wa Tanzania ambako watu wengi bado hawana njia ya kutumia mtandao.

Mwezi huohuo, waliofungua Wikipedia nchini Kenya walikuwa 0,10% za wasomaji wote duniani; kumbe nchini Tanzania waliofungua Wikipedia walikuwa 0,04% tu za wasomaji wote duniani.

Mnamo Januari mwaka 2021 kati ya waliofungua Wikipedia nchini Tanzania, 14% waliifungua kwa Kiswahili. Kumbe nchini Kenya waliofungua Wikipedia ya Kiswahili walikuwa 4% tu, lakini kuna ongezeko kubwa, kwa sababu mnamo Septemba 2018, waliofungua Wikipedia nchini Kenya walikuwa 0,08% za wasomaji wote duniani; kati yao waliofungua Wikipedia ya Kiswahili walikuwa 1.7%. Kumbe nchini Tanzania waliofungua Wikipedia walikuwa 0,03% za wasomaji wote duniani, lakini kati yao 11.2% waliifungua kwa Kiswahili, asilimia inayozidi kukua kadiri makala zinavyoongezeka na kuwa bora zaidi.

Maendeleo

 
Ukurasa wa "Mwanzo" ulivyokuwa mwaka 2004.

Mnamo Julai 2006 Wikipedia ya Kiswahili ilifikisha makala 1,000 na tarehe 14 Septemba mwaka huohuo ilifikia makala ya 2,000.

Mnamo Julai 2007 ilifikisha makala 5,000 na tarehe 26 Septemba 2007, 6,000.

Tarehe 21 Aprili 2008, Wikipedia ya Kiswahili ilifikisha makala 7,000 na tarehe 19 Desemba 2008 ilifikisha makala 8,000, hasa baada ya kuanzishwa makala nyingi za mbegu za kata za Tanzania.

Makala za mbegu za Tanzania, ziliendelea kuisukuma Wikipedia ya Kiswahili hadi kufikia kiwango cha makala 9,000 tarehe 2 Februari 2009 na makala 10,000 tarehe 21 Februari 2009.

Ilipofika tarehe 9 Aprili 2009, Wikipedia ya Kiswahili ilifikia kiwango cha makala 11,000 na tarehe 25 Aprili 2009 ilifikia makala 12,000.

Mnamo tarehe 20 Juni 2009, Wikipedia ya Kiswahili ilibadilisha ukurasa wake wa mwanzo katika sura mpya.

Mnamo tarehe 17 Agosti 2009 ilifikia makala zipatazo 13,000, na kuendelea kuifanya iwe Wikipedia ya kwanza kwa ukubwa katika Afrika.

Haikushia hapo: tarehe 11 Septemba 2009, Wikipedia hii ilifikia makala 14,000 na tarehe 25 Desemba 2009 makala 15,000.

 

Tarehe 31 Mei 2010 ilifikia makala 18,000 na tarehe 21 Agosti mwaka huohuo makala 20,000.

Tarehe 28 Oktoba 2011 ilifikia makala 22,000.

Tarehe 15 Februari 2014 ilifikia makala 26,000 na tarehe 28 Oktoba mwaka huohuo makala 27,000.

Tarehe 25 Januari 2015 ilivuka idadi ya makala 28,000, tarehe 13 Juni 2015 ilifikia makala 29,000, tarehe 22 Septemba mwaka huohuo ilifikia makala 30,000 na kuendelea tena.

Upande wa maharirio, tarehe 10 Oktoba 2015 yamefikia idadi ya milioni 1.

Tarehe 10 Novemba mwaka huohuo ilivuka makala 31,000 na kupiku Wikipedia ya Kiyoruba.

Tarehe 13 Februari 2016 ilivuka idadi ya makala 32,000 na kusonga mbele kiasi cha kufikia 33,000 tarehe 18 Aprili 2016, halafu 34,000 tarehe 20 Agosti 2016 kwa makala Kinung.

Makala juu ya James Tate imeifanya itimize idadi ya 35,000 tarehe 12 Januari 2017. Mwaka huohuo, tarehe 20 Mei 2017 idadi ya makala ilifikia 36,000, tarehe 30 Julai ilifikia 37,000 kwa makala juu ya Ziwa Ambussel, tarehe 12 Oktoba 38,000 kwa makala juu ya mto Jubba na tarehe 24 Desemba ilifikia 39,000.

Tarehe 17 Machi 2018 mradi wa milima umeleta makala ya 40,000: Nidze. Mradi wa mito ya Tanzania umesukuma Wikipedia hii kufikia idadi ya makala 41,000 kwa ukurasa juu ya Mto Ligunga tarehe 2 Mei 2018 na 42,000 kwa ukurasa wa mto Jigulu tarehe 21 Mei.

Mradi wa mito ya Kenya umefikisha idadi ya makala kuwa 43,000 kwa ukurasa juu ya Mto Kaptarit tarehe 7 Julai 2018, kuwa 44,000 tarehe 30 Julai kwa ukurasa juu ya mto Nyairoko, kuwa 45,000 tarehe 12 Agosti kwa ukurasa juu ya Mto Ilangi, kuwa 46,000 tarehe 15 Oktoba kwa ukurasa juu ya mto Wakavi, tena kuwa 47,000 tarehe 8 Novemba kwa ukurasa juu ya mto Olkimatare.

Tarehe 7 Februari 2019 mradi wa visiwa vya Tanzania umevusha Wikipedia yetu katika elfu ya 48 kwa ukurasa juu ya kisiwa cha Musira.

Tarehe 23 Machi 2019 mradi wa Mito ya Uganda umevusha Wikipedia yetu katika elfu ya 49 kwa ukurasa juu ya mto Wangodugu, tarehe 3 Mei 2019 umeifikisha katika idadi ya 50,000 kwa ukurasa juu ya mto Ocere, tarehe 31 Mei umeivusha tena katika elfu ya 51 kwa makala juu ya mto Osia na tarehe 16 Julai umeifikisha idadi ya 52,000 kwa makala juu ya Mto Rwoho.

Tarehe 10 Agosti 2019 mradi kuhusu ugatuzi nchini Cote d'Ivoire umezaa makala ya 53,000 kuhusu Tarafa ya Tiémélékro. Tunawashukuru wachangiaji wetu kutoka nchi hiyo ya Afrika Magharibi.

Tarehe 4 Oktoba 2019 mradi kuhusu watakatifu wa Afrika umefikisha makala za Wikipedia hii katika idadi ya 54,000 kwa ukurasa juu ya wafiadini Suksesi na wenzake 17, na tarehe 13 Desemba 2019 mradi huohuo umefikisha idadi ya makala hadi 55,000 kwa ukurasa juu ya Yusto askofu.

Tarehe 10 Machi 2020 mradi wa Makabila ya Uganda umefikisha Wikipedia yetu kwenye makala ya 56,000 kwa ukurasa juu ya Wakumam.

Tarehe 17 Machi 2020 mradi wa wachezaji wa mpira wa miguu umefikisha Wikipedia yetu kwenye makala ya 57,000 kwa ukurasa juu ya Gilmar Rinaldi. Kurasa elfu kwa juma moja tu!

Tarehe 3 Aprili 2020 mradi wa mito ya Burundi umefikisha Wikipedia yetu kwenye makala ya 58,000 kwa ukurasa juu ya Mto Gihororo (Karuzi).

Tarehe 22 Mei 2020 mradi wa miji ya Rwanda umefikisha Wikipedia yetu kwenye makala ya 59,000 kwa ukurasa juu ya Mukarange.

Tarehe 20 Agosti 2020 mradi wa mito ya Burundi umefikisha Wikipedia yetu kwenye makala ya 60,000 kwa ukurasa juu ya Mto Rubirizi (Muramvya).

Tarehe 8 Novemba 2020 Wikipedia yetu imetimiza tena idadi hiyo (baada ya makala 907 kufutwa na steward fulani kwa mkupuo mmoja). Ukurasa husika ni juu ya mtakatifu Andrea Avellino.

Tarehe 15 Machi 2021 tumefikia makala 61,000 kwa ukurasa juu ya mtakatifu Agrikola wa Chalon.

Tarehe 7 Mei 2021 mradi wa miji ya Italia umefikisha Wikipedia yetu kwenye makala ya 62,000 kwa ukurasa juu ya San Giovanni Rotondo.

Tarehe 8 Juni 2021 mradi wa Africa Wiki Challenge Arusha kuhusu viwanja vya michezo umefikisha Wikipedia yetu hadi kutunga makala ya 63,000 na kusonga mbele haraka.

Tarehe 19 Juni 2021 Wikipedia hii imevuka makala ya 64,000 kutokana na tendo la kurudisha makala 907 lililofanywa na steward aliyekuwa amezifuta kwa mkupuo mmoja mwaka 2020.

Tarehe 5 Julai 2021 imefikia idadi ya 65,000 kwa makala juu ya Mwea katika mradi wa kata za Kenya na tarehe 14 Agosti 2021 imefikia idadi ya 66,000 kwa makala juu ya Makutano katika mradi huohuo.

Tarehe 9 Septemba 2021 imefikia idadi ya 67,000 kwa makala juu ya Nairagie Ngare katika mradi wa vijiji vya Kenya.

Tarehe 29 Oktoba 2021 imefikia idadi ya 68,000 kwa makala juu ya Chambishi katika mradi wa miji ya Zambia.

Tarehe 11 Januari 2022 imefikia idadi ya 69,000 kwa makala juu ya Maroua katika mradi wa miji ya Kamerun.

Tarehe 10 Machi 2022 imefikia idadi ya 70,000 kwa makala juu ya Ilesa katika mradi wa miji ya Nigeria.

Tarehe 23 Aprili 2022 Wikipedia hii imefikia idadi ya 71,000 kwa makala nyingi za mradi wa . Sasa kazi kubwa ni kuziweka sawa.

Tarehe 14 Mei 2022 imefikia idadi ya 72,000 na kusonga mbele. Bado kazi ya kuweka sawa makala nyingi zilizotungwa kwa mashindano.

Tarehe 6 Juni 2022 imefikia idadi ya 73,000 kwa makala juu ya Frenda, mji wa Algeria.

Tarehe 15 Julai 2022 Wikipedia hii imefikia idadi ya 74,000 kwa makala juu ya Ghuba ya Venezuela.

Tarehe 17 Septemba 2022 Wikipedia hii imefikia idadi ya 75,000 kwa makala juu ya Kouandé, mji wa Benin.

Tarehe 23 Desemba 2022 Wikipedia hii imefikia idadi ya 76,000 kwa makala juu ya Bouhjar, mji wa Tunisia.

Tarehe 25 Machi 2023 Wikipedia hii imefikia idadi ya 77,000 kwa makala juu ya Chomutov, mji wa Ucheki.

Tarehe 15 Juni 2023 Wikipedia hii imefikia idadi ya 78,000 kwa makala juu ya Jamil Adam katika mradi wa wachezaji wa mpira wa miguu.

Tarehe 9 Desemba 2023 Wikipedia hii imefikia idadi ya 79,000 kwa makala juu ya Chemchem (Unguja) katika mradi wa kata mpya za Tanzania.

Kati ya Wikipedia za Afrika

Kwa lugha zenye asili ya Afrika na visiwa vya jirani, Wikipedia kwa Kiswahili ndiyo ya nne kwa idadi ya makala zote ikifuatia Wikipedia ya Kiarabu cha Misri, ile ya Kiafrikaans na ile ya Kimalagasy. Kwa kuangalia yaliyomo halisi (bila makala mafupi sana) ndiyo ya tatu baada ya Kiarabu cha Misri na Kiafrikaans.

Pia ilikuwa ya kwanza kati ya Wikipedia za lugha za Niger-Kongo kuvuka kiwango cha makala 1,000. Sasa zimeongezeka, lakini ya Kiswahili bado inaongoza.

Wikipedia kwa Kiswahili ilikuwa ya pili katika Afrika nzima kuvuka kiasi cha makala 10,000 baada ya Wikipedia ya Kiafrikaans. [5]

Tazama pia

Marejeo

Viungo vya nje